Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia kwenye taarifa hasa ya Kamati ya Maji na Mazingira. Kabla sijaanza kuchangia kwanza niwapongeze Wenyeviti wote wa Kamati hizo mbili, Mheshimiwa Vita Kawawa na comrade kaka yangu Mheshimiwa Kiswaga kwa kazi kubwa wanayoifanya na kwa jinsi wanavyotuongoza. Ninawashukuru sana na kuwapongeza Mawaziri wa Wizara mbili ambazo kwao wanatupa ushirikiano, kwanza Wizara ya Maji Comrade Mheshimiwa Jumaa Aweso, tunakushukuru sana kwa kazi kubwa na nikupongeze tena Mheshimiwa Selemani Jafo kwa kazi kubwa unayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa katika sehemu mbili kama muda utatosheleza nitaanza na biashara ya carbon (carbon trade). Biashara hii ni biashara mpya wengi hawajaielewa ningependa nianze kuielezea kwamba hii biashara ya hewa ya ukaa ni biashara ya namna gani na ningeomba nitoe tafsiri angalau kwa lugha ya kigeni. Carbon trade is a commerce meant to lower carbon emissions and capture atmospheric carbon dioxide by protecting forest as a leading captor. Sasa ni biashara ya kupunguza emission za hewa ya ukaa kwenda angani lakini na kushusha kiwango cha carbon dioxide ambayo iko angani, hewa ambayo iko kwenye atmosphere ili kwenda kwenye viwango vya chini na ni kitu gani kinachoshusha hasa cha kisayansi ni misitu kwa sababu yenyewe ina vidakio tunavyoviita captors hii ndiyo carbon trade. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni fursa mpya katika ulimwengu wa sasa, biashara hii inafanyika na inalipa katika nchi za ulimwengu wa tatu ambazo zinatoa hewa chache zinazotoka kwenye viwanda ni chache ukilinganisha na nchi zilizoendelea kwa maana kwamba carbon emission to the atmosphere is very much lower compared to the developed industrialized countries. Kwa hiyo hiki ndicho kiini hasa hasa cha biashara hiyo kwamba zile nchi ambazo hazichafui hali ya hewa zikiwa na captors kama msitu basi zinaweza zikafaidika na biashara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara hiyo inafanywa na watu gani? Biashara hiyo inaweza ikafanywa na mtu binafsi, inaweza ikafanywa na makampuni yaliyosajiriwa na inaweza ikafanywa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni eneo jipya, biashara hii kwa hapa kwetu nchini imeanza mwaka 2018 na Waziri juzi alituambia mpaka 2022 kwa miaka takribani mitatu minne, Tanzania ilikuwa imepata bilioni 32 lakini kwa mipango ambayo sasa Wizara ya Mazingira inayoongozwa na Comrade Selemani Jafo anasema wamejipanga kila mwaka watakuwa na uwezo wa kupata trilioni 2.4 za Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii biashara inaenda kuitajirisha nchi yetu endapo mambo yafuatayo tukiyafanya, inaonekana ni nyepesi kuzipata hizo lakini ni kazi ngumu.

Moja, nchi yetu ina misitu ya kupandwa na ile ya asili jumla ya misitu tuliyonayo ni 589. Misitu yote hii inafaa kwa biashara ya carbon, kwa maana kwamba yote hii ni leading captors wa atmospheric carbon dioxide ina uwezo wa capture. Kwa hiyo, hii ndiyo bidhaa ambayo tunayo ambayo inaweza ikatuingizia fedha hizi za Kitanzania trilioni 2.4 tunazipataje? Sasa hivi sisi hatujafaidika, nimpongeze Mheshimiwa Jafo Waziri wa Mazingira kwa juhudi ambayo amekwishaifanya, tayari wamekwisha tengeneza mwongozo lakini huo muongozo sijajua ni kwa upande gani lakini bado haijafika mpaka kwenye ngazi ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri yafuatayo yafanyike ili Tanzania iweze kufaidika na biashara hiyo. Kwanza ni capacity building, ni lazima Serikali ijipange kujenga uwezo kwa watumishi wote wanaohusika na Wizara za Maliasili na Utalii na zile za Mazingira na wadau wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili, ni lazima utengenezwe uelewa wa pamoja kwa wananchi, creation of awareness to the community ili wananchi waelewe hii biashara inaendeshwa namna gani? Wote tukishajenga uelewa wa pamoja basi wananchi naamini watashiriki kimalifu katika kutunza mazingira, hususani ni misitu na tutafaidika na biashara hizi za carbon. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu kuna uvunaji unaoendelea wa miti asili ambao unafanywa na TFS, huwa wanauza vipande vya misitu kwa ajili ya wananchi wale ambao wamesajili biashara ya mkaa na kuni ili kufanya biashara. Ni kweli sasa hivi hatuna njia mbadala ya nishati ambayo inaweza ikatumika kwa watu ambao ni maskini, ningeomba fedha hizi ambazo zitatokana na biashara hii ya ukaa ziende kwenye tafiti ikiwa ni pamoja na tafiti za kutafuta nishati mbadala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nihame hapo lakini niende tena hapohapo kwenye Wizara ya Mazingira. Tunayo Sheria ya Mazingira ni ya muda mrefu sana, Sheria ya Mazingira Namba 191 inatakiwa ihuishwe, na ni vema sasa Serikali vilevile iharakishe mchakato wa kulifanya Balaza la Mazingira kuwa Mamlaka Kamili ambayo sasa Balaza la Mazingira ambayo ni NEMC ibadilike iwe authority, iwe ni National Environmental Management Authority ili kuipa nguvu na iweze kufanya kazi kikamilifu, itakuwa na meno lakini itakuwa na soko kwenye taasisi za kidunia zinazotoa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho niende kwenye Wizara ya Maji harakaharaka…

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umekwisha malizia sekunde kumi.

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Maji kwa juhudi kubwa ambayo ameifanya inaonekana ni chanya kabisa na atakuwa ni mkombozi hata kwa Mkoa wa Tabora. Ipo juhudi kubwa anapeleka miradi kwenda kutatua changamoto ya maji na siyo kwa Tabora tu hata kwenye Mikoa mingine, tunampongeza na hongera sana kazi yake inaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)