Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Dr. Stergomena Lawrence Tax

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kukushukuru kwa kunipa fursa na mimi ya kuchangia katika taarifa ya Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Napenda kuanza kwa kumshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati, Mheshimiwa Vita Rashid kawawa, Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Wajumbe wote wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Pia nawashukuru Waheshimiwa Wabunge, kwa michango yote ambayo mmetupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Kamati kwa Miongozo Madhubuti ambayo wameendelea kutupatia, ushauri lakini pia na ushirikiano mkubwa ambao umetuwezesha kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi mkubwa ambao unatokana na michango ambayo wametupatia na miongozo ambayo wameendelea kutupatia. Nawaahidi tu Waheshimiwa Wabunge na Kamati kwa ujumla kwamba michango yote na ushauri wote ambao umetolewa, tutaendelea kuuzingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa na mimi kutoa ufafanuzi katika baadhi ya hoja ambazo zimejitokeza katika taarifa zilizowasilishwa lakini pia katika michango ya Waheshimiwa Wabunge mbalimbali. Nianze na hoja ambayo imejitokeza, imeongelewa na Kamati lakini pia imechangiwa na Waheshimiwa Wabunge ambayo inahusiana na ufinyu wa bajeti. Katika Kamati imeonyeshwa kwamba, katika mwaka wa fedha tulitengewa kiasi cha shilingi bilioni 222, milioni 833 na laki 1 na 71 kwa ajili ya bajeti ya maendeleo ya mwaka huu wa fedha. Katika kiasi hicho kwa ujumla wake tumepata asilimia 35.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kueleza kuwa, kiasi hiki ni cha mwaka mzima lakini katika kiasi hiki cha mwaka mzima, kwa nusu mwaka ambao umeripotiwa, tumekwishapata kiasi cha asilimia 65. Ni matumaini yetu kwamba kwa kiasi kichobakia, tutaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha na kiasi hicho kitapatikana kama ilivyosisitizwa na Waheshimiwa Wabunge, na pia kama ilivyosisitizwa sana na Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kueleza kwamba, katika Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Amiri Jeshi wetu Mkuu, Vyombo vya Ulinzi na Usalama ikiwa ni pamoja na Wizara, vimepewa uzito mkubwa sana. Kama mtakavyoona, mkifuatilia bajeti ambayo tumeendelea kupata imekuwa ikiongezeka tangu Mwaka 2021/2022. Katika mwaka 2021, bajeti tuliyokuwa tumetengewa kwa ujumla wake ilikuwa shilingi trilioni 2.4; lakini mwaka 2022/2023 bajeti hii iliongezeka na kufikia shilingi trilioni 2.7 ikiwa ni sawa la ongezeko la asilimia 13. Kwa Mwaka huu, bajeti tuliyotengewa ni kiasi cha shilingi trilioni 3 ikiwa ni sawa na asilimia tisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba hoja ya Kamati ilijikita zaidi katika Bajeti ya Maendeleo, lakini kwa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, huwezi kutenganisha Bajeti ya Maendeleo na Bajeti ya Matumizi Mengineyo kwa sababu vifaa vikinunuliwa lazima vitunzwe, vifaa vikinunuliwa, wanaoviendesha lazima wafanye mazoezi, vifaa vipashwe moto, ndege zirushwe, Marubani wapate nasaha, na kadhalika na kadhalika. Kwa hiyo hizi bajeti zote mbili ni muhimu sana kwa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Kwa muktadha huu, naomba kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais wetu na Amiri Jeshi wetu Mkuu kwa umuhimu mkubwa ambao ameutoa kwa Wizara yetu na kwa taasisi zake. Kazi inaendelea kufanywa kama ambavyo mmeona na mambo mengi yanaonekana, nchi yetu, mipaka yetu ipo salama, amani imetamalaki ndani ya Taifa letu kwa hiyo namshukuru sana Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuwapongeza Makamanda wote, Maaskari wote na Maafisa wote kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Ulinzi ni jukumu letu sote kwa hiyo naomba pia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa kushiriki katika kuhakikisha kwamba Taifa letu liko na amani na ulinzi uko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imeongelewa, ni suala la JKT kwamba vijana wengi wanatakiwa waende JKT lakini mpaka sasa hivi hatujaweza kuwapeleka vijana wote wanaomaliza Kidato cha Sita. Ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba vijana wote wanakwenda JKT kwa sababu Serikali inautambua umuhimu wa kuwapeleka vijana JKT ili waweze kuwa mahodari lakini pia kwa maslahi mapana ya Taifa letu. Kwa maana hiyo ndiyo maana Mwaka 2013 Serikali ilirejesha Mafunzo ya JKT ambayo yalikuwa yamesitishwa Mwaka 1994 ili kuwawezesha vijana wanaomaliza Kidato cha Sita waweze kwenda JKT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda hatua kwa hatua, na imetolewa katika taarifa kwamba kwa mwaka jana tuliweza kuchukua asilimia 50 ya vijana waliokuwa wamemaliza form six. Matarajio yetu ilikuwa ni kuwachukua vijana wote wanaomaliza kidato cha sita kufikia mwaka 2025/26.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyoelezwa, kutokana na changamoto za Miundombinu na kibajeti, inawezekana lengo hili tusilifikie lakini tumeupokea ushauri wa Kamati, tutaufanyia kazi ili kuona kwamba tunaweza kuwachukua vijana wote kama inavyotakiwa. Niunganishe hoja hii na hoja iliyokuwa imetolewa na Mheshimiwa Mbunge Ngassa, kwamba ili sharti lililowekwa la kwamba vijana wanaokwenda kuajiriwa katika Vyombo vya Ulinzi na Usalama, lazima wawe na Mafunzo ya JKT nililitolea majibu nafikiri wiki iliyopita wakati nikijibu moja ya maswali na ni kwamba ni kweli tumekwishaona kwamba kuna changamoto hiyo. Katika Taarifa ya Tume ya Jinai ni Hoja ambayo imetolewa Mapendekezo na Serikali inalifanyia kazi. Tutaendea kulifanyia kazi kadri itakavyowezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Hoja nyingine ambayo imetolewa kuhusiana na Jeshi la Ulinzi la Wananchi kuwekeza katika Teknolojia. Hiki ni kitu muhimu sana na napenda tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako Tukufu kwamba hatuko nyuma katika suala hili. Dhima ya Jeshi letu ni kuwa na Jeshi la kisasa. Si suala jipya, ni suala ambalo tunaendelea nalo na tumeendelea kuwekeza na kujipanga vizuri kiteknolojia. Najua Teknolojia inakua kwa haraka na sisi tunajitahidi hivyohivyo kwenda kwa haraka. Unaposema kuwekeza katika Teknolojia, si katika dhana na vifaa tu lakini pia ni katika utaalamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote tunayafanya na kama waliosikiliza wakati Mheshimiwa Rais, Amiri Jeshi Mkuu akifungua Kikao cha Makamanda kilichofanyika Mwezi jana, Mwezi Januari, hili pia alilisitiza. Hii inaonyesha wazi kwamba, hata Amiri Jeshi Mkuu, anatambua hili na ameendelea kusisitiza kwamba lazima twende na Teknolojia. Hiyo ilikuwa ni hoja ambayo ilitolewa na Mheshimiwa Lugangila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja ambayo ilitolewa na Mheshimiwa Fakharia kuhusiana na vifaa, kutenganishwa vifaa vya Jeshi. Tumeipokea hoja hii, tunaifanyia kazi na tutaendelea kuifanyia kazi. Hoja ya Mheshimiwa Grace Tendega kuhusu bajeti kwenda Mzinga, tumeliongelea sana, Kamati imesisitiza sana, tutaendelea kulifanyia kazi. Hoja ya Mheshimiwa Ngassa, nimeshaijibu, hoja za Mheshimiwa Zahor ilikuwa ya kiujumla kwa Serikali nzima, tutaendelea kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kurudia kwamba hoja zote tumezipokea na tutazifanyia kazi. Naomba kutoa hoja. (Makofi)