Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hotuba ya Waziri wa Nishati na Madini kama ilivyowasilishwa leo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Madini nchini bado haijaeleweka hasa kwa wananchi wengi wa vijijini, jambo linalowafanya wananchi wengi kunyanyasika hasa pale ardhi yao inapogundulika kuna madini na wao kutakiwa kuhama pengine bila ya hata kujua stahiki zao, zaidi ya kuambulia mashimo. Sambamba na hilo, hata utaratibu wa upatikanaji wa leseni kwa wachimbaji wadogo, hauko wazi hasa kwa watu waishio vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Liwale katika Kijiji cha Lilombe kuna machimbo ya madini ya dhahabu na sapphire, lakini wachimbaji wadogo wanapotaka leseni, hulazimika kwenda Tunduru Mkoani Ruvuma ambako ndiko kuna Ofisi ya Kanda.
Vile vile soko la madini wanayoyapata hulazimika kwenda kuyauzia Tunduru, hivyo Halmashauri ya Liwale haina mapato yoyote yatokanayo na machimbo hayo. Maeneo ya machimbo hayo ni ardhi inayomilikiwa na Kijiji cha Lilombe, lakini inapotolewa leseni wananchi hawa hawashirikishwi katika lolote. Hivyo kuweka mgogoro kati ya wachimbaji hao na Halmashauri ya Kijiji. Nini kauli ya Serikali juu ya mgogoro huu? Kwa nini kusifunguliwe Ofisi ya Madini Liwale? Kwa nini wachimbaji wasilipe ushuru kijijini ili kijiji kipate mapato yatokanayo na ardhi yao badala ya kuachiwa mashimo na mapato yaende mkoa mwingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Liwale iko kilometa 120 toka Wilaya ya Nachingwea ambako kuna umeme wa gesi asilia, lakini kwa masikitiko makubwa hadi leo Liwale inategemea umeme wa mafuta (generator) ambao kutokana na ukosefu wa barabara kuna wakati Liwale hubaki gizani kutokana na kukosa mafuta. Vile vile generator hilo kwa sasa limezidiwa na watumiaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi huu wa REA kwa Wilaya ya Liwale ni wa kusuasua sana hasa baada ya kukosekana kwa umeme wa uhakika. Wilaya yenye vijiji 76 ni vijiji vitano tu vyenye umeme wa REA. Njia kuu ya umeme kutoka Nachingwea hadi Liwale ujenzi wake haujapewa msukumo unaostahili. Kumekuwepo na visingizio vingi, haijulikani kikwazo ni nini na nani kati ya Mkandarasi, TANESCO au Serikali. Namwomba Waziri mwenye dhamana kuhakikisha mradi huu unakamilika ili kusukuma maendeleo ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa kiwanda cha kuchakata gesi (LNG – LINDI) ni bora ukaharakishwa sambamba na kulipa fidia kwa wale waathirika wa ujenzi huo. Vile vile ni jambo la kuzingatia kuwa vijiji vyote vinavyopitiwa na bomba hili la gesi ni lazima vipatiwe umeme sambamba na kuwalipa fidia watu wote ambako bomba hili limepita. Hakuna dhambi kubwa itakayofanywa na Serikali hii kama mtawanyima umeme wanavijiji Mikoa ya Lindi na Mtwara. Naomba kuwasilisha.