Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye Ofisi hii muhimu sana. Kwanza, wazee wetu waliwahi kusema kwamba kupanga ni kuchagua. Kwa hili nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kuitenga Ofisi hii ya Rais, Mipango na Uwekezaji kusimama peke yake na kumpa mtu makini kabisa, Profesa Kitila Mkumbo kuisimamia. Namwamini Profesa na naamini kwamba anakwenda kutuongoza vizuri na kuweka mipango ya nchi yetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sensa tuliyofanya mwaka 2022 inaonesha kwamba 76% ya Taifa hili ni vijana chini ya miaka 35. Kwa maana hiyo nilitegemea kwamba mipango yote ambayo tunaipanga sasa hivi katika kila sekta kwa asilimia kubwa ni lazima izunguke kundi hili kubwa, 76% ni nyingi sana na katika hili ningependa sana tuangalie changamoto ambayo ni ya kwanza kabisa kwa vijana wa Taifa hili, changamoto ya ajira.

Mheshimiwa Spika, katika mipango yetu ni muhimu tukawaelekeza vijana kwamba nchi hii inakwenda wapi na wao waendeje. Ni muhimu kwa sababu sidhani kama kuna afya kuliacha kundi hili lijiindee katika karne hii ya 21 kuji-surprise na kuwa na kesho ambayo hawaitambui; kwenda na kutegemea kwamba tutaikuta kesho na tutapambana nayo tutakavyoikuta, sitegemei hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo? Katika nchi yetu sasa hivi kuna maeneo matano ambayo tunayaona kulingana na projections zake, utashi wa viongozi wetu na maendeleo ya sekta hizo, kwamba ni sekta ambazo zitaendelea ku-boom kwa miaka 20 mpaka 50 inayofika. Kuna sekta za utalii, viwanda, kilimo, uchukuzi na sekta ya uchimbaji. Nategemea katika mipango yetu tuoneshe ni namna gani tumejipanga kulielekeza kundi hili kubwa. Kwanza katika namna ya uelimishaji wake kwenda ku-tackle mabadiliko watakayoyakuta katika sekta hizi, lakini pili kuangalia namna gani tuna wa-groom kuendana na mabadiliko ya nchi hii katika sekta hizi.

Mheshimiwa Spika, leo hii tunaongelea biashara katika eneo huru la Afrika ambapo Afrika nzima, nchi zaidi ya 50 zitakuwa na soko huru la pamoja. Lazima katika mipango yetu tuoneshe ni namna gani tunakwenda kuwa-groom vijana wetu kupambana na uhuru huu ili kuweza kunufaika na eneo hili huru la biashara la Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ni lazima Wizara hii ituambie, je, inafurahishwa na vijana ambao wanatoka katika vyuo na vyuo vikuu vyetu katika nchi hii? Kama sivyo, je, tunaingiaje katika mpango wao wa kuweza kutuinua na kutuweka sawa ili leo hii tunapokuwa tunaongelea dira ya mpaka mwaka 2050 tuone namna gani vijana tunafika 2050 tukiwa imara?

