Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kwa kunipatia fursa hii. Pia naomba kipekee kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai.

Mheshimiwa Spika, ninampongeza pia Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya yeye pamoja na wasaidizi wake wote akiwemo Waziri Mkuu, Naibu Waziri Mkuu na Viongozi wote wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pongezi hizo zinaambatana na ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Bwawa lile ni kubwa, lakini linataka kututoa Watanzania hapa tulipo, kutupeleka katika hatua nyingine zaidi ya kiuchumi. Ni bwawa kubwa ambalo kama tutalitumia vizuri, manufaa yake tutayaona na tumeanza kuyaona kwa sababu umeme umeshaanza kuzalishwa. Shukurani kwa Viongozi wa Chama na Serikali ambao mmesimamia bwawa lile.

Mheshimiwa Spika, ni rai yangu kwa Watanzania wote kuendelea kutunza miundombinu ile hasa wale ambao wanatoka maeneo jirani yenye mito inayoingiza maji kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, tuendelee kutunza vyanzo vyetu ili mradi wetu uwe endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue pia fursa hii kumshukuru Naibu Waziri Mkuu pamoja na Naibu Waziri wa Wizara ya Nishati, kwa jitihada kubwa ambazo wamezifanya katika sekta hii ya nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Newala Vijijini kwa mfano, tunavyo vijiji 107, lakini wakati naingia ni vijiji 31 tu ndivyo ambavyo vilikuwa na umeme. Leo ninapoongea, vijiji 35 tayari vimeshawashwa umeme, vijiji 13 vimeshawekewa transformer bado kupimwa umeme uwashwe, vijiji 25 vinaendelea na kazi katika hatua mbalimbali. Ni vijiji vitatu tu ndiyo ambavyo bado na ninaamini kwa jitihada na namna ambavyo Waziri na timu yake wanafanya kazi, basi vijiji hivi navyo vitafikiwa kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na shukrani hizi, katika mradi huu wa REA naomba, hivi vijiji ambavyo nimezungumzia ni vile ambavyo vimefikiwa na kilometa moja tu ya ujenzi wa umeme. Kwa hiyo, maeneo mengi ya taasisi kwa mfano, shule, zahanati, nyumba za ibada, zote bado hazijafikiwa na mradi huu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa lengo ni kumfikishia mwananchi huduma na kumpunguzia mzigo, naiomba Serikali, zile kilometa mbili ambazo zinaenda kujengwa katika kila kijiji, basi tusimamie zijengwe kwa haraka ili taasisi nilizozitaja zipate umeme na wananchi waweze kuhudumiwa ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, leo hii unaenda kwenye zahanati ambayo imejengwa vizuri, kwa mfano kule Newala Vijijini kuna zahanati ya Namangudu, zahanati nzuri kabisa ya kisasa haina umeme. Sasa mama anaenda kujifungua, anamulikiwa kwa mwanga wa simu, hapana! Siyo sawasawa, kwa sababu Serikali inasema kuongeza kilomita mbili itakuwa ni jambo la haraka. Naomba tumsimamie mkandarasi aliyepewa kazi ili kazi hii ikakamilike haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ipo changamoto nyingine ya kukatikakatika kwa umeme hasa Mkoa wa Mtwara. Naomba sana, najua Serikali inafanya jitihada kubwa, imeshaleta mtambo wa megawati 20, tumeona umeme upo, ila shida ni miundombinu. Ninaiomba Serikali isimamie miundombinu ili umeme ule usikatikekatike sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, najua zipo jitihada nyingine nyingi tu. Kwa mfano, wameshafunga baadhi ya maeneo auto recloser ili kupunguza umbali wa kusafirisha umeme. Naomba tuisimamie kwa haraka ili umeme usikatike maeneo mengi kwa wakati mmoja. Najua ni gharama, lakini inawezekana kwa sababu tumeshaamua, basi tufanye hima umeme uwafikie wananchi, na tupunguze hii adha ya kukatikakatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba long term plan iwe ni kuufikishia Mkoa wa Mtwara na Lindi umeme kutoka gridi ya Taifa. Mpaka sasa umeme haujafika Gridi ya Taifa. Tunajua Serikali inayo mikakati ya dhati ya kufikisha umeme, lakini naomba usimamizi wa haraka zaidi na tupeleke pesa ili tupate Gridi ya Taifa kwa Mkoa wa Mtwara kutokea kule Songea kama ambavyo mmetuahidi na wananchi wetu wa Mtwara - Newala waweze kufanya uwekezaji mkubwa sasa. Wengi wanashindwa kuwekeza katika maeneo yetu kwa sababu ya ukosefu wa umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukienda Newala unakutana na viwanda vya korosho vimekaa tu kama maghala ya kutunzia bidhaa, lakini inawezekana sababu mojawapo ya wale wawekezaji kushindwa kuendelea kubangua korosho ni kukatikakatika kwa umeme. Kwa hiyo, naiomba Serikali isimamie tupate umeme kutoka gridi ya Taifa ili uwekezaji Mkoa wa Mtwara ukawe wa uhakika na kuinua kipato cha wananchi wake. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii, naunga mkono hoja. (Makofi)