Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri. Pia nawapongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, Kamati na viongozi mbalimbali na watumishi wa Wizara kwa maandalizi mazuri ya bajeti. Naipongeza Serikali kwa kuwa na mradi huu adhimu wa umeme vijijini. Faida nyingi zimepatikana na uchumi wetu umeboreshwa na mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika REA II, Jimbo la Bagamoyo lilipata miradi 10 tu na miradi hii ilitegemewa kukamilishwa Juni 2015. Ingawa miradi hiyo ni michache lakini utekelezaji wake umesuasua sana na uko nyuma ya ratiba, hadi leo miradi minne (4) kati ya hiyo 10 haijakamilika kama ifuatavyo:-
(i) Kijiji cha Buma, nyaya hazijafungwa katika nguzo;
(ii) Kijiji cha Kongo, hivi karibuni tu ndiyo nyaya zimepelekwa;
(iii) Kijiji cha Kondo, mradi haujaanza;
(iv) Kijiji cha Matimbwa, nguzo 20 hazijafungwa nyaya. Zahanati mpya ya Kijiji ilijengwa kwa ufadhili wa NGO ya Korea ipo katika eneo hili ambalo halijafikiwa na umeme; na
(v) Kijiji cha Pande, mradi umehamishwa kwa sababu wananchi wanapisha ujenzi wa bandari.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Waziri atuthibitishie kuwa miradi hii itapewa kipaumbele kumalizika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu REA III, katika Jimbo la Bagamoyo tumewasilisha miradi 29 tu. Ni matumaini yetu kuwa utekelezaji REA III Bagamoyo utakuwa bora zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo linaathiri maendeleo ya uchumi na ya kijamii kwa wana Bagamoyo ni kukatika kwa umeme mara nyingi Bagamoyo Mjini na katika Kata za Magomeni na Dunda. Serikali isimamie upatikanaji wa umeme kwa uhakika zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ugunduzi wa gesi asilia Bagamoyo na Chalinze, tumeshuhudia utafutaji ukifanywa na fununu za kupatikana gesi Bagamoyo na Chalinze. Tatizo ni kuwa hakuna taarifa za kugundulika gesi katika majimbo tajwa. Waziri atujulishe kama kweli gesi imegunduliwa Bagamoyo na Chalinze.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.