Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Kwanza niungane na wenzangu kukupongeza sana kwa kuwa na hiki kiti kipya, Rais wa Mabunge ya Dunia, kwa kweli umekuwa ni mfano wa kuigwa na Watanzania tunajivunia sana. Tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili yako wewe mwananunu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuendelea kuwaletea maendeleo wananchi Watanzania wakiwemo Jimbo langu la Nyasa. Pia nawashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote wawili wa Mipango, pamoja na Fedha kwa jitihada kubwa wanazozifanya kutika kuhakikisha kwamba nchi yetu inakwenda vizuri kimaendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupongeza pia ni kuwatia watu moyo. Nawashukuru sana, Mheshimiwa Mkuu wangu wa Mkoa wa Ruvuma, Mheshimiwa Kanali Laban Thomas na Mkuu wangu wa Wilaya ya Nyasa Mheshimiwa Sanga, kwa kweli wanajituma sana. Mwenyezi Mungu awasaidie pamoja na wengine wote wanaowasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo jambo langu litajikita hasa kupitia mipango hii katika eneo la maendeleo jumuishi na hapo naangalia katika maendeleo endelevu ya mwaka 2030 lengo la tatu la afya pamoja na kuleta ustawi wa watu. Katika mipango hii inayoletwa mbele yetu, watu ndiyo kiini, watu ndiyo jambo kubwa kuliko jambo lingine lolote lile. Kwa hiyo, napenda kujikita hapo, na kwa sababu mipango inapendekeza kuangalia maendeleo jumuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nijikite katika suala la lishe. Nimejiuliza sana, mimi siyo mtaalam sana katika masuala ya afya, lakini kama mtu ambaye huwa napenda kulisikia jambo na kulifanyia mkazi, napenda kujiuliza sana, katika mikoa ambayo inaongeza kwa udumavu ni ile mikoa ambayo inaongoza kwa kilimo au kutoa chakula katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia mikoa hiyo nauona Mkoa wa Ruvuma upo ndani, Iringa upo ndani, Mbeya upo ndani, Njombe upo ndani, Katavi, Rukwa, hasa maeneo haya ya magharibi, sijui wenzetu wa Kigoma safari hii wameponapona vipi; Mtwara na wenyewe wapo kule kusini japo hawapo nadhani ni kwa ajili ya kula korosho na mbaazi, lakini najiuliza ni kwa nini mikoa ambayo inazalisha sana ndiyo inakua na udumavu uliopitiliza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imeanza kuzungumzwa siyo leo, toka miaka ya 2010 tumeanza kupata taarifa hizo. Nimefuatilia, tunapata majibu tu kwamba hawali mchanganyiko wa vyakula na nini. Najiuliza, mbona nikifika hapa Dodoma tunakula tu vile vile, tunafanana fanana? Tofauti ni nini? Nikaona pengine kuna suala lingine ambalo halijapata majibu na halijafanyiwa kazi. Mimi nimeanza kuunganisha udumavu na ukosefu wa miundombinu ya uhakika kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia upande huu wa magharibi ya nchi yetu kwa muda mrefu suala la miundombinu na mipango ya kimkakati ya kimaendeleo kidogo ilikuwa inaenda siyo sawa na maeneo mengine katika nchi. Kwa hiyo, inawezekana hiyo ikawa ni sababu. Nikiangalia sasa hivi hata tunapozungumzia reli, mchuchuma; reli itoke Mtwara mpaka Mbamba Bay hiyo tunaizungumza na msishangae tukafika miaka bado tunazungumza tu. Bandari ya Mbamba Bay tunazungumza tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukanda huu wa kuunganisha kutokea Mbamba Bay unakuja mpaka Ludewa mpaka Mbeya ambao ni nzuri sana kwa utalii ingeongeza uchumi, upo tu, hakuna barabara huko. Ndiyo maana maeneo hayo yote yamedumaa. Kwa hiyo, nilikuwa napenda kumwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Mipango, hebu tuangalie kwa kina, hili suala la udumavu katika mikoa hii niliyoitaja unatokana na nini? Ni kweli kula chakula tu? Kama ni chakula, ni kwa sababu gani huko tu ambako sisi tunazalisha zaidi? Kwa hiyo, iko haja ya kutafuta mambo mengine ya kina ya kusaidia mikoa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nategemea katika mpango wa maendeleo unaokuja, suala la udumavu litawekewa mkakati maalum ili kuhakikisha kwamba Taifa hili linatendewa haki kwa watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nafuatilia hata kwa watu ambao wamebahatika kupata ufadhili wa Benki Kuu wa kwenda kusoma. Nikisikiliza majina, kwa sababu ya ufaulu mkubwa nakuta majina hasa yanakuwa ya upande mmoja. Tunafurahi kwamba wachukuliwe waliofaulu vizuri, lakini yawezekana maeneo mengine huu udumavu ndiyo umechangia hata hawawezi kupata hiyo nafasi. Kwa misingi hiyo, hilo ni suala la hatari katika nchi. Ni lazima tupate jibu la uhakika kwa nini udumavu unaendelea kuwa katika mikoa hiyo hiyo miaka yote na siyo katika mikoa mingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimejiuliza hata kule Kagera, nao kwenye kiwango cha umaskini kila mwaka wanatajwa, lakini akina ushomire ndio wanatoka huko, kwenye udumavu pia wapo. Sababu ni zipi? Hatuwezi kuendelea kuwa na majibu rahisi. Ni lazima tuangalie kwa kina mikoa hii ambayo kila siku inatajwa kuwa ina udumavu, ipate majibu ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tunasema kwamba tunaanglia wananchi wetu waweze kuwa na ustawi wa afya njema, lakini pengine hizi shida zinatokea toka kwenye kuzaliwa kwao. Tumejitahidi tumejenga vituo vya afya vya kutosha, sasa hivi na watumishi tunapeleka, lakini suala la kujifungua haliishii tu kujifungua salama kwamba mama ana mtoto, mama yuko mzima wakati wa kujifungua. Anajifungua mtoto wa aina gani? Kuanzia tumboni mtoto aangaliwe lakini pia hata kwenye kujifungua, wapo wakunga. Sasa hivi tunapoajiri tunafanya kwa ujumla, nurse anaajiriwa kama nurse, lakini pengine hatuangalii wale wakunga. Ndiyo maana wakunga wa jadi bado wana heshima zao kwa namna wanavyowasaidia akina mama kwenye kujifungua na kuondoa changamoto kama hizo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Haya, ahsante sana.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba katika mfumo wetu wa utumishi uangalie Mkunga ana nafasi gani katika ajira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)