Mheshimiwa Spika, katika taarifa ya Profesa, anatuonesha namna ambayo amechukua maoni sehemu mbalimbali za nchi hii kwenye Dira hii ya 2050, waliotoa maoni haya 80% ni vijana kati ya miaka 15 mpaka 35. Hii inaonesha kwamba moja, vijana wanataka sana sana kushiriki kwenye kushauri namna Serikali na nchi yao inavyoenda na mbili, wanapenda na wao wahusishwe kwenye mipango ya nchi hii. Kwa hiyo naiomba sana Ofisi hii katika kupanga mipango yake na namna inavyoshauri sekta mbalimbali, isilisahau kundi hili muhimu sana la vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hayo, nizungumzie sekta ya kilimo. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Leo hii tunakwenda kuzungumzia sekta ambayo tunaitengea zaidi ya trilioni moja kwenye bajeti, kwa hiyo ni lazima tuonyeshe ni namna gani sekta hii inakwenda kutusaidia kuzalisha zile ajira milioni tatu zilizokuwa zimeahidiwa tangu mwanzo. Tuna Miradi kama ya BBT, naomba sana katika mipango yetu tuoneshe ni namna gani tunakwenda kushusha Mradi wa BBT kwenda kuwa localized kwenye wilaya na mikoa yetu. Hii itatuondolea sana changamoto na malalamiko ya vijana wengi kwamba wameachwa nje ya mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna maeneo ambayo yalikwishatolewa maelezo na Mheshimiwa Waziri Mkuu yatengwe kwenye kila halmashauri zetu ili kuhakikisha kwamba vijana wanapewa maeneo hayo kujiendeleza wao wenyewe. Maeneo haya yatumike kwenye miradi hii ili vijana kwenye wilaya zetu na mikoa yetu, waende kunufaika huko moja kwa moja na ndipo tutakapoona hizi ajira milioni tatu zinazalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunazungumzia bajeti ya trilioni moja kwa ajili ya sekta hii. Naamini, tusije tukafanya kilimo cha kizamani. Ili tufanye kilimo cha kisasa ni lazima tuuangalie ugani kwa namna ya tofauti sana. Napendekeza tuanzishe mamlaka ya ugani kama tulivyoanzisha TARURA na RUWASA, ili kusudi mamlaka hii ishuke mpaka vijijini kwenda kuwasaidia wakulima wadogo wadogo kulima kibiashara na kujiongezea thamani ya mazao wanayoyazalisha. Hivi ndivyo ambavyo tunaweza kwenda kweli kukomboa kilimo chetu na kukiweka kwenye value sawasawa na bajeti tunayoitengea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inabidi vilevile tuwekeze kwenye value addition, lazima tuwekeze kwenye viwanda. Kwenye hili nilikwishashauri ndani ya Bunge hili Tukufu, kwamba ni lazima tutoe incentive kwa Watanzania wanaotaka kuanzisha viwanda katika Serikali zingine za nchi hii tofauti na Dar es Salaam na Pwani. Baba wa Taifa alikuwa na maana kubwa sana kuanzisha viwanda katika kila sehemu kulingana na mazao au na vitu vinavyopatikana kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kitu hatari sana kuona viwanda vyote vya nchi hii, almost 80 percent, viko sehemu moja. Siku maeneo haya yakipatwa na emergency yoyote, maana yake ni kwamba uchumi wa Taifa hili utayumba kwa kiasi kikubwa. Lazima tuoneshwe mipango na incentive gani watatoa kwa Watanzania. Iwe ni incentive za kikodi au mapunguzo ya thamani ya vitu kadhaa ili kusudi waweze kuanzisha viwanda na processing industries katika sehemu mbalimbali za nchi kwa ajili ya kusaidia wale wanaozalisha kule kule waweze kuona tija ya maendeleo haya ya miundombinu ambayo tunafanya kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa pia kushauri, leo hii sisi watu wa Kanda ya Ziwa, tuna Ziwa Victoria. Sasa, ni lazima tuone mipango ya kutumia ziwa hili kuondokana na kwanza, shida ya maji na pili tuwe na scheme za umwagiliaji za kutosha. Ni aibu sana kwa sisi ambao tuna maji ya Ziwa Victoria kuanza kuja humu Bungeni na kulia changamoto ya maji. Tunalia na changamoto ya kwamba, kipindi cha kiangazi hatuwezi kulima ilhali tuna ziwa. Tunaweza kutengeneza irrigation schemes. Lazima kwenye mipango yetu Waziri atupe mpango wa muda mrefu wa kuhakikisha maeneo haya yanazalisha kwa wingi kulingana na rasilimali tulizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina zaidi ya 51% ya Ziwa Victoria, kwa hiyo ni lazima tujue ni kwa namna gani tunakwenda kulitumia ili kukuza uchumi wetu hasa wa maeneo ambayo yanazunguka eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, kwenye sekta ya nishati nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sababu ameonesha dhima na nia ya moja kwa moja ya kufanya Watanzania tuanze kutumia nishati safi. Katika hili nampongeza sana. Nampongeza pia Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Watumishi wote wa Wizara kwa scheme waliyoifanya ya kugawa mitungi ya gesi katika sehemu mbalimbali. Nawapongeza kwa sababu nimefuatilia katika bajeti watakayoileta katika Bunge hili Tukufu wamekwenda mbele zaidi, kuona ni namna gani tutapeleka nishati ya gesi asilia vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunagawa mitungi ya gesi lakini si Watanzania wengi watakaokuwa na uwezo wa kwenda ku-refill mitungi ile ikiisha. Ni lazima tutafakari namna gani tutakuwa na uendelevu wa project hii, hasa kwenye jamii za ufugaji. Wao tayari nishati ya kuzalisha hii gesi asilia wanayo ya kutosha na gharama yake ni nafuu. Tutenge bajeti twende tukawekeze huko ili tuwe na uendelevu wa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kitu kinaitwa economies of scale; nilitegemea, kwa sababu sasa hivi kuna matumizi makubwa sana ya hii nishati safi, basi angalau gharama ya gesi ingeshuka kulingana na matumizi yake makubwa. Naomba sana pia kwenye mipango tuliangalie hili la namna gani ya kushusha nishati hii ya gesi ili wengi waweze kuipata kwa wepesi. Kwa sasa hivi inatumika kwa wingi na kwa economies of scale, naamini kwamba tunaweza tukashusha. Tusije tukaishia ku-mobilize Watanzania kutumia nishati safi, lakini tukapandisha faida na kuwanufaisha watu kadhaa; wakati tungeweza kushusha na kufanya Watanzania wengi zaidi wakatumia nishati hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya mwisho ni kwenye suala zima la uwajibikaji na utawala bora. Kwenye hili nampongeza sana Profesa kwa sababu katika hotuba yake, ameelezea misingi 10 ambayo ataisimamia kwenye Ofisi yake. Msingi namba nane amesema nidhamu katika matumizi ya fedha za umma na msingi namba 10 amesema ni kusimamia mipango tutakayoipanga na kuitekeleza. Kwenye hili amenipa imani kubwa sana. Nimwombe sana Profesa ili tuweze kufikisha au kufikia kule tunakopanga kufikia ni muhimu sana tukaimarisha nidhamu katika matumizi ya fedha za umma. Kwa kufanya hivyo tu ndiyo itatuwezesha kufikia huko, kwa sababu tukiendelea kupanga mipango mizuri lakini fedha ambazo zinaenda kutimiza mipango hiyo hazifiki kule zinakotakiwa, naamini tutakuwa na mkwamo mkubwa sana katika mipango hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)