Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi kwa kunipa nafasi ili nichangie kwenye mpango wetu huu wa mwaka 2024/2025. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya yeye pamoja na wasaidizi wake Mawaziri na Manaibu Waziri, wanafanya kazi nzuri na kubwa kuhakikisha kwamba maendeleo yanawafikia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inaongozwa na dira na mipango ya miaka tofauti tofauti. Kuna mipango ya miaka mitano, miaka kumi na tano, miaka 30 na mpaka miaka 60. Hii mipango ya mwaka mmoja mmoja ambayo tunajadili hapa kwenye Bunge kila mwaka ningependa niishauri Serikali walau iwe inangalia mambo current zaidi ili tuweze kuisaidia nchi yetu. Kwa nini nasema hivi, mwaka jana taifa letu limepitia mchakato wa Sensa ya Watu na Makazi iliyoongozwa kwa ushupavu mkubwa sana na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya mwanzo ya Sensa hii ilitoka Oktoba, mwaka jana lakini mpaka sasa tunapozungumza final report bado haijatoka. Sasa tunazungumza mpango ambao ndiyo wa kwanza tangu tufanye Sensa hii. Sisi kama Wabunge, bila hii final report tunashauri vipi Serikali namna ya kuboresha mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana ni muhimu hii mipango ya mwaka mmoja mmoja iangalie vitu current. Tumetumia zaidi ya bilioni 400 kufanya Sensa hii. Sasa, tija ya fedha hizi itaonekana kwa namna gani? Tunatumia ripoti hii kupanga mipango ya muda mfupi na muda mrefu ya nchi yetu. Naishauri Serikali iangalie namna final report ije ili Waheshimiwa Wabunge waishauri Serikali kama inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kwenye Sensa hii tumeona kwamba kuna idadi ya watu kiasi gani, wanawake kwa wanaume kwa kila mkoa. Kuna mikoa yenye watu wengi na kuna mikoa yenye watu wachache. Kwa mfano, Mkoa wa Njombe una watu kama laki nane na kitu tu. Kuna Mkoa wa Dar es Salaam ambao tunaongelea una watu zaidi ya milioni tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango lazima iende tofauti kwa sehemu na sehemu. Pia, ninavyosema tuongelee mipango current, namaanisha; siku Serikali nyingi tumeona, Rais wetu na wasaidizi wake wamesaini mkataba mzuri na mkubwa sana wa Bandari ambao unakwenda kufanya na kuleta mageuzi makubwa sana ya kiuchumi nchini kwetu. Hata hivyo bado mpango wetu haujaweza ku-incorporate zile financial implications ambazo zitaletwa na mkataba huu. (Makof)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pia, kuna mikataba au miradi mikubwa sana ambayo inaendelea kwenye nchi yetu ambayo tunategemea ndani ya miaka hii 2024/2025 ikamilike na itakuwa na financial implications kubwa sana kwenye nchi yetu la. Mpango haujatuonyesha, naongelea kwa mfano, Bwawa la Mwalimu Nyerere, tumekuwa tukisubiri mradi huu kwa muda mrefu na tumepewa matumaini na Serikali yetu na niipongeze sana kwamba mradi huu unakwenda vizuri na unakwenda kukamilika. Faida za mradi huu na financial implications zake tuzione kwenye mipango yetu ili tuone namna gani tunasonga mbele kwanzia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Prof. Kitila Mkumbo akiwa bado Mbunge alikuwa anazungumzia sana Mradi wa Liganga na Mchuchuma. Sasa amekabidhiwa kijiti, ninashukuru na kumpongeza kwa sababu nimeona kwamba kwenye mpango wake anaona haja ya Serikali kuanza kufanyia kazi mradi huu. Nadhani kuna haja, tofauti na sentensi hii tu aende mbele zaidi kushauri kama alivyokuwa anashauri akiwa amekaa pale; kwamba ni namna gani anafikiri tuende sasa na mradi huu ili ulete tija kwenye taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango ni mzuri sana lakini kwa bahati mbaya ninahisi, kaka yangu Mheshimiwa Prof. Kitila amewasahau vijana kwenye mpango huu. Kwa nini nasema hivi, nizungumzie suala la changamoto ya upatikanaji wa mitaji kwa vijana. Tukiwa tunazungumzia takwimu ambazo zililetwa na Wizara yetu ya Kilimo, ikiwa inaonyesha justification za Mradi wa BBT; ilionyesha kwamba vijana zaidi ya 16 million kwenye nchi yetu, wanawake kwa wanaume wana changamoto ya kupatikana kwa mitaji. Yaani hawana accessibility ya financial institutions zile kubwa kwa maana ya mabenki na hizi ndogo ndogo kwa ajili ya kijipatia mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru na kuiopongeza sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, kwa sababu iliona haja na changamoto hii ikaleta mpango wa 4:4:2 au mikopo ya asilimia 10 kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa sababu aliiona changamoto ambazo makundi haya maalum yanapitia kwenye halmashauri zetu na akatoa maelekezo ya mfuko huu. Hiki kitu kilifanyika Aprili mwaka huu, mpaka leo tunavyozungumza ni miezi saba na hakuna hatua ambayo tumeiona kwa macho ikifanyika kuonyesha kwamba kweli mfuko huu utarudishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema Justice does not have only to be done. It should be seen to be done. Serikali inatuambia kwamba inafanyia kazi mchakato huu. Ninakataa kuamini kwamba, mfuko huu tayari uko kisheria. Vyanzo vya fedha za mfuko huu zinajulikana lakini maelekezo ya Mheshimiwa Rais yalikuwa mahususi, fedha hizi zipitie kwenye benki. Haimaanishi tunaanzisha benki mpya ili tukae muda mrefu namna hii, ni benki hizi hizi tulizonazo. Ninakataa kuamini kwamba, Serikali hii yenye wataalam wengi wa kutosha wanaofikiri vizuri, wanahitaji zaidi ya mwaka mzima kuweza kuja na mpango huu kwa ajili ya vijana…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. NG’WASI D. KAMANI: … lakini, kitendo cha kwamba mpango huu haujataja jambo hili unamaanisha kwamba vijana tusiwe na matumaini…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ng’wasi, samahani kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Festo Sanga.

