Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia hoja zilizoko mezani. Kwanza kabisa nadhani sote tutakubaliana kwamba, Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, anafanya kazi kubwa sana ya kutafuta fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo, kwa ajili ya kutuletea maendeleo kwenye Taifa hili. Kwa hiyo, kuna kila sababu ya kuhakikisha fedha hizi zinakuwa na tija katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye ukurasa wa 11 wa Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) utaona kwamba, wamebaini upotevu wa fedha nyingi ambao unatokana na dosari katika usimamizi wa ukusanyaji wa mapato. Mfano, ukiangalia, katika mwaka 2021/2022, TRA imerekodi nakisi ya bilioni 887.3 katika ukusanyaji wa mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye ukurasa wa 10 kwenye Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) utaona kwamba, wametoa taarifa na wameainisha kuwepo kwa mifumo dhaifu ya ukusanyaji wa mapato ya ndani pamoja na kushindwa kukusanya madai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano ni katika mwaka 2021/2022, kuna upotevu wa bilioni 11.07 zilizokusanywa na mashine za ukusanyaji wa mapato (POS) ambazo hazikuwasilishwa benki. Sasa kwanza, tunataka fedha hizo ziwasilishwe benki, hiyo ndio hatua ya kwanza. Hatua ya pili, tunataka wote waliohusika na ubadhirifu huu wachukuliwe hatua. Watanzania tunataka kuona hatua inachukuliwa, hii ni jinai, huu ni ubadhirifu, tunataka tuwaone wako katika mikono ya sheria wabadhirifu wa fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende mbele tutengeneze Suluhu ya kudumu. Tunahitaji kutengeneza na tuendelee kuwekeza katika kutengeneza mifumo imara ya kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato, lakini katika manunuzi ya umma. Nafahamu Serikali imefanya jambo kubwa sana katika eneo hili, lakini tunahitaji kuwekeza zaidi. Hii mifumo iwe inasomana kwa sababu, tukifanikiwa kutoa mkono wa binadamu katika makusanyo ya mapato na katika manunuzi ya umma, basi, tutafanikiwa kwa kiwango kikubwa kusaidia kuondoa au kupunguza kwa kiasi kikubwa upotevu wa fedha za umma, rushwa, lakini pia, tutakuwa tumeongeza uwazi katika matumizi ya fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 10 cha Sheria ya Public Audit Act kimefafanua majukumu ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG). Kwa hiyo, pamoja na majukumu yake ana jukumu kubwa la kufanya ukaguzi wa hesabu za Serikali kwa niaba ya Bunge. Kwa hiyo, CAG kimsingi ni jicho la Bunge katika kuisimamia Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kazi hizi za CAG mara nyingi kazi yake yeye anayoifanya CAG ni post mortem, yaani anakuta ubadhirifu ulishafanyika, fedha zilishapotea, wezi walikwishaiba kwa hiyo, yeye anatoa ripoti anaiwasilisha kwa hiyo, kazi yake inakuwa imeishia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu muhimu sana anaitwa Mkaguzi wa Ndani. Mkaguzi huyu wa Ndani ni mtu muhimu sana, hii Ofisi ya Mkaguzi wa Ndani ni ofisi muhimu sana ambayo inahitaji kuwezeshwa kwa sababu, Mkaguzi wa Ndani anaweza kuzuia upotevu wa fedha. CAG anakuja kutoa ripoti, kuripoti ubadhirifu wa fedha, matumizi mabaya ya fedha, lakini huyu Mkaguzi wa Ndani ana uwezo wa kuziwia ubadhirifu wa fedha kabla haujatokea au kabla haujafika mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kila mwaka Ripoti ya CAG inaletwa kwenye Kamati inajadiliwa, inakuja Bungeni, tunatoa