Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Kwa mara nyingine namshukru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai na kunipa fursa ya kutoa mchango wangu kwenye Taarifa ya Kamati ya Miundombinu. Kwanza namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa anaoufanya kwenye sekta hizi za mawasiliano kwa sababu Taifa bila mawasiliano uchumi hautakuwa imara na mambo mengi na maendeleo ya wananchi yatakuwa duni, kwa hiyo, nampongeza sana kwa uwekezaji mkubwa anaoufanya kwenye sekta hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Kamati pia kwa taarifa nzuri na nami mapema kabisa nisema nakubaliana na taarifa yao na naunga mkono taarifa yao. Nitakuwa na mchango kwenye maeneo kama mawili muda ukiruhusu maeneo matatu. Kwanza, ni eneo la sekta ya mawasiliano. Miezi kadhaa iliyopita tulishuhudia uzinduzi wa mradi mradi wa mawasiliano kupitia sekta hii ya mawasiliano na hasa taasisi hii ya UCSAF.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa imefanyika naipongeza Serikali na naipongeza Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya. Utakuwa ni shahidi mara kwa mara tunapokuwa Bungeni hapa kunakuwa bado na maswali mengi juu ya mawasiliano hasa kwenye eneo la minara, kwa mujibu wa Kamati yetu ya Miundombinu kasi ya utekelezaji wa miradi ya mawasiliano hasa kwenye ujenzi wa minara bado hairidhishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kupitia Wizara tuangalie kama kuna changamoto yoyote, kama kuna shida ya uhaba wa fedha kwenye utekelezaji wa miradi yetu kupitia UCSAF, tuone nini tunaweza kufanya ili kuharakisha utekelezaji wa miradi hii ya mawasiliano ili wananchi wetu waweze kupata mawasiliano kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitolea mfano kwenye eneo langu la Ukerewe bado changamoto ni kubwa sana kwenye maeneo kama ya Bukiko na maeneo mengine kiasi kwamba bado wananchi wanahitaji kwenda kwenye maeneo yenye miinuko ili waweze kupata mawasiliano. Kwa hiyo, naiomba Wizara inayohusika na sekta hii ifanye kazi kubwa ili miradi hii ambayo inatakiwa kutekelezwa itekelezwe kwa haraka na wananchi waweze kupata mawasiliano katika mazingira yaliyo mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo natamani kuchangia ni eneo la usafirishaji. Kupitia taarifa ya Kamati imeonesha kwamba bado kunahitajika pesa ili kuweza kusaidia kampuni ya usafirishaji wa meli MSCL iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi. Ni kweli kwamba Tanzania tuko kwenye eneo ambalo ni la kimkakati, tuna ukaribu na mahusiano na nchi za Jirani, nchi kama DRC, Uganda kuna Visiwa vya Ushelisheli, Visiwa vya Comoro na mataifa mengine ya jirani na yote ni maeneo ya kimkakati kibiashara. Maeneo haya ili yaweze kufikika ni muhimu sana tukaimarisha kampuni yetu ya MSCL ili iweze kuwa na meli za kusafirisha mizigo na abiria kwenda kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna fursa kwenye nchi hizi za jirani ni fursa za kiuchumi kwa wananchi wetu, ni lazima tuwekeze kwenye kampuni hii ya MSCL iweze kufanya ukarabati na iweze kutengeneza meli ili meli hizi ziweze kufikia maeneo haya ya masoko na kufanya wananchi wetu waweze kuwa imara kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kwa safari za nje tu hata kwa ndani bado tuna changamoto. Kwa mfano, kwenye Ziwa Viktoria tuna meli ambazo bado ziko kwenye matengenezo na wananchi wetu