TAARIFA

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye pendekezo la Mheshimiwa Rais kutumia benki, in a records taifa letu limewahi kutumia DCB Bank kwenye ya Dar es Salaam na kwenye records hawajawahi kuwa na upotevu wa fedha kwa kiwango ambacho sasa zimepotea. Kwa hiyo, Serikali ina delay lakini ina sehemu ya kwenda kujifunza DCB Bank na kuchukua hatua na kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais.

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Ng’wasi, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii na inazidi kuonyesha ni namna gani it is unjustifiable kwa Serikali kukaa muda mrefu namna hii bila kuleta utaratibu hii na vijana wakaendela kutumia fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema, kitendo cha Profesa Kitila kutoku-incorporate katika mpango wake namna gani fedha hizi zitaenda kurudi kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu ina maanisha kwamba tuondoe matumaini katika kipindi hiki cha 2024/2025 kwamba mfuko huu utarudishwa na fedha hizi zitarudi kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani mpango huu Mheshimiwa Kitila unapokuja kutujibu katika mrejesho wako wa mwisho, utuambie namna gani fedha hizi zinakuja kwenda katika channels zinazotakiwa na ziwafikie walengwa. Mheshimiwa Kitila, kwa nini nasema hivi, vijana wanawake kwa wanaume, ndiyo asset kubwa na nzuri ya nchi yoyote ambayo inajielewa katika dunia hii. Ni kwa sababu vijana ndiyo tunategemea watakuja kuwa wazazi waliobora baadaye, walezi waliobora baadaye, viongozi waliobora baadaye lakini wafanya maamuzi katika taifa hili. Kama tusipoanza kuwawezesha leo, ninaamini tunatishia kesho zilizo salama za taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka kusema kitendo cha kuchelewesha mikakati ya kuhakikisha vijana wanapata mitaji katika nchi hii kina multiplying effects. Effect ya kwanza ambayo mimi ninaiona na immediate kabisa na imepigiwa kelele na baadhi ya watu ni issue ya gambling, tunaiita kamari. Vijana wengi sasa wameishia kwenye kucheza kamari. Na tafiti za msingi zimefanyika kwamba, Kamari iwe ni online, iwe ni hizi tunaita sports betting zote zina implications kwenye psychology ya kijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, implication yake kiutafiti ni kwamba, mtu wa kawaida anatakiwa aonyeshwe namna gani anahitaji kukifanyia kazi kitu ambacho anataka kukipata. Hata maandiko yamesema asiyefaya kazi na asile. Lakini Kamari zinajaribu kumuonyesha kijana kwamba kuna njia nyepesi zaidi za kupata kitu kilichokikubwa zaidi. Changamoto ninayoiona hapa ni kwamba, tunaenda kuzalisha watu ambao wataona kwamba wana haja ya kuona namna ya kurahisisha mazingira yao ya kupata fedha. Mtu huyu ukimpeleka kwenye utumishi wa umma huwezi ukamwambia akae afanye kazi asubuhi mpaka jioni, siku saba, mwezi, miaka ili apate kitu fulani ilhali anaona kuna njia nyepesi ya kuweza kufanya ili apate kitu kilichokikubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi naona kwa kuendelea kuchelewesha haya, tuna-multiply effect kubwa sana. Siyo ya leo tu ya vijana wetu lakini kesho ya taifa letu. Nadhani ni wakati sasa tuchukue hatua, tufanyie kazi shida ya upatikanaji wa mitaji kwa vijana pamoja na kupuunguza changamoto ya ajira. Tunajua kwamba Serikali haiwezi ikaajiri vijana wote lakini tukiwapatia mitaji, tukiwatengenezea mazingira yaliyobora; tunaenda kuzalisha taifa lenye vijana ambao kesho taifa letu litakuwa na nguvu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, Profesa Kitila nakuomba, mjadala wetu wa mpango umetanguliwa na mjadala wa Ripoti ya CAG. Nilichangia mwaka jana, nikashauri kwamba tunahitaji kutengeneza sheria mpya ya uwajibikaji wa watumishi wa umma. Lakini kwa sababu mpango huu tunataka tuuone uki-reflect kwenye uchumi wa nchi yetu, na moja kwa moja Ripoti ya CAG ilikuwa inaonyesha namna gani uchumi wetu unadhidi kuathiriwa na matendo ya baadhi ya watumishi wetu, ninadhani kuna umuhimu mpango wako ukaonyesha namna gani unakwenda kufanyia kazi changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kutengeneza mipango ya bajeti ya trilioni 47 tunayoizungumzia sasa ilhali hatujarekebisha changamoto ambazo tumetoka kuzijadili juzi. Maana yake ni kwamba, tunategeneza mazingira yale yale ya viwango vikubwa zaidi kuendelea kupotea kadiri tunavyozidi kuongeza bajeti. Nadhani tutakuwa hatuendi vizuri kama taifa kama tunadhani kutatua changamoto zetu ni kuongeza ukubwa wa bajeti bila kuziba kunakovuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukabaki na bajeti zetu ndogo lakini kama fedha inakwenda kule inakostahili na inatumika vuzuri, bado tukapata maendeleo makubwa kuliko kuwa na bajeti kubwa ambazo zina mianya mingi zaidi inayovuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)