Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti,asante sana kwa kunipa nafasi, ili na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Nishati na Madini. Nichukue nafasi hii kwanza kabisa kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Busanda kwa kuniamini na kuendelea kunipa ridhaa na niwahakikishie kwamba nitaendelea kuwatumikia kwa uaminifu wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara kwa ujumla kwa kazi kubwa wanayoifanya. Kikubwa zaidi nimepitia kitabu cha bajeti ambacho kimejieleza vizuri sana katika ila hatua, kwa hiyo, napenda kuipongeza sana Wizara kwamba wameweka mipango mizuri, cha msingi ninachoomba ni utekelezaji wa mipango hii ambayo wameiweka katika kitabu cha bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa umeme nimeona jinsi ambavyo ndani ya bajeti mmeelezea vizuri sana katika aya zote 45 mpaka 49 nimesoma, nimeona jinsi ambavyo Wizara imejipanga kupeleka umeme kabambe katika maeneo ya vijijini. Kupeleka umeme kwa kuhakikisha kwamba wanaangalia taasisi muhimu katika maeneo hasa ya vijijini, kwa hiyo, hilo nalipongeza sana naipongeza Wizara, niombe tu muhakikishe basi muweze kutekeleza kulingana na mipango yenu mliyoiweka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha pili, katika bajeti hii nimeona pia kuna ongezeko kubwa sana la fedha za bajeti za umeme vijijini kutoka shilingi bilioni 357 mpaka shilingi bilioni 534, ongezeko la asilimia 50. Kwa hiyo, ninaona jinsi ambavyo Wizara kusema ukweli imejipanga kufanya kazi kubwa na nina uhakika kwamba kupitia bajeti hii ya mwaka 2016/2017 wananchi wengi wataweza kunufaika zaidi.
Niombe sasa kulingana na mipango ambayo tumeipeleka, kwa sababu mimi nimeenda katika Mkoa wangu kupitia Ofisi ya TANESCO tumeweza kubaini vijiji ambavyo havijafikiwa na umeme. Niombe sasa Serikali iweze kutekeleza kulingana na jinsi ambavyo wamepanga ili tuweze kuona wananchi wanaweza kunufaika zaidi na upatikanaji wa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika jambo la sekta ya madini ni kwamba katika upande wa madini, nimeona pia jinsi ambavyo Serikali imejipanga katika kuhakikisha kwamba inasaidia wachimbaji wadogo wa madini. Imesema kwamba mtapeleka mitaji kwa ajili ya kuwawezesha wachimbaji wadogo, niiombe Serikali iweze kulifanyia kazi hili, ni kilio cha kila siku. Kwa hiyo ninaomba Serikali iweze kuendelea kuwekeza, imetenga kweli shilingi bilioni 6.6 ni fedha nyingi, niombe Serikali ihakikishe inalifanyia kazi suala hili kusaidia wachimbaji wadogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko sehemu ambapo wachimbaji wadogo wako wengi sana na mara nyingi hili bado ni lalamiko kubwa kwa wachimbaji wanyonge wadogo wadogo. Kwa hiyo, niombe Serikali pia inapotekeleza majukumu yake, itushirikishe na sisi Wabunge ili tuone kwa sababu malalamiko Wabunge ndio tunaoletewa kila siku kwamba mbona sisi hatujapata mitaji, lakini kwenye utekelezaji tunaona jinsi ambavyo Serikali inafanya kazi kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kule kwa wananchi hatuoni hayo mambo, kwa hiyo niombe Serikali safari hii hizo shilingi bilioni sita ilizotenga, ikumbuke pia na wachimbaji wadogo wadogo wa Mkoa wa Geita hasa kule busanda ambako nina wachimbaji wadogo wengi ambao wanajikimu kwa kupitia shughuli za uchimbaji wa madini.
