Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE.JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati, nampongeza sana Mwenyekiti wa Kamati yetu ya NUU kwa uwasilishaji mzuri sana. Vilevile, nawapongeza Wajumbe wa Kamati yetu kwa kazi kubwa tuliyoifanya mpaka kuleta taarifa hii leo Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa kwenye maeneo kama mawili kama muda utaruhusu. Eneo la kwanza ni lile linalohusu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu ni moja kati ya mataifa yenye heshima kubwa sana duniani. Taswira yake ni nzuri kimataifa na inajulikana tokea harakati za uhuru mpaka kushiriki kwenye masuala mbalimbali ya kimataifa. Mfano mzuri ni namna Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyoshiriki kwenye mambo muhimu na ya msingi sana ya kimataifa, jambo linaloongeza taswira nzuri ya Taifa letu nje na kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na changamoto moja, majengo yetu na balozi zetu huko nje hazina taswira nzuri yenye kuakisi heshima tuliyonayo kimataifa. Naipongeza Serikali kwa mpango wake wa miaka 15 wa kutekeleza miradi 16, kuboresha mazingira na balozi zetu huko nje, lakini mpango huu umekuwa unakumbwa na tatizo kubwa la kibajeti. Mpaka leo tunavyozungumza, katika mpango huu wa miaka 15, miaka mitano sasa umekuwa unasuasua na utekelezaji wake umekuwa ni wa shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya changamoto zinazosababisha mpango huu kutokutekelezeka kwa muda uliopangwa kama nilivyosema, ni bajeti. Pamoja na tatizo la kibajeti na Wizara kuanza sasa kufikiri kuingia kwenye makubaliano na sekta za umma na sekta binafsi ili kuweza kushirikiana na kufanya maboresho kwenye majengo yetu na balozi zetu kule nje. Vilevile, shida kubwa imekuwa ni muda unaochukuliwa kwa ajili ya kufanya majadiliano na taasisi hizi ili ziweze kufanya kazi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba majadiliano haya yasichukue muda mrefu, kwa sababu tokea mwaka 2017, leo ni mwaka 2024 bado miradi hii haijaanza kutekelezwa. Tutaweza kujikuta tunafikia miaka 15 hatujafanya jambo lolote na bado taswira yetu kule kimataifa inakuwa ni hasi. Heshima yetu inapungua kwa sababu majengo yetu yanatia aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana 2023 Kamati yetu ilipata fursa ya kutembelea ubalozi wa Ethiopia, Addis Ababa pale. Tuna viwanja viwili ambavyo vimezungukwa na majengo ya balozi nyingine ambazo zimejengwa vizuri, lakini eneo letu limebaki pori, limezungushiwa tu, wahuni wanakaa pale, jambo linalotia aibu na kuharibu taswira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri sana, Kamati yetu ilipata fursa ya kufa…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Joseph kuna taarifa kutoka kwa Mheshiwa Sophia Hebron Mwakagenda.

TAARIFA

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa mchangiaji kwamba pia katika Ubalozi wa Msumbiji tulikuwa na viwanja viwili Samora Machel alitupatia. Kiwanja kimoja angalau kimejengwa, lakini hicho kingine mpaka leo kipo, imefikia hatua kimeweka uharibifu utafikiri ni kiwanja ambacho hakijatoka katika Taifa la Tanzania. Kwa hiyo, ni viwanja vingi sana ambavyo kama Taifa hatujaviendeleza. Namuunga mkono kwa hilo analosema.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mkundi, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea. Bahati nzuri sana Kamati ilipata fursa ya kukaa na Mheshimiwa Rais wa Ethiopia na katika mambo ambayo Kamati ilijadiliana naye, ni namna ambavyo anaweza kutusaidia katika uendelezaji wa viwanja vile. Rais wa Ethiopia alisihi sana kwamba viwanja vile viendelezwe na vilitakiwa kuchukuliwa, lakini kwa heshima ya Taifa lile na mahusiano yake na Tanzania, akaomba visichukuliwe lakini akatupa nafasi tuviendeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ethiopia walitupatia Watanzania miezi tisa kuanzia mwezi Februari ili tuweze kuendeleza viwanja vile. Nasikitika kusema kwamba mpaka leo viwanja vile havijaweza kuendelezwa jambo ambalo linahatarisha kuchukuliwa kwa viwanja vile na kuendelea kututia aibu. Kwa hiyo, naomba Wizara na hasa Serikali ione umuhimu wa kufanya marekebisho kwenye viwanja vyetu na maeneo yetu ya balozi ili taswira yetu kama Taifa iendelee kuwa chanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kuchangia ni eneo la Wizara ya Mambo ya Ndani. Miaka kadhaa huko nyuma jamii ilikuwa na taswira hasi juu ya Magereza yetu. Watu wengi waliamini ukienda gerezani unaenda kuteswa, taswira ambayo ni hasi. Hali halisi ya Magereza yetu leo siyo kwenda kuteseka, bali kufanya urekebu wa tabia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi yetu tumepata fursa ya kutembelea Magereza yetu. Magereza leo yana hali nzuri, usafi ni wa kiwango cha juu tofauti na huko nyuma ambako ulikuwa ukienda Magereza, maeneo mengi yanatoa harufu na taswira nyingine ambayo siyo nzuri kwa hali ya kiafya ya binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Magereza yetu yako vizuri. Kama walivyosema wachangiaji wa awali, uwezo wa Magereza yetu ni kuchukua mahabusu na wafungwa 29,000 lakini ninafarijika kukutaarifu kuwa leo Magereza yetu yana wafungwa takribani 27,000. Tafsiri yake ni kwamba Magereza yetu yana upungufu wa wateja karibu 2,000 jambo ambalo ni maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hatua mbalimbali alizozichukua ili kuhakikisha kwamba hali hii inaweza kufikiwa. Changamoto tuliyonayo ni kwamba haya mafunzo ya urekebu kuna changamoto ya ukosefu wa fedha ili kusaidia Magereza haya kupata vifaa vinavyowawezesha…

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa kuna taarifa kutoka kwa Ali Juma Mohamed.

TAARIFA

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nimpe taarifa ndugu yangu, licha ya kuwa idadi ya wafungwa pamoja na maabusu imepungua, lakini sasa hivi katika Magereza yetu wafungwa pamoja na mahabusu wamekuwa wanalalia magodoro mazuri kabisa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Joseph, taarifa hiyo unaipokea? Malizia mchango wako.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ni ukosefu wa fedha ili vifaa vya kisasa viweze kupatikana kuwasaidia wafungwa hawa wanapotoka wawe na mwanzo mzuri wa kutumia ufundi na ujuzi wanaopata kutoka Magerezani kuanza maisha mapya uraiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mafunzo ya urekebu kwa mtaala ulipo na namna yanavyotolewa, yanatakiwa kufanyiwa tathmini sasa ili yaweze kuakisi hali halisi ya kisasa tofauti na mfumo uliopo sasa ambao unatolewa katika mazingira ya kizamani. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali ifanye tathmni ya mfumo wa mafunzo ya urekebu yanayofanyika sasa iweze kuendana na mazingira ya kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)