Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambayo ameendelea kuipa fedha Wizara ya Kilimo ili kuongeza uzalishaji katika mazao mbalimbali yakiwemo ya chakula na biashara, lakini pia niwapongeze pia viongozi wa Wizara ya Kilimo kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuisimamia Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kuhusu zao la korosho kwa upande wa viatilifu; tunaishukuru Serikali kwa kuendelea kutupatia pembejeo bure kwa wakulima wetu. Naomba Serikali isimamie ubora wa pembejeo zinazopelekwa kwa wakulima wetu. Zipo dosari chache za kiutendaji kutoka kwa wasambazaji wetu, kufuatia ripoti ya Tume iliyoundwa kuchunguza mwenendo mzima wa zao la korosho, yapo maelezo ya dawa isiyostahili kwenye zao la korosho ambayo msimu uliopita walipewa wakulima. Sumu ambayo ni kwa ajili ya maua ya rose na mbogamboga wamepewa wakulima wa korosho. Matokeo ya dawa za namna hii ni kuharibu mimea na kuathiri uzalishaji. Tunaomba dawa ile kwa mamlaka yenu wakulima waarifiwe wasiitumie na zoezi hili lifanyike mapema kwa kuwa huu ndio msimu wa maandalizi ya mashamba.

Mheshimiwa Spika, kuhusu waatalam wetu tulionao site (Maafisa Ugani) wapewe mafunzo ili nao wajue namna ya kutumia viatilifu vinavyoletwa kwenye maeneo yao. Wengi hawajui, hali inayowafanya wakulima kulima kwa mazoea. Rejea maelezo ya taarifa ya Ripoti ya Tume iliyoundwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mfumo wa TMX niiombe Serikali isimamie vizuri mfumo huu ili ulete tija kwa wakulima. Tusiruhusu watu wenye maslahi binafsi kuuingilia mfumo huu, isije wakaja wale wanunuzi wahuni waliokuwa wanajimilikisha makampuni zaidi ya kumi kwenye mtindo wa kulaza sanduku wakijifanya ni watu tofauti kumbe ni mnunuzi mmoja yule yule ndiye anajifanya makampuni kumi. Tuwe makini tusije tukaharibiwa na wajanja wachache.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mjengeko wa bei ya korosho, naiomba Serikali ijitahidi kututafutia masoko ya uhakika ya kununua mazao yetu. Aidha, suala la tozo katika bei ya korosho liangaliwe upya kwa sababu tozo nyingi zinaathiri malipo ya mkulima moja kwa moja. Mfano tunaposema shilingi 110 ya gunia analipia mnunuzi, sio sahihi kwa sababu mwisho wa siku kimsingi anayelipia ni mkulima.

Mheshimiwa Spika, kuhusu uhakiki wa idadi ya miche ya mikorosho kwa wakulima; zoezi limegubikwa na sintofahamu nyingi. Wengi hawajakwenda mashambani wamekadiria tu, matokeo yake ni kutotosheleza kwa pembejeo tunayowapatia.

Mheshimiwa Spika, hitimisho, naunga mkono hoja.