Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Kuazimia Kuwahamisha Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hoja ya Kuazimia Kuwahamisha Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuja kuhitimisha hoja yangu. Moja ya urithi alioniachia marehemu baba yangu Askofu Mwenisongole alioniachia ni kusema ukweli hata kama huo ukweli unakuathiri. Leo hii tunaweza tukajibu hoja hii kwa ushabiki na tunaweza tukatoa hii hoja kama hatuoni tatizo lakini ukweli utabaki kama ukweli tuna matatizo makubwa ya ushirika nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ilikuwa ni ndogo, anayetoa maono, sera na mipango ni Wizara ya Kilimo lakini yule afisa wa chini ambaye anapaswa kutekeleza maono, mipango na yote yuko chini ya TAMISEMI. Iwapo mipango hiyo itaenda vyovyote Waziri wa Kilimo hana uwezo wa kumhoji au kumuwajibisha na mifano iko wazi kila mahali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Simiyu Afisa Ushirika alikamatwa anapora kwa bastola, lakini mpaka leo yupo kazini kwa sababu tu TAMISEMI wameshindwa kumshughulikia, licha ya Tume ya Ushirika kusema huyu mtu hatufai. Tukija Mbozi ni madudu matupu pale ushirika, ukienda Mbinga hivyo hivyo, Mwanza kila mahali na hatuoni huko TAMISEMI kuwachukulia hatua ndiyo maana tukaomba kwamba hawa Maafisa Ushirika warudi Wizarani ambayo inajua taaluma zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ilikuwa ni hiyo, siyo kwamba tulitaka kuharibu D by D bali tulitaka kuiimarisha kuwafanya hawa Maafisa Ushirika wawajibike kwa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge, wakati anahitimisha Bajeti, Waziri wa Kilimo alitoa agizo hapa Bungeni kuwazuia Vyama vya Msingi kukopa. Kwa masikitiko, Vyama vya Msingi bado vinachukua mikopo na Maafisa Ushirika wanawasainia hiyo mikopo na hiyo mikopo haiendi kwa washirika badala yake viongozi wa ushirika wanakula kwa kushirikiana na washirika na Mheshimiwa Bashe hana uwezo wa kuchukua hatua kwa sababu wale wako TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo uende kwa Mheshimiwa Mchengerwa uanze kumwambia habari za ushirika, haelewi kitu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, anayejua hayo ni Mheshimiwa Bashe. Kwa hiyo, hoja yangu ilikuwa hapo, kuwaomba hawa Maafisa Ushirika wawe chini ya Wizara ya Kilimo hata tunapozungumza Bajeti ya Kilimo tunajua hawa watu tumekukabidhi, Maafisa Kilimo, Maafisa Ushirika ambao unawasimamia. Hata hivyo, namshukuru Waziri kwamba ametambua changamoto na ametuomba tumpe muda aje na hiyo Sheria. Kwa hiyo usiku wa deni hauchelewi kuisha, sisi wakati wa Bajeti tutamkamata, ametuomba muda na mimi kama mtoa hoja nipo tayari kutoa muda kwa Serikali kulichakata hili suala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge wote tunajenga nyumba moja na wote tunataka mkulima wetu afaidike na mazao yake.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, hoja gani?

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, namalizia, naomba kutoa hoja kukubaliana na maombi ya Serikali kwamba tuipe muda itimize wajibu wake. (Makofi)

SPIKA: Ngoja kwanza, Waheshimiwa Wabunge. Subirini kwanza Waheshimiwa…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge hoja iliyoko mezani, kwa sababu ni lazima Taarifa zetu Rasmi za Bunge zikae sawa. Hoja iliyoko Mezani na ambayo iko mbele ya Bunge ni Hoja ya Kuwahamishia Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo. Hiyo ndiyo hoja iliyoko mbele ya Bunge. Kama Mbunge nataka nikuongoze vizuri ili ujue ni hoja gani unaitoa.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, sawa.

SPIKA: Ukisema unatoa hoja na ulikuwa unasema unaungana na Mheshimiwa Bashe hiyo kutoa ina sura mbili. Moja, unaiondoa hii hoja yako?

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, hapana.

SPIKA: Ama unaitoa, yaani umebadilisha hii hoja yako tuichukue ile hoja ya Serikali ndiyo tuiweke, ndiyo unayotaka Bunge lihojiwe kwa hiyo. Kwa sababu kama unaiondoa hoja maana yake Bunge hatutalihoji. Kama hoja yako bado ipo hii ndiyo tuliyonayo hapa mezani…

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ndiyo hiyo ipo.

SPIKA: Kama unaibadilisha ndiyo useme sasa umebadilisha hii hoja kwa sababu…

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, hapana.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge tusikilizane kidogo kwa sababu mambo haya kama halijawahi kutokea siyo jambo rahisi sana kujua ule utaratibu. Sasa kama hoja yako hii unairekebisha ili uchukuliane na ile hoja iliyotoa Serikali ya kwenda kutengeneza sheria maana yake hapa hii ya kwako unaiondoa kwenye Taarifa Rasmi za Bunge hoja hii itakuwa ni ile pale, yaani ni ya kwako bado lakini umeibadilisha kwamba Serikali sasa ika…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane, nadhani Mheshimiwa Mbunge umenielewa ili ujue ninapoitoa kwa Wabunge kuwahoji ili hoja hii ifungwe, nataka nijue niwahoji hoja ipi? Hii uliyoleta mwanzo ama iliyorekebishwa na Serikali ambayo bado itakuwa ni ya kwako.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Hoja yangu ni hii, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Kilimo amesema kwamba wanaandaa Sheria kwa kushirikiana na TAMISEMI kuweka mazingira mazuri ya kuwasimamia hawa Maaafisa Ushirika na hii ndiyo ilikuwa ndiyo lengo la msingi la hoja yangu kwamba hawa Maafisa Ushirika wawajibike rasmi kule chini. Kwa maana hiyo ni kwamba nipo tayari kuipa muda Serikali, hoja yangu ni hiyo, kukubaliana na hoja ya Serikali. (Makofi)

SPIKA: Haya, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge nitakapowahoji Mheshimiwa mtoa hoja ameirekebisha hoja yake ya mwanzo. Badala ya kuwa hoja ya kuwahamishia Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo, sasa hoja yake pamoja na kwamba maelezo ni haya haya, hoja yake iliyoko mezani ambayo inaletwa Bunge liamue ni hoja inayohusu Serikali kutunga Sheria ili kuleta ufanisi kwenye utendaji kazi wa Maafisa Ushirika. Ndiyo hoja itakayotolewa kwenu. Sasa Mheshimiwa Mbunge baada ya kusema hayo sema unatoa hoja. (Makofi)

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, naafiki.

SPIKA: Haya Waheshimiwa Wabunge hoja ya Mheshimiwa George Mwenisongole imeungwa mkono. Unaweza kurejea kuketi Mheshimiwa Mbunge, ahsante sana. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge sasa nitawahoji Wabunge kuhusu hoja iliyorekebishwa ya Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole. (Makofi)