Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Ninaomba nianze na kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa jinsi anavyosimamia utekelezaji wa bajeti ya Serikali. Pia, ninachukua nafasi hii kumpongeza sana na kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Chande, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa jinsi wanavyotupa ushirikiano Kamati ya Bajeti katika kutekeleza majukumu yetu. Pia, ninachukua nafasi hii kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, Mheshimiwa Daniel Sillo, kwa jinsi alivyo-present vizuri Taarifa yetu na pia, anavyotusimamia vizuri katika Kamati yetu ya Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono maazimio yote yaliyotolewa na Kamati zote mbili Kamati ya Bajeti na Kamati ya PIC; lakini katika mchango wangu nitajielekeza sehemu kubwa kwenye Kamati ya Bajeti, nitaanza na ukuaji wa Uchumi. Katika mipango yetu na bajeti ya mwaka huu tulitegea kwamba uchumi utakua kwa asilimia 5.3. lakini katika kipindi hiki cha miezi sita baada ya kufanya tathmini uchumi wetu umekuwa kwa asilimia 5.2. Kwa hiyo, tuna uhakika kwamba tutafikia malengo ya ukuaji wa uchumi kama tulivyopanga kwenye bajeti yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mchango wa ukuaji wa uchumi umetokana na uwekezaji katika sekta ya umma (public sector investment). Katika maeneo mengi; ukichukulia mfano wa nchi ya Rwanda, wenzetu sekta ya watu binafsi inachangaia asilimia 31 ya ukuaji wa uchumi. Kwa hiyo, ninaomba Serikali ifanye makusudi mazima ya kuhakikisha kwamba inashirikisha Sekta Binafsi katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejenga SGR na miradi mingine mikubwa katika uendeshaji wa SGR, tuna uwezo wa kutumia kama fursa kwa Sekta Binafsi. Badala ya Serikali kujikita kuendesha SGR inaweza ikatoa nafasi kwa Sekta Binafsi ikajikita kwenye upande wa mabehewa na shughuli nyingine ambazo zitaweza kufanywa na Sekta Binafsi ili tuishirikishe Sekta Binafsi katika shughuli za kiuchumi, shughuli za maendeleo; na tuone kabisa kwamba uchumi wetu unakwenda kwa kushirikiana na Sekta Binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaanda bajeti ya mwaka 2023/2024 tuliweka mikakati na tukabadilisha Sheria ya PPP. Lengo kubwa lilikuwa ni kushirikisha Sekta Binafsi na kuweka mazingira mazuri ili Sekta Binafsi iweze kufanya biashara ili kuhakikisha kwamba inasaidia katika maendeleo ya Taifa letu. Tutakapomaliza mjadala huu, kwa sababu Mheshimiwa Waziri wa Fedha yupo, labda atatupa mwelekeo kwamba PPP imefanya kitu gani kwa kipindi cha miezi saba hadi sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ninataka niongelee suala la mfumuko wa bei. Ninaipongeza Serikali katika taarifa yake mfumuko wa bei tupo kwenye asilimia 3.2. Ina maana kwamba umeshuka ukilinganisha na mwaka jana asilimia 4.8. Sababu zilizotolewa na Serikali kwa kushuka katika mfumuko wa bei ni kwamba kuna kushuka kwa bei ya nafaka kama ngano, mahindi, mchele na mazao mengine, lakini mimi binafsi nilikuwa ninajiuliza kwamba kushuka kwa bie ya nafaka hizo kumetokana na kuongezeka kwa uazalishaji au kumetokana na sera zetu za biashara, kwamba hao wananchi wanakosa masoko ya kuuza mazao yao katika nchi za Jirani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano wakati tunaanza msimu uliopita wakulima wa mazao ya mahindi walikuwa wanahangaika sana kutafuta masoko ya mahindi. Serikali ilizuia lakini baadaye ikasema imeachia mipaka iko wazi. Katika biashara ile wananchi wale hawajaweza kuuza mahindi yao moja kwa moja nje. Leo ukienda Mkoa wa Ruvuma na Mikoa ya Kusini mahindi yameshuka bei hadi shilingi 450 kwa kilo, lakini ukingalia portfolio ya mikopo kwenye benki asilimia 45 ya portfolio hiyo ni mikopo ya wakulima, imeenda kwenye kilimo. Kwa hiyo, unaona kabisa kwamba Serikali isipoweka Sera madhubuti ya kuhakikisha kwamba hawa Wakulima wanapata masoko mazuri na wanauza mazao yao katika masoko yanayoeleweka. Hili suala la kilimo tutafika mahali tutagonga ukuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaiomba Serikali kuweka malengo mazuri ya kuhakikisha kwamba inafungua mipaka inawaacha wakulima wauze mazao sehemu yoyote badala ya kuweka vikwazo. Pamekuwa na vikwazo vingi sana, wakulima wakitaka kuuza mazao wanaambiwa watafute vibali, mara wasage unga na wengine hawajajianda. Hivyo vyote ni vikwazo ambavyo vitawafanya wakulima wasiwe motivated katika kuendelea na uzalishaji wa mazao mbalimbali ya chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilikuwa ninataka kuchangia, kwanza ninataka kuipongeza Mamlaka ya Mapato, kwa makusanyo mazuri. Ukiangalia takwimu zetu Mamlaka ya Mapato tayari kwa miezi sita walikuwa wamekusanya mapato ukilinganisha na bajeti kwa asilimia 49.7. Ninaomba niwapongeze, tunakwenda vizuri, tuendelee kuimarisha mifumo katika ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mapato yasiyo ya kikodi ambayo tunapata kutoka kwenye mashirika yetu mbalimbali mashirika ya umma na taasisi, makusanyo yalikuwa ni asilimia 31.19. Unaona kabisa mchango wa wajumbe wengi wamesema kwamba mashirika yetu bado hayafanyi vizuri kuhakikisha kwamba yanachangia Pato la Taifa. Changamoto kubwa iliyopo ni kwamba mifumo iliyopo ya ukusanyaji wa mapato katika hayo mashirika ya umma, bado ni changamoto. Kwa hiyo, ninaomba Serikali ijaribu kuangalia uwezekano wa kuweka mifumo mizuri na kuhakikisha kwamba mapato yetu yatakusanywa kama inavyotakiwa ili kusaidia kuinua Pato la Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye upande wa matumizi tumeenda vizuri; tunajua kwamba tumefikia asilimia 50.2. Hii inatuonesha wazi kwamba utekelezaji wa bajeti ya Serikali unakwenda vizuri. Tumepata changamoto kwenye miradi ya maji. Vilevile, tumepata changamoto iliyopitia mabadiliko ya tabianchi, tuna changamoto kubwa sana ya kuharibika miundombinu katika maeneo mbalimbali. Kule kwangu kwenye barabara zinazokwenda vijiji sehemu kubwa zimeharibika. Kwa hiyo kuna umuhimu wa Serikali kutenga fedha za dharura kwa ajili ya kutengeneza miundombinu, hasa kipindi ambacho barabara hizo zinaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina zaidi ya hapo, ninaomba niunge mkono hoja Taarifa zote za Kamati. Ahsante sana. (Makofi)