Vilevile katika suala la madini nichukue nafasi hii kwa kweli kuishukuru Serikali, kumshukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri wamefika Geita mara kadhaa. Kulikuwa na changamoto kubwa sana pale Nyarugusu STAMICO kwa mara ya kwanza katika bajeti ya mwaka huu, nimeona Serikali imezungumzia namna ambavyo inakwenda kutatua mgogoro huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na imesema kwamba katika mwaka 2016/2017 Serikali inaenda kumaliza hasa huu mgogoro na wananchi wataweza kupewa eneo la STAMICO. Jambo hili naipongeza Serikali na niombe utekelezaji sasa uweze kufanyika katika mwaka huu wa 2016/2017 na wananchi wana furaha kubwa sana kutokana na jambo hili kwa sababu imekuwa ni kilio cha muda mrefu. Miaka mitano iliyopita kila bajeti nilikuwa nikizungumzia suala hili. Kwa hiyo, mwaka huu mkitekeleza jambo hili, mimi nina uhakika wananchi wote wa eneo hilo la Busanda wataweza kunufaika, na sio tu wa Busanda kwa sababu masuala ya uchimbaji wanakuja watu kutoka sehemu mbalimbali na wanakuwa katika maeneo yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe Serikali katika hiyo aya ya 139 imezungumzia habari ya kuwapatia eneo la STAMICO watu wa Nyarugusu, ninaipongeza na naomba Serikali iweze kulifanyia utekelezaji suala hili ili wananchi waweze kufanya kazi zao sasa, waweze kufanya kazi na kunufaika zaidi katika kuwekeza katika shughuli za uchimbaji wa madini katika eneo hilo. Lakini vile vile Serikali iliahidi kwamba ingeweza kujenga kituo kikubwa sana cha wachimbaji wadogo eneo la Lwamugasa, jambo hili limekuwa ni la siku nyingi lakini katika bajeti nimeangalia Serikali inajenga vituo saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika maelezo nimeangalia Mkoa wangu haupo, niombe Serikali sasa iniambie wakati wa majumuisho, kwamba kituo cha Lwamugasa kimemezwa na nini hakipo tena na wala hakisikiki. Niombe muweze kuangalia bajeti zenu za nyuma na muhakikishe wananchi wa maeneo haya waweze kujengewa hicho kituo cha kuweza kuwasaidia wachimbaji wadogo wadogo. Hasa katika maeneo hayo ili waweze kunufaika na ruzuku, kwa ajili ya kununua zana mbalimbali za kufanyia kazi katika shughuli zao za uchimbaji wa madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba suala hilo liweze kufanyiwa kazi kwa kiwango kikubwa kwa sababu ni ahadi ya Serikali ya muda mrefu na ninyi wenyewe mliahidi, hatukuwa tumeomba lakini ninyi wenyewe mliweka kwenye utaratibu. Lakini vilevile kuna kituo mlianzisha pale Lwamugasa tulifanya uzinduzi wa Benki ya Dunia kwamba ingeweza kusaidia wachimbaji wadogo, tumezindua tu lakini sasa hakuna kunachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba Serikali pia inipe majibu kwamba inasemaje kwa habari ya hicho kituo cha Lwamugasa, ambacho Benki ya Dunia ilikuwa imekubali kuweza kutoa fedha kwa ajili ya kusaidia wananchi wachimbaji wadogo katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niiombe Serikali iweze kuyazingatia hasa eneo la STAMICO Nyarugusu ambalo limekuwa ni kilio cha muda mrefu. Waheshimiwa Marais waliopita wamlizungumzia na kuahidi sana na Mheshimiwa Rais Magufuli alivyokuwa anafanya kampeini zake alisema suala hili limekwisha. Kwa hiyo naomba suala hili liishe lifike mwisho, ili wananchi waweze kufanya kazi zao sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nilikuwa naomba kuzungumzia suala la afya katika sehemu za migodi. Ni kwamba nilikwenda workshop moja wiki iliyopita ya SADC, kuna suala la afya ambalo ni la msingi sana nilikuwa naomba Wizara iweze kulifanyia utafiti, inaonesha kwamba watu wanaoishi katika maeneo ya shuguli za uchimbaji wa dhahabu kuna vumbi la madini ya silica ambalo mara nyingi linasababisha ugonjwa unaitwa silicosis lakini vilevile inasababisha TB.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi niliogopa sana na kushtuka, kwa hiyo, niombe Serikali iweze kufanyia kazi ili wananchi wetu wasije wakaathirika na jambo hili. Kwa hiyo kupitia Wizara ya Nishati na Madini na Wizara ya Afya mjaribu kufanya utafiti wa kutosha ili kuweza kubaini kama kweli hiyo silica ina-affect vipi wananchi wetu katika maeneo ambayo yako karibu na uchimbaji wa dhahabu. Ninaomba suala hili Serikali ilifanyie kazi kwa karibu ili tusije tukajikuta wananchi wetu wanathirika kwa kiwango kikubwa kutokana na uwepo wa silica, ambao pengine wanakuwa wanaathirika na TB bila kujua na hatimaye baadae tukakosa nguvu ya Taifa, kwa sababu watu wataweza kuangamia kutokana na ugonjwa huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkifanya hiyo tathimini na kuweza kuitolea ufafanuzi pengine itatuwezesha sisi pamoja na wananchi kwa ujumla kuweza kujua tatizo na kuweza kutafuta namna ya kujikinga ili kuweza kuondokana na kuweza kupata madhara hasa ya ugonjwa wa TB na magonjwa mengine ambayo yataweza kupunguza nguvu kazi ya Taifa kwa sababu wakiugua hawawezi kufanya kazi zote na pengine uchumi wa Taifa utaweza kutumika pia kwa ajili ya kupeleka fedha katika matibabu ya TB na vitu vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali ilifanyie kazi hilo kwa sababu katika machimbo ya sehemu za Afrika Kusini inaonesha jambo hili limeweza ku-affect watu wengi na sasa hivi ni kilio kikubwa na linazungumziwa sana katika nchi za Afrika ya Kusini. Sisi nchi ya Tanzania kama ni mojawapo ni vizuri Serikali iweze kuangalia suala hili kwa umakini, kikubwa zaidi kuweza ku-protect watu wetu ambao wataweza kuathirika na jambo hili kiafya.
Lakini vilevile na wale wanaofanya kazi migodini, mimi najua hawa wanaofanya kazi migodini wengi mwisho wa siku baada ya muda wanaathirika. Kwa hiyo Serikali ifanyie utafiti kwa watu wanaofanya migodini, ili wasije wakafika mahali sasa hata maisha yao yakaathirika na wakashindwa kufanya kazi zingine baadae baada ya kufanya kazi kwa muda fulani mgodini, baadae wanaathirika kiafya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema mambo hayo, niombe tu Serikali iendelee kuwekeza zaidi na napenda kushukuru naunga mkono hoja, nikiamini kwamba Serikali inaenda kufanyia kazi.