Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii nami nichangie hoja zilizopo Mezani. Kwanza, naunga mkono hoja zote mbili za PAC pamoja na LAAC. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC nitajikita zaidi kwenye masuala yanayaohusiana na LAAC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza, nampongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais, wetu wa Awamu ya Sita, kwa kushusha fedha nyingi katika Halmashauri zetu. Hili jambo limetufanya tuwe na miradi mingi ambayo leo hii tunaona udhaifu ambao umetokana na utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, pili, namshukuru sana CAG kwa kazi kubwa aliyoifanya na kufichua yote haya ambayo tunayasema. Sisi Wajumbe wa Kamati siyo kwa akili yetu, ni wao, wenzetu wamefanya kazi hii bila kuwaogopa Wakurugenzi, bila kuwaogopa Wakuu wa Idara na kuleta taarifa zote hizi ambazo tunazizungumza leo kwamba zina changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitajikita zaidi kwenye Force Account, hasa kuhusu ukiukwaji wa Mwongozo wa Utekelezaji wa Miradi yetu. Force Account imeweka utaratibu, TAMISEMI wanatengeneza BOQ kulingana na mahitaji ya kazi ambayo wanataka kuifanya. Ninaamini TAMISEMI wana wataalamu wote ambao wamefanya kazi ile kwa uadilifu na kujua gharama halisi ya kila mradi ili waende kuushusha chini.

Mheshimiwa Spika, mfano halisi, ndugu zangu kitaalamu angalia hata bei ya sigara inavyokuwa, nchi nzima ni bei moja. Wataalamu walikaa wakakubaliana kulingana na gharama ya kila mahali waka-standardize wakaona gharama ya ununuzi na kuuza sigara ni kiasi hicho. The same applied kwa TAMISEMI, wameshafanya utafiti wa kutosha wa gharama za kila eneo na wakachukua average kwa ajili ya utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachojitokeza sasa ni watekelezaji, usimamizi unakuwa siyo mzuri. TAMISEMI wanatoa taarifa yao vizuri, Mwongozo upo kwa kila Halmashauri. Tulitegemea variation katika Halmashauri isizidi asilimia 10 kwa maana ya kuongeza na kupungua, lakini bahati mbaya variation ya maeneo mengi ni zaidi ya asilimia 15. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuchukue mfano, Mkoa wa Morogoro. Mvomero wana variation ya asilimia 51 katika ujenzi wa Sekondari zile za SEQUIP ambayo ni shilingi milioni 470, lakini wanahitaji zaidi shilingi milioni 241,363 na ushei ili kukamilisha mradi ule ili uweze kukamilika. Morogoro DC wao kidogo wana afadhali wana variation ya asilimia 15 ambayo inasimama shilingi milioni 73 kwenye ile shilingi milioni 470. Ulanga asilimia 34, Malinyi asilimia 26 na Mlimba asilimia 29.68. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini ninasema hivi? Wataalamu wetu kwenye Halmshauri, kila mtu na mtazamo wake. Kwa sababu kama wangekuwa wanasimamia vizuri na kutumia ofisi zetu za mkoa kusingekuwa na variation kutoka wilaya moja mpaka wilaya nyingine kiasi kwamba inafanya Force Account ionekane haina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukingalia katika utekelezaji huo huo, usimamizi utakuta hata majengo yanayojengwa, ukweli ni kwamba kutokana na changamoto waliyozungumza wenzangu na taarifa ya Kamati ya wataalamu wa ujenzi kutokuwepo, basi hata changamoto yenyewe ya majengo yanakuwa ni below standard. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli hili jambo linasikitisha sana. Pamoja na kuona hivyo, lakini kuna maeneo too much, yamezidi. Mfano uliotolewa kwenye taarifa yetu, kwa mfano pale Newala, kwingine pale Namtumbo kwenye mradi ule wa Sekondari ya Wasichana wa shilingi bilioni tatu wanahitaji zaidi ya shilingi 1,450,000,000 variation ni zaidi ya asilimia 49. Kwa kweli nina mashaka na wataalamu wetu katika Halmashauri, kwamba hawataki kumsaidia mama miradi ikamilike wananchi wafaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kinachotokea wao ni kuangalia maslahi yao binafsi, mfano mmoja mdogo sana, utakuta kwenye Force Account wameanzisha mtindo wa kununua manunuzi yote ya vifaa kutokana na mtandao. Ukinunua kwenye mtandao unakuta mfuko mmoja wa simenti shilingi 28,000 au 25,000. Ukienda dukani au kwenye soko uhalisia ni shilingi 18,000 au 19,000.

Mheshimiwa Spika, hili jambo nalo mtandao unachangia kwa asilimia kubwa. Niliona sehemu tulikotembelea, wao wameweka bati mmoja shilingi 62,000, wakati bei ya soko ni shilingi 38,000 mpaka shilingi 42,000. Kwa hiyo, manunuzi ya kwenye mtandao yamefanya Force Account iwe na gharama kubwa kuliko vile ambavyo soko lilivyo. Kwa hiyo, nadhani kuna haja ya wenzetu kupitia sheria hii na mwongozo wa Force Account utumike kama ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la matumizi ya Kamati. Hizi Kamati zimekuwa kama fingerprint ya kusema kwamba tuna Kamati ya Manunuzi, tuna Kamati ya Mapokezi na tuna Kamati ya Usimamizi. Hizi zote hazifanyi kazi, imekuwa kama mapambo. Hawapewi Semina, wanaleta mzigo, wanaleta na delivery note, hakuna cha invoice, hawajakaa vikao vyovyote, vikao vinakaliwa juu na Halmashauri, wanarudisha kule wanapeleka vitu. Kwa kweli hili jambo linafanya kwamba Force Account inaonekana kwamba haina ufanisi mkubwa kwa sababu kuna watu wamejipanga kuihujumu Force Account kwa manufaa yao wenyewe badala ya manufaa ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli jambo hili kama hatutalitilia mkazo kwa kuwachukulia hatua wale wote waliohusika katika ubadhirifu huu wa kuongeza gharama ya ujenzi tofauti na iliyokadiriwa, nadhani tutakuwa hatuwatendei haki wananchi wetu, kwa sababu kuna majengo mengi sana yaliyojengwa kwa Force Account hayajakamilika.

Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)