maazimio, mwaka unaofuata tunaenda hivyo hivyo, lakini sasa ili kutengeneza suluhu tumwezeshe huyu mkaguzi wa ndani. Niipongeze Serikali katika eneo hili kwa sababu, katika kipindi cha bajeti, Mkaguzi wa Ndani ameweza kuanzishiwa Fungu Na.6 kwa hiyo, amewezeshwa kibajeti. Hapo awali tulikuwa tunaona changamoto, huyu Mkaguzi wa Ndani, kwa mfano, kwenye Halmashauri, alikuwa anategemea fedha ya kufanya kazi zake kutoka kwa Mkurugenzi na Mkurugenzi ndio huyohuyo anayekaguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukikuta kwamba, Mkurugenzi na yeye ni sehemu ya ubadhirifu, maana yake anatengeneza mazingira magumu ya Mkaguzi wa Ndani kufanya kazi. Atasema hamna fedha, atasema hamna gari, mara gari halina mafuta, lakini kwa kuanzishwa kwa Fungu Na.6, hili imeweza kusaidia kumuwezesha Mkaguzi wa Ndani kufanya majukumu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa twende mbali kwa sababu, Ripoti ya Mkaguzi wa Ndani inaishia kwenye Menejimenti. Sasa Menejimenti yenyewe ndiyo hiyo hiyo mara nyingi ndiyo inayotuhumiwa kwa ubadhirifu. Kwa mfano, katika Halmashauri. Mkaguzi wa Ndani akileta ripoti katika Menejimenti ndio hao hao watuhumiwa wanaokaa kupokea hiyo ripoti. Unategemea nini kitafanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Ripoti ya Mkaguzi wa Ndani wa Serikali iende mbali zaidi. Tutengeneze mamlaka ya juu zaidi, tutengeneze mamlaka za kikanda, lakini iende juu ifike mpaka kwa mamlaka za juu ifike hata katika Ofisi ya Waziri Mkuu ambaye ndio msimamizi wa shughuli za Serikali. Pia, tunaweza tukaangalia ikafika hadi kwa Katibu Kiongozi, ili watu wachukuliwe hatua za nidhamu kabla ubadhirifu haujafika mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoteza fedha nyingi sana kwa kusubiri kwamba, wezi waibe, wahamishwe vituo, ukaguzi ufanyike, fedha zimepotea, tunakuja kujadili hapa kila mwaka, kila mwaka ripoti hizi zinakuja zinajirudia. Kwa hiyo, tutafute suluhu ya kudumu na tuiwezeshe Ofisi hii ya Mkaguzi wa Ndani iweze kuwa imara, ili iweze kutusaidia kuepuka au kukinga ubadhirifu unaofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Ukurasa wa 29 wa Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali (PAC) utaona kwamba, imeainishwa. Katika hoja za ukaguzi, kuna hoja za ukaguzi ambazo zinatokana na dosari katika usimamizi wa mkataba na athari zake katika matumizi ya fedha za umma. Mfano, utaona kwamba, Serikali imepata hasara ya bilioni 36.8 ambayo imetokana na tozo ya riba kwa TANROADS kwa kuchelewa kulipa wakandarasi na washauri wa miradi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bilioni 36.8 ni fedha nyingi sana na fedha hizi ndio zinasababisha miradi itumie gharama kubwa zaidi kuliko ile iliyokuwa imepangwa. Mradi unakuwa umepangiwa kutekelezwa kwa milioni 100, lakini mwisho wa siku unashangaa mradi umetekelezwa kwa milioni 150. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaomba sana, hizi fedha zinazopotea zingeweza kutumika katika maeneo mengine yenye uhitaji wa rasilimali fedha. tunaomba Serikali itafute suluhu ya kudumu ya kulipa fedha kwa wakati, wakandarasi walipwe fedha zao kwa wakati, washauri wa miradi walipwe fedha zao kwa wakati, ili tusije tukalipa riba ambayo ni hasara kubwa kwa Serikali na hizi fedha zinaweza kutumika katika maeneo mengine kwa maslahi mapana ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, naomba kuunga mkono hoja za Kamati zote tatu. (Makofi)