Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii ili nami nitoe mchango wa mawazo kuhusiana na bajeti ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe pongezi za dhati kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu pamoja na timu yake yote ambao wamewasilisha bajeti yao vizuri, bajeti ambayo imesheheni mambo mengi ambayo yanaenda kulisukuma Taifa hili katika maendeleo ya dhati.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumshukuru Mheshimiwa, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kile ambacho amekifanya kwenye maendeleo ya kilimo kwa msimu ambao umeisha. Tulipitisha bajeti iliyopita ya 2023/2024, fedha ziliongezwa kwenye kilimo na tumeona mikakati mingi ambayo Serikali imeifanya ikiwemo ujenzi wa mabwawa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na mengine mengi ambayo yataleta tija kwenye kilimo chetu, ukizingatia kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa letu. Kwa hiyo, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika pongezi hizo, nitoe mfano wa kile ambacho Serikali imekifanya. Kwa mfano, wakulima wa zao la korosho katika nchi yetu ya Tanzania, kwa msimu wa 2023/2024 Serikali ilijitahidi kutoa pembejeo bure kwa wakulima ili kuongeza uzalishaji kama vile ambavyo iliahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hilo, tunashukuru sana kwamba kwa mfano kwenye zao hilo la korosho uzalishaji umeongezeka kidogo tofauti na msimu wa mwaka 2022/2023. Msimu huu wa mwaka 2023/2024 kutokana na kutolewa kwa pembejeo ambazo zilikuwa bure, ongezeko lipo. Tunaishukuru sana Serikali kwa sababu hali ya wananchi wetu katika mifuko ilikuwa ni ngumu na hivyo wasingeweza kupulizia. Wananchi wengi wanaolima korosho katika nchi hii wamenufaika na pembejeo zile, na zao la korosho uzalishaji angalau umeongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Mtwara, ukienda kwenye Chama Kikuu cha Ushirika cha Watu wa Tandahimba na Newala (TANECU) kwa msimu wa mwaka 2022/2023 uzalishaji ulikuwa ni tani 33,000 peke yake, lakini kwa msimu huu wa 2023/2024 zimeongezeka tani 33,000 na kufanya uzalishaji kuwa tani 74,000. Tunaishukuru sana Serikali kwa sababu hali hiyo isingefikiwa. Hicho ni chama kimoja tu, ikija kuunganishwa kwa Tanzania nzima kwa zao la korosho, basi tutaona ongezeko litatofautiana sana na lile la msimu wa mwaka 2022/2023. Tunaishukuru Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ongezeko hilo, nashukuru pia kwenye hotuba ambayo tumeletewa iliyopo mbele yetu, ukienda aya ya 46 inasema: “Pamoja na mambo mengine Serikali itahakikisha kilimo kinakuwa na faida kwa kuhamasisha uongezaji wa thamani kwenye mazao na upatikanaji wa masoko ya uhakika ndani na nje ya nchi.” Tunashukuru sana kwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee hapo. Pamoja na uzalishaji kuongezeka, hili ambalo Serikali imelisema la kutafuta thamani ya mazao pamoja na kutafuta masoko ndani na nje ya nchi, ndipo changamoto ilipo kwa wakulima wetu wengi; na mazao mengi yanakwama kwenye masoko. Ukienda kwa watu ambao wanazalisha mpunga, wanazalisha mpunga mwingi lakini unakuta wanakwama kwenye bei. Ukienda kwenye korosho, halikadhalika, uzalishaji ndio huo, lakini kwenye bei inakuwa ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, msimu huu ambao umeisha, huu wa mwaka 2023/2024 changamoto ya bei imekuwa ni kubwa mno kwenye zao la korosho, bei iko chini. Pamoja na bei kuwa chini, kuna utitiri wa tozo ambazo zinamkumba mkulima wa korosho. Naiomba Serikali yangu tukufu ambayo inasikia, ijaribu kutafuta namna ya kupunguza tozo kwa sababu mkulima anachopata ni kidogo, lakini tozo zimekuwa nyingi kiasi kwamba sasa kile anachokipata pamoja na udogo wake chote kinaishia kwenye tozo. Kwa hiyo, kunakuwa na tofauti kubwa kati ya zile gharama za uzalishaji kuanzia palizi, upuliziaji mpaka kuja kuvuna na kile ambacho mkulima akienda kuuza anakuja kukipata kama take home.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iangalie, ikae chini itafakari suala la tozo ili mkulima apate angalau kitu ambacho kitamfariji, kwa sababu sasa hivi kwa kweli imekuwa ni chanagamoto kubwa. Hapo niseme tu, lawama kubwa tunaibeba sisi ambao ni wawakilishi wa wananchi. Kwa hiyo, Serikali iendelee kututafutia masoko na pia kuangalia hizi tozo kwani zimekuwa kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye zao la korosho kunakatwa Export Levy. Export Levy ilivyokatwa, tunashukuru baadhi ya matunda tumeanza kuyaona ikiwemo na pembejeo. Basi naiomba Serikali ifanye kitu ambacho Export Levy itakuja kumnufaisha mkulima wakati anauza zao lake kwa sababu kwa kweli hali imekuwa siyo yenyewe. Hali hii ni kwa sababu sisi bado tunategemea kuuza korosho ghafi, hicho ndicho ambacho tunakwama nacho. Uuzaji wa korosho ghafi ndiyo unaotufikisha hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua jitihada za Serikali za kuweka mpango wa kutengeneza au kuanzisha industrial park ambayo itachakata korosho zote hapa ndani na hatimaye tuuze korosho ambazo siyo ghafi tena, lakini, hiyo ni long term plan. Short term plan lazima tuitafute. Masoko ya korosho yanatafutwa kipindi msimu tayari umeshatangazwa wa kuuza korosho. Kwa hiyo, inakuwa kama kuna uharaka fulani, matokeo yake tunaenda kuangukia kwa wanunuzi ambao wanatulalia kwenye bei. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa sababu imeshaweka kwenye mikakati kutafuta masoko ya bidhaa zake za kilimo, basi ifanye mapema kabla ya msimu kutafuta wanunuzi. Kwa sababu, kama itafanyika mapema, ule uharaka haraka ambao mara nyingi hauna baraka utapotea na mkulima yule ataenda kunufaika na soko la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine niongelee suala la maji. Nashukuru sana Serikali yetu inafanya jitihada kubwa sana kuhakikisha kwamba suala la maji linafikia hatua nzuri. Katika Sera yake ya Maji inasema ifikapo 2025, basi kwa wale ambao wanaishi mijini wapate maji safi na salama kwa asilimia 95 na wale ambao wako vijijini wapate maji safi na salama kwa asilimia 85 ifikapo 2025. Katika kufikia hilo, tunaona juhudi ambazo Serikali imekuwa ikizifanya ili kuhakikisha kwamba maji safi na salama yanapatikana kwa wananchi wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hilo namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sababu kulikuwa na mradi wa miji 28. Mradi ule ulisuasua sana, lakini bahati nzuri ukasainiwa mwaka juzi, 2022 na umeanza utekelezaji katika baadhi ya maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wananewala ni wanufaika wa huo mradi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante. Kengele ya pili hiyo.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi