Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru, ila nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Profesa Sospeter Muhongo pamoja na timu yake kwa kazi nzuri na uwajibikaji uliotukuka katika kuwatumikia wananchi wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nijielekeze kuchangia katika Usambazaji wa Umeme Vijijini (REA) katika hotuba iliyokuwepo mbele yetu. Nchi yetu ina malengo ya kuwa nchi ya viwanda na kufikia katika azma ya uchumi wa kati. Pamoja na jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali, lakini ukweli ni kwamba, tuna changamoto kubwa ya vikwazo vya uchumi kimojawapo ni kukosekana kwa nishati ya uhakika ya umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia kubwa ya wananchi wetu wanaoishi vijijini wanakosa huduma hii muhimu ya nishati ya umeme ambao ni kichocheo kikubwa cha maendeleo ya watu wetu. Niiombe Serikali iongeze kasi ya usambazaji na kuiongezea fedha za kutosha Wizara ya Nishati kuhakikisha inasambaza umeme kwenye vijiji vingi na kwa wakati muafaka pia, kukamilisha miradi ya umeme ambayo haijakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukisambaza umeme vijijini tutawezesha wakulima kuongeza thamani ya mazao kwa kufungua viwanda vidogo vidogo, tukisambaza umeme vijijini wavuvi watahifadhi samaki; pia, itawawezesha wafugaji kuhifadhi nyama kwa muda mrefu, sambamba na kuongeza ajira kwa vijana kwa kuanzisha shughuli mbalimbali za kijasiriamali; mfano saluni za kike na za kiume, uuzaji wa vinywaji baridi, viwanda vya kuchomea vyuma na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nitumie nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri katika bajeti hii ahakikishe vijiji vifuatavyo katika Jimbo la Pangani vinapatiwa umeme huu wa REA; Kigurusimba Misufini, Mivumoni, Matakani, Kidutani, Jaira, Kikokwe, Langoni, Mtango, Mtonga.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia, tunaomba Wizara iwe na mkakati maalum wa kuunganisha umeme katika shule za sekondari za kata, zahanati na vituo vya afya, ili kuimarisha huduma za jamii za wananchi wetu.