wanapata wakati mgumu sana kwenye huduma za kila siku kuweza kusafiri kutoka eneo moja kwenda eneo jingine. Nitumie nafasi hii kwa sababu sisi kwa mfano kwenye eneo langu ninalotoka, Eneo la Ukerewe tunategemea usafiri wa meli. Sasa kunapokuwa na upungufu wa uwekezaji kwenye utengenezaji wa meli inakuwa ni changamoto kubwa ya usafiri kwa watu wanaotoka visiwani kama Ukerewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali ikiwezekana inisaidie kutoa ufafanuzi. Siku za karibuni kumekuwa na utaratibu wa usafiri kwa mfano kutoka Ukerewe kwenda Mwanza. Meli zipo, napongeza kuna uwekezaji wa watu binafsi lakini wanapeana zamu kiasi kwamba badala ya meli kusafiri zote kwa wakati mmoja inasafiri meli moja au meli mbili wanapeana zamu jambo linalopelekea kunakuwa na mrundikano mkubwa sana wa wasafiri kwenye vyombo hivi vya usafirishaji, jambo ambalo ni risk kwa wananchi hawa, inaweza kutokea ajali halafu likawa jambo jingine kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini Serikali inaruhusu jambo hili badala ya kuruhusu vyombo vyote vikafanya kazi, vikasafirisha wasafiri katika mazingira mazuri lakini inapokwa wanaruhusu wanapeana zamu inakuwa ni risk kwa wasafiri wanaosafiri kupitia vyombo hivi. Naiomba Serikali iwekeze itoe pesa iwasaidie MSCL. Bahati nzuri sana MSCL ina uongozi mzuri na imara ambao kama watapewa mtaji wanaweza kufanya mambo makubwa na kufanya shirika hili kuwa na nguvu kuweza kuvutia uwekezaji kwenye nchi zilizo jirani na kuimarisha uchumi wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu na la mwisho ni eneo la TANROADS, wamesema wachangiaji wengi na Kamati imeeleza. Bajeti ya kuwezesha TANROADS kuweza kuimarisha barabara zetu ni karibu shilingi trilioni tano. Mwaka jana tumepitisha bajeti ya shilingi trilioni moja nukta kadhaa lakini siyo jambo la siri barabara zetu hivi sasa, hasa kutokana na mvua nyingi zilizonyesha barabara zetu zina matatizo mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna haja ya TANROADS kujengewa uwezo ili waweze kuimarisha barabara zetu hasa zinazotuunganisha kutoka kwenye maeneo ya Mikoa na maeneo mengine yaliyo imara kiuchumi ili kusaidia kuimarisha uchumi wa watu wetu. Pamoja na kuongeza pesa hizi vilevile wale Wakandarasi wanaopewa miradi hii nashukuru Mheshimiwa Kalogeris amesema hapa kwamba ni dhamira ya Mheshimiwa Rais kuimarisha wakandarasi wetu wa ndani lakini bado nimekuwa nina mashaka sana na baadhi ya wakandarasi wetu. Mara kwa mara nimekuwa nasafiri kwa barabara kwenda Mwanza, kuna barabara ya kutoka Shinyanga Eneo la Hungumalwa kama sikosei kuja mpaka Mwanza, eneo lile linatengenezwa karibu kila mwaka lakini kila linapotengenezwa muda mfupi kunakuwa na matatizo kwenye barabara ile, sasa sijui tatizo ni wakandarasi au mazingira ya eneo lile lakini hoja yangu hapa naiomba Wizara iweze kuwasimamia wakandarasi wetu ili wanapopewa miradi hii thamani ya pesa vilevile iweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru Mheshimiwa Rais lakini na Wizara, Mheshimiwa Bashungwa najua unafanya kazi kubwa sana, barabara yetu ya kutoka Nansio kuja Kisorya ilitengewa pesa mkandarasi amekwishapatikana lakini haijaanzwa kujengwa kwa sababu ya changamoto za Wizara ya Fedha kupitia TRA, naomba sana utusaidie kuamua eneo hili ili barabara hii muhimu sana ianze kutengenewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)