Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo kwa hotuba nzuri ya bajeti. Pia niwapongeze wasaidizi wake Wizarani kwa jinsi ambavyo wanasukuma ajenda za uwekezaji hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita kwenye masuala yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza naishauri Serikali isimamie vyema utekelezaji wa Sera ya Uwekezaji ili kuisaidia nchi yetu kuzalisha kwa kutumia rasilimali tulizonazo na kutuletea maendeleo makubwa na kuongeza pato la Taifa. Pa kuanzia ni vyema Serikali ikabiliane na vikwazo vinavyoikabili Sekta ya Uwekezaji ambavyo baadhi ni vikwazo vya kikodi, vikwazo visivyo vya kikodi, vikwazo vinavyohusiana na utaratibu wa masuala ya uwekezaji na vikwazo vya wezeshaji uwekezaji hasa wale wa ndani. Kama Serikali itaangalia kwa makini vikwazo hivi, itakuwa imeweka mazingira wezeshi ya uwekezaji ili kuwawezesha wadau kushiriki kwa mafanikio na kufurahia matunda ya kuwekeza.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili, utahusu maeneo ya kimkakati ambayo Serikali inatakiwa kufungua fursa za uwekezaji kwa wadau mbalimbali. Nchi yetu imebarikiwa kuwa na maeneo makubwa yanayoweza kutumika kuzalisha mazao mbalimbali ya kimkakati. Maeneo mengi ya Tanzania hupokea mvua za kutosha na pia yana maji yanayoweza kutumika kumwagilia na kuzalisha mazao, kwa mfano, maeneo ya Iringa, Mbeya, Njombe na West Kilimanjaro yana maeneo makubwa yanayofaa kuzalisha mazao ya kimkakati ya ngano na shayiri ambayo yana soko kubwa la ndani na kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kwenye Sekta ya Mafuta ya Kupikia, nchi yetu ina uwezo mkubwa wa kuwekeza kwenye kilimo cha mazao ya mafuta ya kupikia kama vile alizeti, michikichi, karanga, ufuta na nazi. Uwekezaji huu kwenye kilimo ni vyema ukaenda sambamba na uanzishaji wa viwanda vya kuyaongezea thamani mazao hayo ili tuzalishe mafuta yetu na kuyauza ndani na nje. Kuna uwezekano mkubwa sana wa kuvutia wawekezaji wa sekta ya mafuta ya kula katika Mikoa ya Singida, Tabora, Dodoma, Simiyu, Kigoma, Manyara, Lindi, Mtwara, Pwani na Morogoro.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo uwekezaji wake utakuwa na tija kubwa ni kuwekeza kwenye ujenzi wa viwanda vya mbolea na viuatilifu. Nchi yetu ni nchi ya kilimo na Serikali yetu inatumia fedha nyingi za kigeni kuagiza mbolea na viuatilifu vya viwandani. Soko la bidhaa hizi ni kubwa hapa nchini na kwa majirani zetu. Naishauri Serikali ihamasishe na kuweka mazingira rafiki ya kuwekeza katika maeneo haya ili kulisaidia Taifa na wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Serikali kwa kuboresha huduma za afya kwani hospitali, vituo vya afya na zahanati zimetapakaa nchi nzima. Kutokana na hili, ni wakati muafaka sasa Serikali ikahamasisha uwekezaji katika ujenzi wa viwanda vya dawa kwani soko la ndani lipo na ziada itapelekwa nje. Kwa kufanya hivi, nchi yetu itakuwa imejinasua kwenye tabia ya kuwa mwagizaji wa dawa kutoka nchi ya India na nyinginezo za nje.

Mheshimiwa Spika, fursa nyingine ni kuwekeza katika utengenezaji wa pikipiki hapa nchini. Hii ni kutokana na ukweli kwamba kuna matumizi makubwa ya pikipiki hapa nchini. Vijana wengi wamejiajiri kwenye biashara ya pikipiki. Hivyo basi, kuna umuhimu wa kuwa na viwanda vya pikipiki na ni vyema Serikali ikaweka mazingira mazuri na kuvutia wawekezaji katika eneo hili. Tukiwa na mwekezaji wa kimkakati, bei za pikipiki zitakuwa chini na vijana wataweza kuzimudu.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali itahamasisha uwekezaji kwenye maeneo haya machache niliyoainisha, hii italisaidia Taifa katika safari yake ya kukuza uchumi na kutuletea maendeleo.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.