Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ambayo nami nitatoa mchango wangu. Nami kama ambavyo wamesema wenzangu, nami ni miongoni mwa Wajumbe wa Kamati ya LAAC, Kamati ambayo kwa kweli kwa kiwango kikubwa tunafanya kazi kwa ushirikiano wa kutosha. Pia nampongeza sana CAG kwa sababu taarifa yake inatusaidia kuweza kubainisha machache ambayo tutayachangia kwenye Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni shukrani kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa namna anavyoendelea kutupatia pesa za utekelezaji wa miradi kwenye kila Jimbo. Wiki mbili zilizopita nilikuwa Jimboni na hapa nitoe shukurani za Wanajimbo, maana nilikwenda kukabidhi ambulance ambayo ilitoka katika Ofisi yake na wananchi wa Kibaha Vijijini wanampongeza na wanamshukuru sana kwa kuwapatia gari kwa ajili ya huduma za wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili kwa jioni hii, napenda kutoa pole kwa Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo, Taifa leo ukilisikia kwa miezi michache au siku chache hizi, baadhi ya watu maarufu waliokuwa viongozi kwenye nchi yetu wamepoteza maisha. Nampa pole Mheshimiwa Rais kwa kupotelewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu Mstaafu ambaye naamini viongozi wetu na wengine wengi wapo huko sasa hivi kwa ajili ya maandalizi ya kumzika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile, natoa pole kwa Wanajimbo la Kihaba Vijijini kwa kuondokewa na kipenzi chao, ambaye ndio alikuwa Mbunge wa kwanza wa Jimbo la Kibaha Vijijini, baba yangu Mheshimiwa Dkt. Ibrahim Said Msabaha, ambaye tumemzika jana. Nawapa pole sana Wanajimbo la Kibaha Vijijini, waendelee kuvuta subira kwa sababu yale ambayo walianza kuyapata kutoka kwake, kijana wake na kijana wao nitaendelea kuyapambania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo nitajielekeza kwenye maeneo machache, lakini kwa kweli kabisa kwa namna ambavyo Kamati tumepitia tunajielekeza sana kwenye Force Account. Hata wewe hapa katika kuanza kufuatilia na kutaka kutufanya tukae vizuri, ulitaka kuona kama Azimio lililo mbele yetu ndiyo mawazo ambayo watu wanaendelea kuchangia?

Mheshimiwa Spika, sisi kama Kamati tumepitia na tumeona Force Account kwa upande ilikuwa na faida kubwa sana, lakini zipo changamoto ambazo zimejitokeza kwenye Force Account na kwa sababu hiyo, chini ya Mwenyekiti wetu shupavu kabisa Mheshimiwa Halima Mdee, tukaja na maazimio yale ambayo tunaliomba Bunge liwe sehemu ya maazimio kwamba baadhi ya miradi mikubwa ifanywe nje ya Force Account. Tumetoa mawazo yetu pale kwamba baadhi ya miradi ambayo tunakuwa tumekubalina, basi iendelee kufanywa na Force Account. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama Mjumbe wa Kamati, nitapita katika sura ile ambayo Mwenyekiti wetu alituongoza na Kamati tulikubaliana kwamba lazima kwenye na miradi ambayo itafanywa na Force Account na lazima kuwe na miradi ambayo pia inaweza ikatekelezwa na Wakandarasi. Kwa mfano, kwa nini tumefika kwenye mawazo ya namna hii? Nitapita kwenye maeneo machache ya kuona namna gani Force Account imeleta na imeonesha changamoto, na ndiyo maana Wajumbe wa Kamati tumekubaliana kwamba lazima kuwe na miradi ambayo inafaa kutekelezwa na Wakandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tumejaribu kupitia miradi michache, nitatoa hapa mifano miwili tu. Ukiangalia pale kwenye Halmashauri ya Mtama, walipewa shilingi milioni 470 kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Sekondari, lakini mpaka ambapo wamefikia, wamehitaji na wamekwenda kufanya ile kazi kwa shilingi milioni 655.272; lakini ukienda kuiangalia Nzega, tunajenga jengo lile lile, lenye mchoro ule ule ambao watalaamu wa kutoka TAMISEMI wameupeleka, Nzega wamepewa shilingi milioni 470, lakini mpaka taarifa ya CAG inatoka, wameshatumia shilingi milioni 849.575, na bado zipo kazi hazijakamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nini maana yangu au maana yetu kama Wajumbe wa Kamati? Tunaona kwamba pamoja mawazo mazuri ambayo yalitolewa na Serikali kwenye kuitumia Force Account, lakini watekelezaji na wasimamizi wa Force Account, Halmashauri moja mpaka Halmashauri nyingine kila mmoja ana mtazamo wake na kila mmoja ana namna ya kufikiria anawezaje kukamilisha miradi. Kwa sababu haiwezekani kuwe na utofauti wa karibu shilingi milioni 200 kwenye jengo moja lenye thamani ambayo tayari lilishafanyiwa tathmini na wataalamu wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ilitakiwa kama ni tofauti ionekane ndogo sana. Ukienda katika hali hii, unakuta kwamba lipo tatizo la wasimamizi kila mmoja ana mtazamo wake kwenye hili. Kwa hiyo, tunaomba sana, mawazo yale yaliyotolewa na Kamati yaendelee kupata nguvu ya kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukirudi kwenye utaratibu mzima wa wingi wataalamu, miradi yetu mingi inashindwa kukamilika kwenye ubora. Tunafahamu sote hapa kama Wabunge kwamba Serikali mwaka 2019 walikuja na mwongozo wa kusimamia majengo, ni jengo lipi linatakiwa liishi kwa umri gani? Sasa tutakuja kuona kwamba wataalamu wa kusimamia ubora wa majengo haya kwenye Halmashauri zetu, hawapo.

Mheshimiwa Spika, hapa tena ninatoa mifano michache uone. Kule Sikonge wametekeleza miradi 111, lakini wana Mainjinia wawili tu. Kule Kaliua wametekeleza miradi 141, wana Mainjinia wawili tu. Ukienda Tanganyika wametengeneza miradi 169, wana Mainjinia wanne. Kwa Halmashauri chache ambazo tumezipitia 21, tumegundua zina Mainjinia 79, lakini wametakiwa kusimamia miradi 3,167. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu tujiulize ndugu zangu, Injinia ndio mwenye jukumu la kusimamia mradi. Miradi elfu tatu ikasimamiwe na Mainjinia 79, tunategemea kwenda kupata ubora unaostahili? Ndiyo pale Serikali, kwa sababu nia ni kuwahudumia wananchi, kwa nia njema kabisa, wanaamua Mwalimu simamia Sekondari ijengwe, Mganga simamia Kituo cha Afya kijengwe. Lengo ni kuweza kufikisha huduma kwa wananchi, lakini kiukweli zinafika huduma ambazo sasa zinakwenda kuharibu miradi, kwa sababu kila jengo lina thamani yake na lina muda wake wa kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri ambao nafikiri tunatakiwa tuufanye, kwanza tukubaliane na mapendekezo ya Kamati, na ninawaomba ndugu Wajumbe katika hili tuwe na maazimio ya kweli. Miradi yote mipya ambayo inakwenda kuanzishwa, kwa mfano, unaenda kuanzisha Vituo vya Afya Vikubwa kabisa, ni vizuri miradi hii wakakabidhiwa Wakandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii Force Account ambayo tayari na sisi tuliianzisha kwa mujibu wa sheria zetu, iendelee kubaki kusimamia miradi yenye ukarabati mdogo. Kwa sababu ni kweli, unakwenda kufanya ukarabati wa darasa lililochimbuka sakafu, unakataa kumtangaza Mkandarasi kwa suala la kumnunulia tu simenti kusogea pale, kumsogezea mchanga, halafu kuweka namna ya kulisimamia; tukifanya hivi, tutaenda kuokoa fedha nyingi kama ambavyo Serikali ilifikiria na pia tutajenga haya majengo na tutakosa hizi lawama ambazo leo tunatupiana hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitusikiliza Waheshimiwa Wabunge unaweza ukaona kama kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaonekana wanawaandama Wakurugenzi, lakini siyo kwamba tunawaandama kwa sababu eti hatuwapendi. Ndio wenzetu, ndio tunafanyanao kazi, na hakuna ambaye hajui kwamba hawa ni sehemu ya kazi ya Serikali. Tunachokizungumza, kwenye vikao vyetu vya Kamati, ukihojiana na hawa Wakurugenzi, ukiwasikiliza, kila mmoja anakutolea taarifa ya mradi huo huo unaofanana kwa lugha ambazo hazifanani. Zinasababisha Wajumbe kama watu wenye akili timamu kuona hapa ipo sababu inayomfanya huyu ajibu hivi na hapa ipo sababu inayofanya mtu huyu ajibu hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kwamba ni lazima Serikali iendelee kutekeleza miradi hii, lakini ni lazima tutumie mawazo ya Kamati, pia lazima tutumie ushauri unaotolewa na CAG, kwa sababu CAG anakuwa amepita kwenye yale maeneo na anaona sababu za wazi zinazosababisha matatizo haya. Tukubaliane tuweke maazimio ambayo yatakwenda kutekeleza miradi hii.

Mheshimiwa Spika, mimi kama Mjumbe wa Kamati, naungana kabisa na ninaunga mkono Kamati yangu na ninaomba Bunge lifikirie hivyo kwamba miradi hii siyo yote inayostahili kufanywa na Force Account, kwa sababu hali ya utekelezaji wa miradi kule siyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo jambo lingine ambalo nalo tulitazame, na hili litazamwe kwa upana mkubwa sana na viongozi wa Serikali. Vifaa vyetu tunavyokwenda kutengenezea miradi yetu; simenti, nondo, rangi na vingine vyote, inawezekana lipo tatizo la ubora. Kwa sababu tukiangalia majengo ambayo yamejengwa miaka mingi ya nyuma, ukiangalia ubora wake, ukienda kulitazama na jengo linalojengwa leo jipya na vifaa hivyo, unapata mashaka kwamba yawezekana vifaa vyetu tunavyotengeneza kwenye viwanda vyetu vinaweza vikawa na ubora mdogo. Siyo kwamba nasema hivi kwa kuvituhumu hivyo viwanda vinavyotengeneza, lakini nataka Serikali itoe macho kwa kina ili iende ikatazame vifaa hivi vinavyotengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeenda baadhi ya maeneo, unaweza ukashangaa, ukiitazama tiles zinawekwa pale, kona hazifanani. Yaani maana yake, ukubwa wa tiles unatofautiana. Sasa ukishafikia kwenye hatua hii, maana yake ubora wa utengenezaji wa vifaa viwandani nao una changamoto zake.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)