Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ninapenda kukushukuru na nitoe mchango wangu kwenye maeneo matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, jeshi letu kwa muda mrefu limekuwa likitoa msaada mkubwa sana wa ulinzi ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndani ya Bara la Afrika na nje ya Bara la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika zama za sasa mbinu na medani za kivita zimebadilika sana na kwa maana hiyo basi, tunao wajibu kama Taifa tuliandae vizuri jeshi letu ili likabiliane na changamoto za karne ya 21. Katika karne hii vita vingi vya kimkakati havitapiganwa kwa kutumia mizinga mikubwa bali kama mwenzangu alivyosema hapa vitapigwana kwa kutumia roboti, mifumo ya cyber na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo basi, ninalotaka kulisema hapa ni kwamba tunao wajibu kama Taifa tuangalie changamoto hizo ili tuweze kuwasaidia wanajeshi wetu. Nitataja maeneo matano ambayo Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania lina changamoto:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, mtakubaliana nami katika karne hii maadui wa nchi wanaweza kutumia mifumo ya cyber kuharibu benki, mashirika ya umeme, hospitali, vituo vya hifadhia data na kadhalika, kwa kutumia mifumo ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya pili, maadui wanaweza kuharibu hewa, maji na kwa kitaalamu tunaita biologically and chemically warfare.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya tatu, kadiri nchi yetu inavyoendelea ndivyo mahitaji ya wahandisi mahiri wanavyohitajika hasa katika miundombinu ya bandari, reli za kisasa, viwanja vya ndege na anga.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya nne, ninayotaka kuielezea hapa ni siasa za dunia katika karne hii zitahamia katika Bahari ya Hindi kwa sababu katika Bahari ya Hindi, kuna rasilimali kubwa sana kama mafuta, gesi asilia, madini, samaki na usafiri wa mizigo. Kwa maana hiyo basi mataifa yenye nguvu yatamimika sana katika eneo hilo. Ninapendekeza hapa Majeshi ya Maji katika nchi wanachama wa maeneo hayo wafanye mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kukabiliana na changamoto ya Bahari ya Hindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya tano, Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania limekuwa likishiriki katika misheni mbalimbali za Kimataifa na kusema kweli jeshi letu limefanya kazi nzuri sana, kwa maana hiyo basi pamoja na umasikini wetu kuna haja sisi kama Taifa tuwaandalie vijana wetu malipo mazuri ya fidia kwa wanajeshi ambao kwa bahati mbaya watapata ulemavu wa kudumu na wale watakaopata vifo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, ninaiomba Wizara ya Ulinzi ishirikiane na Chuo Kikuu cha Taifa Muhimbili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Dodoma ili kuandaa vijana wenye taaluma katika kozi nitakazozieleza; kozi za Cyber Security, Space Technology, Military Medicine, Maritime Security pamoja na Mechatronic Engineering ili tupate vijana wenye weledi katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtakubalina nami kwamba nchi yetu sasa inatekeleza miradi mikuu ya kimkakati Bwawa la Mwalimu Nyerere na reli ya Taifa. Miradi hii inahitaji ulinzi wa hali ya juu sana pamoja na mahitaji ya matengenezo ya kiufundi hasa miradi hii itapokamilika. Kwa maana hiyo basi kuna haja ya kuandaa vijana wetu wa jeshi wenye taaluma kwenye maeneo hayo ili miradi hii ikikamilika na yatakapotokea mahitaji ya matengenezo. Tusikimbilie nje kutafuta wahandisi wa nje, bali jeshi letu litoe msaada wa kiufundi na kitaalamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)