Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa nafasi hii na uhai kuwepo katika Bunge hili, maana tunaishi kwa neema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Sospeter Muhongo wewe ni jembe tu hata wakipiga kelele, tunakuamini wewe pamoja na Naibu Waziri wako na watendaji wengine wote wa Wizara, kazi mnayoifanya inaonekana, hapa tulipofikia pamoja na figisufigisu zilizofanywa, lakini tumefika hapa tulipo kwa sababu ya kazi yako kubwa uliyoifanya. Watanzania wanajua, ndiyo maana wanakuunga mkono na ninaamini watu wenye akili hakuna atakayesimama kukupinga wewe. Kwa hiyo, ninampongeza sana, songa mbele, jeshi kubwa liko mbele yako na nyuma yako, tunakulinda kwa nguvu zetu zote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia kuhusu Wizara hii, kwa kweli nina kila sababu za kuwapongeza Wizara hii imeonesha dhamira kubwa ya kutaka kutusogeza mbele. Ukisoma hii bajeti fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo ni fedha kubwa, hii ni dhamira nzuri ya Serikali kutaka kuinua uchumi wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini umeme ndiyo kila kitu, hata Waziri wa Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Mwijage anaposema anataka Tanzania ya viwanda kila kona, tusipokuwa na umeme wa uhakika hatuwezi kuwa na viwanda. Kwa hiyo, hizi Wizara zinategemeana, niendelee kusema juhudi zenu ni nzuri na tunakuunga mkono, ukiangalia kwa mfano upande wa REA imeongezeka karibu asilimia 150 utoka shilingi bilioni 350 mpaka shilingi bilioni 535, kwa kweli hii ni dhamira ya dhati kwa Wizara hii. Mimi ninawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho ninaomba kwa Mheshimiwa Waziri na Serikali hizi fedha zinapotengwa zitolewe, siyo leo tunapitisha bajeti mwisho wa siku zinatolewa asilimia tano.
Ninaiomba Serikali ijitahidi hizi pesa zitolewe Watanzania wanahitaji kupata umeme wa uhakika, umeme wa kutosha. Kwa mfano, kule kwetu Kyerwa tangu uhuru ndiyo tumeanza kuona umeme wengine walikuwa wanashangaa umeme ulipowashwa. Bado haujafika mbali, umeme kule kwetu Kyerwa umepita maeneo machache, Mheshimiwa Waziri umefika Kyerwa umeona Watanzania wa Kyerwa namna walivyo na uhitaji wa umeme. Maeneo mengi ya vijijini ndiyo kuna uzalishaji, tunaposema tunataka kujenga viwanda tukipata umeme wa uhakika, hivi viwanda vinaweza vikajengwa vijijini tukazalisha huko vijijini, tukafungua viwanda vidogovidogo na tukaongeza ajira kwa vijana wetu ambao wako mitaani hawana ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninakuomba Mheshimiwa Waziri, jambo hili ninakusifu sana kwa kutotenga vijiji hapa maana kuna kuchomekeana sana hapa, kuna wengine wanapita mlango wa nyuma, kwa sababu hukutaja vijiji ninakuomba wote tukagawane mkate huu sawa, Watanzania ni wamoja na wote tupewe sawa siyo wa kupendelewa, kuna upendeleo na hili naomba mlisimamie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wengine wakati mwingine wanatoa pesa ili wapewe miradi hilo lipo, ndiyo maana unakuta mwingine amepitishiwa vijiji vyote kwingine hakuna, naomba Mheshimiwa Waziri hata hao watendaji wako hao uwaangalie vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri suala la umeme ni muhimu sana na ili Tanzania iweze kuendelea tuweze kufanikisha malengo tuliyonayo tunahitaji umeme wa uhakika, siyo umeme huu tunasema tunafunga umeme lakini umeme huo siyo wa uhakika. Kwa mfano, kwetu Kyerwa, umeme unawaka lakini huwezi ukawasha mtambo wowote mkubwa, umeme unawaka na kuzimika, kule tunapewa umeme masaa mawili, matatu. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri huu umeme usiangalie mijini tu hata huko vijijini ni muhimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la gesi, Mheshimiwa Waziri suala la gesi ni muhimu sana kwa Taifa letu na tumshukuru Mungu kwa jinsi ambavyo tumepata gesi ya uhakika. Hii gesi isijikite kwenye umeme tu wataalam wanasema gesi tunaweza tukaitumia kwenye umeme asilimia kumi, kuna vitu vingi ambavyo tunaweza tukavipata kupitia umeme kwa mfano plastiki, kuna nguo ambazo zinazalishwa kupitia gesi naongelea gesi kuna mbolea na vitu vingine hii gesi isije ikapotea bure. Kama tunaweza kuzalisha umeme asilimia kumi, je, hii asilimia 90 tumejiandaa vipi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na hili lazima uliangalie tusije tukasema tuna gesi kumbe gesi yenyewe tunaitumia asilimia kumi tu, kwa hiyo ninaomba mliangalie.
Mhehsimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Waziri nataka nilisemee Kyerwa tuna madini ya tin, haya madini kule kwetu Kyerwa majirani zetu ndiyo wanaoyafaidi, asilimia kubwa hatuyafaidi Watanzania yanavushwa na hilo Mheshimiwa Waziri unalijua, naomba tulisimamie vizuri ili tukafaidi haya madini ni ya Watanzania siyo ya nchi jirani. Serikali hili mnalijua sijui mmejiandaa vipi kwa ajili ya kulisimamia vizuri ili haya madini yasiendelee kupotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuhusu madini Mheshimiwa Waziri ulifika kule Kyerwa, vijana wetu ambao wanachimba madini wako kwenye mazingira ambayo siyo mazuri tuwaboreshee mazingira yawe rafiki, tutenge maeneo ambayo ni kwa ajili ya vijana wetu hao wachimbaji wadogo wadogo.
Wakati mwingine hawa vijana wanafanya utafiti, wakishagundua madini hawa wakubwa wanakuja wananunua yale maeneo wale vijana ambao wameanzisha wanaondolewa.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri kama ulivyoongea na wale vijana ukasema utatuma wataalam, waje wapime watenge maeneo kwa ajili ya hawa vijana nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, ninakumini wewe ni mchapakazi ninaomba hili ulisimamie kwa ajili ya vijana wetu...
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Naunga mkono hoja.