Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuhitimisha hoja ya upande wa Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema mtangulizi Kaka yangu Profesa Kitila, kama Serikali katika hatua hii na kama Kanuni zetu zinavyotutaka, tumepokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge. Tumewasikiliza na tutakuwa na kazi katika ngazi ya Serikali kufanyia kazi maoni ya Waheshimiwa Wabunge katika maandalizi ya bajeti ambayo itakuja mapema mwakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hatua hii nikushukuru wewe pamoja na Kamati na Wabunge wote kwa maoni waliyoyatoa kwa wingi na uzito mkubwa. Waheshimiwa Wabunge, tumewasikilza, tumeyapokea na kwa kweli sisi tuliokuwa tunawasikiliza, tuwahakikishie wapiga kura wenu kwamba wana Wabunge makini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa tumepokea, katika kuhitimisha naomba niseme mambo machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jambo la kwanza, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, kwa kuwa amefanikiwa kubadilisha kwa kiwango kikubwa kubadilisha kumbukumbu za Bunge na michango ya Wabunge katika kipindi cha sasa katika Wizara yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa Naibu Waziri katika Serikali ya Awamu ya Nne na nimekuwa kwenye Baraza Serikali ya Awamu ya Tano. Michango mingi ya Wabunge katika Bunge lako Tukufu yanapokuja masuala ya bajeti ilikuwa ni Wizara ya Fedha inakwamisha Wizara nyingine kwamba, fedha haziendi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kila Mbunge anakiri kupokea fedha nyingi sana za miradi ya maendeleo katika majimbo yenu. Kila mmoja, kila wilaya na hata panapokuwepo na mikutano ama vikao vya Wakuu wa mikoa ama Wakuu wa Wilaya, kila Mkuu wa Mkoa anakiri kupokea fedha nyingi katika maeneo yao ya utawala. Hizo ndizo kazi anazozifanya Mheshimiwa Rais anapokesha na anapozunguka huku na kule, nchi na nchi, bara na bara anatafuta fedha na zinamiminika katika miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo moja pekee kwenye upande wa bajeti ambalo limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge ni kuhusu usimamizi wa fedha zinapokwenda kwenye miradi hii ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili Mheshimiwa Rais alilitambua mapema tu. Alipoapishwa na wakati anaapishwa na kwenye Baraza la Mawaziri mara nyingi amekuwa akielekeza kuhusu usimamizi wa fedha za umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hatua ambazo zimechukuliwa ambazo Waheshimiwa Wabunge wameziongelea kwa kiwango kikubwa ambazo zinahusisha namna bora ya kusimamia fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ngazi ya Serikali na ngazi ya Wizara ya Fedha masuala haya ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyasemea, sisi tutaendelea kuyazingatia. Mheshimiwa Rais alielekeza tuimarishe nguvu ya Wakaguzi wetu, CAG pamoja na Mkaguzi wa Ndani ili wakague thamani ya fedha katika miradi yetu. Jambo hilo linafanyika na fedha zimeendelea kuongezewa kwa ajili ya Wakaguzi wetu ili wakague miradi ya maendeleo. Nitoe rai kwa viongozi wote Serikalini wakiwemo Maafisa Masuuli tufuatilie kwa ukaribu na tuchukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama ya utawala wa sheria ni kufuata utaratibu. Natamani hata mimi niende kama ambavyo maoni ya wananchi wengi na hata baadhi ya Waheshimiwa Wabunge waliliona kwamba lazima panapotokea jambo pachukuliwe hatua pale pale, lakini gharama ya utawala wa sheria ni lazima taratibu zifuatwe. Kwanza panafanyika ukaguzi, pili, panafanyika majibu kutoka kwa Maafisa Masuuli waelezee hoja zile zilizokuwa zimetolewa na hatua zinazofuata panatakiwa pafanyike uchunguzi na baada ya uchunguzi hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa. Hiyo ndio gharama ya utawala wa sheria. Rai yangu watendaji wote Serikalini katika ngazi zao wachukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muundo wa nchi yetu ni mzuri sana. Ukienda ngazi ya Wilaya ambako ndiko miradi inatekelezwa pana muundo mzima ule ambao uko katika ngazi ya Kitaifa, pale kwenye mradi pana Mkuu wa Wilaya kama ni ngazi ya Wilaya, pana Kamanda wa TAKUKURU, pana Kamanda wa Polisi, pana Idara, pana Upelelezi, pana Mahakama, pana wa kukamata na pana Magereza. Kila kitu kipo palepale mradi unapokamilikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hatuna haja ya kusubiri ziara za Viongozi Wakuu ili tuchukue hatua kwenye maeneo ambayo mradi haukutekelezwa vizuri. Kwa kweli kama darasa limejengwa vibaya, tukataka tusubiri Rais aje mpaka kwenye kijiji achukue hatua kwenye darasa ambalo lilijengwa vibaya, tutakuwa hatumtendei haki Rais ambaye ametutafutia fedha zimekuja na eneo ni letu na mradi ni wetu, lakini tumeshindwa kuusimamia na kuchukua hatua ama kuchukuliana hatua katika eneo husika. Kwa hiyo nitoe rai ngazi zote zinazosimamia miradi wasimamie ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hatua hii ya uandaaji wa Bajeti, hoja zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge tumewaelekeza Maafisa Masuuli wote wazingatie miradi inayoendelea, tuitengee fedha kama kipaumbele miradi inayoendelea ili tusiwe na matumizi mengi ya fedha zinazotumika nje ya bajeti au kuwa na miradi ambayo haina fedha katika bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameongelea suala la fidia, tumelizingatia, maeneo yote ambayo hayana mizozo, tutaendelea kulipa fidia. Tumeelezea habari ya maeneo ambayo yamechukuliwa kwa ajili ya EPZA, tumeelezewa maeneo ambayo Serikali imeyachukua kwa matumizi tofautitofauti kwa miradi ya maendeleo. Tutaendelea kulipa fidia kwa maeneo hayo ili kuweza kuhakikisha kwamba tunakwenda vizuri. Haya ni maeneo ambayo Taasisi zetu za Vyombo vya Ulinzi na Usalama vimechukua maeneo kwa ajili ya maendeleo, lakini kuna maeneo ambayo wananchi wanapisha miradi ya maendeleo ama kuna maeneo ambayo tunajenga miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo hayo ambayo tunajenga miradi ya maendeleo mathalani tumeenda tunajenga mradi wa umwagiliaji katika eneo lao, kama tumeondoa nyumba ya mwananchi atalipwa fidia lakini kama tunajenga Mradi wa Umwagiliaji katika eneo ambalo wananchi wale watalima kisasa wale ambao eneo lile unajengwa mradi wa umwagiliaji mathalani bwawa watapewa maeneo ya kulima. Watapewa maeneo ya kulima washiriki kwenye mradi ule wa umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusije tukakwamisha Miradi ya Umwagiliaji tukarudi kenye utaratibu wa kutegemea mvua kwa sababu ya kubishana kuhusu wapi tujenge mradi wa umwagiliaji. Hii ni teknolojia, ni ulimaji wa kisasa, unatuhitaji wote tujitoe kwa ajili ya kukamilisha hilo. Kwenye maeneo haya niliyoyasema ambayo yanachukuliwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo nilimsikia Mbunge wa Segerea akiongelea fidia yao ya eneo la Kipunguni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishafika eneo lile na tuliwatangazia wananchi kwamba tunataka tuanze kulipa mwezi Septemba. Kilichotuchelewesha kama ambavyo Mbunge ameongea kwa hisia si kwamba fedha ilikosekana ya kulipa fidia hiyo, isipokuwa ilipofanyika uhakiki iligundulika kati yao miongoni mwao kuna ambao tayari walishapewa maeneo mengine lakini majina yao yalikuwepo tena kwenye fidia kwa maana hiyo ingeweza kuwa kulipa fidia mara mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wengine tuliposema tunataka kuanza kulipa, wakawa hawajaridhika na fidia inayotakiwa kulipwa, kwa maana hiyo ilibidi ufanyike utaratibu wa kuweza kulimaliza hilo ili masuala ya kulipa yaweze kuendelea. Kwa hiyo tutaendelea kulipa, tunaamini kwamba baada ya kuwa tumeshamaliza mzozo huo ndani ya mwezi mmoja ama mwezi mmoja na sehemu hivi tutaenda kwenye utaratibu wa kulipa hili likiwa linahusisha Kipunguni pamoja na maeneo mengine ambayo yalikuwa na kesi ya aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liliongelewa pia jambo la masuala ya mifumo tumeshapokea, kazi inaendelea, sasa hivi tunaweka automation kwenye masuala ya mifumo ya upande wa Forodha, tutaendelea na mifumo kwenye upande wa kodi za ndani na tutaendelea na mifumo kwa upande wa makusanyo mengine ili maelekezo ya Mheshimiwa Rais yanayohusisha mifumo yaweze kutekelezwa kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kumalizia, mwenzangu mtangulizi wangu ameongelea suala la kilimo na amegusia pia na masuala ya uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti pamoja na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote, kuna hili suala la suala la mifugo. Naomba tukubaliane kwamba mambo yamebadilika sana na jambo hili halihitaji taharuki katika kulishughulikia. Sote tunakubaliana kwamba hatuwezi kudiriki kutangaza kwamba ufugaji katika nchi yetu ni jambo la hatari, wote hatuwezi tukadiriki kufanya hivyo. Ufugaji na mifugo ni mali na ni utajiri wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wengine sisi tuliotokana na jamii hizi za kifugaji tunajua, mifugo inakuwa sehemu ya familia na mifugo ina majina mengine yana majina ya mjomba, wengine shangazi ni sehemu ya familia na mtu akichukua mifugo ni kama vile ameteka watoto wako ni kama vile ameteke sehemu ya familia yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hatuwezi tukatangaza nchi hii kwamba itakuwa ya mifugo tu, utaratibu tuliokuwa tunatumia kufuga zamani, sasa hivi unaendelea kuwa mgumu na tunakokwenda utaendelea kuwa mgumu zaidi. Kwa hiyo ni lazima tukubaliane tena bila taharuki utaratibu mpya ambao tutatumia kulima, utaratibu mpya ambao tutatumia kufuga na utaratibu tutakaotumia kujenga. Hivi vitu vitatu kwa sababu uwingi wa watu unaongezeka, uwingi wa mifugo unaongezeka, mahitaji ya kulima yanaongezeka, hivi vitu vitatu kwa uchache wake lazima vyote viweze kubadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mimi nikichunga ilikuwa ukiamka ukishakula, wewe ni kupiga mluzi tu na kuwahimiza, tulikuwa tunaongea tunaelewana na mifugo, ukiamka tu hapa unasema wochage mapembe bije, ukishafungulia mlango unaachilia siku nzima mpaka mkishaona mmechoka jua linaelea, mnarudi tena lakini sasa hivi mazingira hayo yanaenda hayawezekani. Kwa hiyo ni lazima tuwekeze kwenye ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi yetu vitu vingi vizuri tunavifanya kwa kuonesha. Ukienda kwenye Maonesho ya Nanenane ukaiona mifugo ile, ni mifugo ambayo inapatikana na kwingine kote duniani. Ukishamaliza maonesho imeisha hiyo, ukienda kwenye kilimo hivyohivyo, vitu unavyoviona kwenye maonesho ni bora sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili tuweze kukabiriana na huku kupungua ama kuongezeka kwa mpambano wa matumizi ya ardhi, ni lazima hivi vitu ambavyo huwa tunavionyesha kwenye Maonesho ya Nanenane ndiyo uwe mtindo wa maisha. Maana yake tutapata wingi uleule kwa ubora, tutapata mahitaji yaleyale kwa kiasi kidogo lakini kwa ubora mkubwa, hiyo itatusaifdia katika matumizi ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongea na wenzetu wa Wizara ya Mifugo na tumeongea na wenzetu wa Wizara ya Kilimo na Mheshimiwa Rais ametoa hayo maelekezo. Tuwawezeshe wenzetu hawa wa hizi sekta ili kuweza kufanya hizo transformation ambazo ndio itakayotoa majawabu ya moja kwa moja ya kupunguza huu ushindani wa matumizi ya ardhi. Hizi sekta zote ni za muhimu katika nchi yetu na ni sekta za kihistoria na vilevile tunaendelea kuongea na wenzetu wa Wizara ya Ardhi kuangalia pia mjengo wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaendelea kujenga huu mjengo tunaotumia kwa huu mtawanyiko mkubwa, sasa hivi kwa sensa hii tuliopewa ukiongeza miaka 20 miaka 30 ijayo tutaelekea milioni 200, kwa mjengo huu tunaoenda nao kwanza mkumbo singalila, kama majani yale yanayotambaa hayaendi juu. Hii nchi yote itakuwa na maeneo ya makazi. Tutakosa maeneo ya uzalishaji, hatutakuwa na eneo la kulima, hatutakuwa na eneo la kufugia. Kwa hiyo ni lazima na hilo na lenyewe tumeendelea kuongea huko tunakokwenda mbele tuendelee kuliwekea utaratibu ambao utasaidia kukidhi mahitaji makubwa yanayohitajika ya matumizi ya ardhi, huku ukiruhusu shughuli nyingine za kimaendeleo ziendelee kufanywa na wananchi wetu kujipatia kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Waheshimiwa Wabunge, tumepokea yale yaliyokuwa yanahusiana na Majimbo yenu, hatuwezi kutaja mmojammoja, kila Mbunge ametaja baadhi ya mambo ambayo yanahusu miradi inayoendelea na mahitaji ya fedha katika sekta za huduma za jamii, miundombinu pamoja na maeneo mengine. Mchango wa kila mbunge tumeuchukua na tulikuwa tunaongea hapo na Waziri wa TAMISEMI, tumeyachukua na tukishamaliza Bunge hili hiyo ndiyo itakayokuwa kazi tutakayoenda kuifanya ili kuweza kuhakikisha tunapokuja Bunge la Bajeti tuweze kutoa taarifa hiyo ya utekelezaji wa maeneo hayo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyasemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa mara nyingine na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, naomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)