Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima. Pia nakupongeza wewe kwa namna ambavyo unakiongoza kikao hiki vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri na njema, ya maana anayoifanya kwa Watanzania, kwa bajeti ambazo amekuwa anatuletea hapa na sisi tukizipitisha na namna ambavyo zinaonyesha matunda chanya kwa Watanzania wa mijini na vijijini. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye leo bajeti yake ndiyo tunaijadili hapa. Amekuwa ni mtu mwema, mchapakazi, msimamizi mwema na msaidizi mwema wa Mheshimiwa Rais na Watanzania wote. Nampongeza kwa jambo hilo na ninaomba nitumie nafasi hii kumtia moyo yeye na Waheshimiwa Mawaziri wanaofanyanao kazi ofisini kwake; Mama yangu Mheshimiwa Jenista na Manaibu wake wote, Mheshimiwa Deogratius na Naibu Mawaziri wengine wote kwa kazi nzuri wanayoifanya. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mniruhusu nizungumze maneno machache ya kushauri namna bora ya kuwahudumia Watanzania, na kwa sababu leo tunazungumza na Ofisi ya Msimamizi wa Mawaziri wote, naamini kupitia yeye watanielewa na kutekeleza yale ambayo nitayashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilichonileta humu ndani ni wananchi wa Sumve ambao walinipigia kura, na kuna mambo niliwaambia nitafanya kwa kushirikiana na Serikali kwa kuishauri. Sasa yale mambo ambayo tumekuwa tukiwashauri na kusimamia Serikali, tunashukuru yamefanyika mengi, lakini kuna jambo la msingi sana kwenye Jimbo la Sumve naliona kama vile haliko sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii ni ya kwetu sote. Watanzania wote tunalipa kodi na tunategemea maendeleo yanapokwenda kwa Watanzania yaende walau kwa kuangalia kila eneo linapata nini? Maendeleo yanapokuwa yanajazana labda Dar es Salaam, tunaona sijui trilioni ngapi zinajenga mwendokasi, halafu Sumve tangu niwe humu, leo ni mwaka wa nne huu Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waheshimiwa Mawaziri wake wamekuwa wakinisikia nikisema kwamba kuna Jimbo kule linaitwa Sumve halina hata milimita moja ya lami. Halafu nikimaliza kuongea hivyo, anatokea Mheshimiwa Waziri anayehusika anatoa ahadi lukuki na hatekelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeanza kuzungumzia suala la Wilaya yetu ya Kwimba kuunganishwa kwa lami na Mkoa wa Mwanza tangu nilipoingia humu, sioni utekelezaji, naona majibu yasiyotekelezwa. Nimeanza kuhangaika na Mheshimiwa Dkt. Chamuriho akiwa Waziri wa Ujenzi, akawa ananikalisha pale kwenye kiti chake kila siku ni ahadi lakini hakuna kitu. Nikaenda kwa Prof. Mbarawa, akapata hiyo nafasi, tena yeye tulikwenda ofisini kwake Wabunge wote wa Mwanza, tukaahidiwa, lakini hakuna kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi yupo kaka yangu Mheshimiwa Bashungwa, naye hakuna kitu. Nikiongea nao wananiambia michakato ya manunuzi, na kadhalika. Yaani wananchi wa Sumve na watu wa Kwimba hawajui hayo mambo ya upembuzi yakinifu na hayo manunuzi. Wanachojua ni lami itokee Magu ipite Bukwimba iende mpaka Hungumalwa, tuunganishwe na sisi. Wanachojua ni lami itokee Fukalo ije Nyambiti iende Malya ili iunganishe na mnyororo wa utalii wa Mbuga ya Maswa na Mbuga ya Serengeti tufaidike na utalii. Sasa hatuwezi kuendelea hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka nikichangia bajeti yangu ya pili, kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, Waziri wa Fedha wakati ule aliniandikia mpaka memo ya kuniambia kwamba, tunajenga hivi na hivi. Baadaye tena wakasema sijui wanakopa nini? Yaani hawajengi, kila siku ni story tu. Sasa wananchi wa Sumve wameniambia hivi, ukifika Bungeni kwa heshima waliyonayo na Ofisi ya Waziri Mkuu na namna ambavyo mambo yanakwenda, wewe nenda ukaunge mkono bajeti ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama itafika bajeti ya ujenzi, halafu hakuna mambo yanayoeleweka, usiiunge mkono. Watu wa Ujenzi niko very serious kwenye hili. Very serious, na sitaki mchezo. Wananchi wa Sumve wanataka na wenyewe wawe na lami. Haiwezekani ninyi kwenye Majimbo yenu mna lami, sisi hatuna halafu bado tunakuja humu wote tunaitana Wabunge. Ni lazima tuheshimiane kabisa. Hatuwezi kuwa tunakuja hapa tunaahidiwa vitu ambavyo havitekelezwi. Haiwezekani. Ni bora sasa sisi watu wa Sumve tuambiwe hatuhusiki humu. Kitu cha msingi hapa tunataka lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu waambie Mawaziri wako wanaohusika, waache kuwapa ahadi hewa watu wa Sumve. Nami Mbunge wa Sumve sitaki ahadi hewa kwa niaba ya wananchi wangu. Tunataka na sisi tujengewe barabara ya lami, story za kilometa 10 mnazotuambia ambazo na zenyewe hamjengi, sisi hatuko interested na kilometa 10 za kulambishwa lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka lami ambayo itatufanya na sisi tuweze kwenda mjini na magari yetu mazuri, lakini hii namna ya kutufanya sisi tuwe tunatuma nginjanginja, ninyi mnatanua na magari mazuri mjini, haipo. Watu wa Sumve wameniambia kuhusu miundombinu mtatusamehe, tunataka barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hilo naomba nihamie kwenye suala lingine la ushauri tu. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamezungumza hapa kuhusu suala la kikokotoo. Kwanza, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa hatua ambazo amezichukua na maelekezo ambayo amekuwa akiyatoa na kuonesha moyo na nia ya kutamani jambo hili liende na liishe vizuri ili watumishi wetu waishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kikokotoo linakuja kwenye hoja ya kwamba ukiliangalia kwa undani lina hoja, kwamba watumishi wetu uwezo wao wa kutunza pesa na kupanga matumizi ya pesa ni mdogo. Ndiyo hoja ya kikokotoo inakuja hapo. Yaani watu wakipewa hela zao hawataweza kuzitumia vizuri, hawatazitunza vizuri, kwa hiyo, sisi Serikali tuwatunzie, tutawapa kidogo kidogo. Ndiyo hoja yenyewe ukiiangalia ukubwa wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka tujadiliane hapa kwa kushauriana, hawa watumishi ndiyo leo wako kwenye maofisi, ndiyo leo wanatuletea makabrasha yote tunajadili bajeti hapa, ndiyo leo wamepanga kila kitu huko, ndiyo hao wanaolinda nchi yetu na ndiyo hao wanafanya kila kitu, lakini tukifika wakati wanastaafu sasa, maana unajua huwa tunasema kwenye utumishi tunataka experience. Hawa watu mpaka wamestaafu wana uzoefu na matumizi ya pesa, wana uzoefu na maisha na wanajua wanafanya nini. Eti sasa wakishazeeka tunawaona hawa hawawezi kutunza pesa zao, tuwatunzie tuwe tunawapa pole pole. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye logic inaonekana kwamba siyo jambo jema. Jambo hili sisi tunasema ni zuri. Kuna wakati niliambiwa hapa sijafanya utafiti, lakini ukweli ni kwamba huko site hili jambo halijaingia kwenye vichwa vya watumishi, yaani limefeli na hawalielewi na wale ambao wamelazimika kuingia kwenye kikokotoo, wengi imewa-frustrate, wengi wanakufa kabla ya muda.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kasalali, ahsante sana.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iliangalie jambo hili kwa jicho lingine. Nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)