Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MANDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hizi zilizopo mezani na mimi nichukue fursa hii kuwapongeza sana wenyeviti wa Kamati hizi mbili kwa taarifa zao. Niwapongeze sana wachangiaji waliochangia kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuishauri Serikali kwa niaba ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, kwenye Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali ukurasa wa 40 kulikuwa na hoja ya Mradi wa Urasimishaji wa Makazi. Serikali mwaka 2013 ilikuja na mpango wa miaka kumi wa kurasimisha makazi holela kwa maana yako maeneo mengi hasa Dar es salaam na miji mingi mikubwa ambayo tayari makazi yalijengwa bila kupangwa na kupimwa.

Mheshimiwa Spika, mradi huu ulikuja kama suluhu ya kuunganisha nguvu, kwa maana ya kutumia kampuni binafsi za upimaji na upangaji kama wataalamu na kuziba lile gap la upungufu wa wataalamu, kutumia wananchi kuchangia zoezi zima la kupanga na kupima, lakini pia Serikali kuratibu. Zoezi hili likikamilika litasaidia kuongeza mapato lakini pia kupunguza migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Spika, ardhi kwa mujibu wa sheria zilizotungwa na Bunge lako zinapaswa kumilikiwa kisheria. Umiliki wa ardhi mijini unasimamiwa na Sheria Na. 4 ya mwaka 1999, na kila mtu anayeishi kwenye eneo lililopangwa na kupimwa atamiliki ardhi yake kwa hati, na ndio umiliki ambao Serikali imekuwa ikihimiza kupitia Mradi wa Urasimishaji, na hii inaondoa migogoro kwa sababu umiliki huu huu wa kienyeji, nimetumia lugha ambayo si sahihi; ni umiliki wa haki ya Mungu, kwamba ili umthibitishie mtu unamiliki ni lazima uapie. Hata hivyo, zoezi la urasimishaji lilienda kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, nilitaarifu Bunge lako mpaka kufikia mwezi Januari, 2024 jumla ya vipande vya ardhi 2,400,000 vimetambuliwa na viwanja 2,500,000 vilikuwa vimekwishapangwa kwa maana ya TP Drawings. Kati ya hivyo, viwanja 1,400,000 upimaji wake umekamilika, kwa maana ya survey, na viwanja 1,100,000 sawa na asilimia 42 bado havijakamilika.

Mheshimiwa Spika, niombe pia kupitia Bunge lako niseme kwamba katika pesa ambazo zilikadiriwa kukusanywa ili zoezi hili likamilike, shilingi bilioni 331 ni bilioni 72 tu ndizo zimechangwa na wananchi, na ndiyo maana zoezi hili limekuwa linakwenda kukwama.

Mheshimiwa Spika, sasa ni nini suluhu? Suluhu namba moja, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekwishatoa maelekezo, na kupitia Mradi wa LTIP zimetengwa jumla ya dola milioni 62; zile dola milioni 21 alizosema Mheshimiwa Mtemvu ni kiasi cha fedha hizo na mradi huu unakwenda kukwamuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo maeneo yote na tumeanza na Dar es salaam, hapa Dodoma tumekwishafanya pilot, jimbo la Mtemvu yeye ni shahidi litakuwa la kwanza pale Dar es salaam na kazi kubwa inafanyika.

Mheshimiwa Spika, zoezi hilo la ukwamuaji linakwenda pamoja na kliniki za ardhi ambazo ukiangalia kwenye viwanja hivi 1,400,000 vilivyopimwa, ni ankara 623,000 tu ndizo zimeanza kufanyiwa process za kupata hati na ni hati 230,000 tu zimemilikishwa. Sasa kutoka viwanja 1,400,000 mpaka hati 230,000 ni namba ndogo lakini kliniki hizi zinamsogezea mwananchi huduma karibu zaidi na zinampunguzia urasimu wa kufuatilia hati. Hivi ninavyozungumza kliniki iko pale Kibo – Tegeta; na kuanzia Jumatatu tarehe 29 mpaka tarehe 25 kliniki ya ardhi itakuwa pale Bunju kwenye Wilaya ya Kinondoni. Hiyo wiki moja ni ile wiki ambayo na Wizara ya Ardhi kwa maana ya Waziri na watendaji wa makao makuu watakuwa pale Bunju kwa ajili ya kutatua migogoro ya ardhi pamoja na kuendelea kukwamua zoezi hili la urasimishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilithibitishe Bunge lako kwamba Wizara imejipanga, uongozi thabiti wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, umekwishatupatia maelekezo na pesa zipo. Ninaamini kwenye ripoti zijazo za CAG na ripoti zijazo za Kamati, zoezi la urasimishaji litakuwa limefika mahali pazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kulishukuru Bunge lako kwa miongozo na maelekezo mnayotupatia na wakati wote Serikali iko tayari kwa maelekezo, ushauri wa Bunge na wakati wote tunachukulia very serious ripoti hizi za Kamati na michango ya Wabunge wote waliochangia tumechukua na tutaifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kadri ya ratiba ya Bunge kwenye vikao vinavyokuja, tutakuwa tukitoa taarifa ya zoezi la urasimishaji na mazoezi mengine ya ardhi ili kuweza kuhakikisha kwamba kero za ardhi zinafika mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru tena na ninaunga mkono hoja. (Makofi)