Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia jioni ya leo na mchango wangu nianze kwa kuleta shukrani za Wanahanang kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo imefanyika kwenye sekta ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani hizi zikimfikia Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, moja kwa moja ziende kwa Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati Mheshimiwa Judith Kapinga na wataalamu wote wa Wizara ya Nishati, kwani kwa kipindi kifupi Wilaya ya Hanang imepata umeme kwenye vijiji 46, tumepata umeme kwenye vitongoji 49 na pia tunaendelea na mchakato wa vitongoji 15 na Mheshimiwa Waziri nimemwona, amenieleza kwamba tutapata pia kwenye vitongoji 81. Kwa jumla, tutapata vitongoji 305 kuunganishiwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia TANESCO wameendelea kupeleka umeme kwa wananchi, kwenye maeneo ambayo yalikuwa yamepata umeme kabla na hii niliiomba kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 mahususi eneo la Kateshi ambalo lilipata umeme muda mrefu, eneo la Giting, Nangwa, Miaskoni, Jorodom, Ganana, Gendabi maeneo haya umeme umeongezwa kwa maana ya kujazilisha yale maeneo ambayo yalipata umeme siku nyingi. Nashukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Hanang. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine napongeza kazi kubwa inayofanywa na Wizara, pia kwa uwekezaji ambao Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ameruhusu fedha nyingi ziende kwenye sekta ya nishati hasa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi hizi ukiangalia taarifa tuliyonayo au taarifa tuliyopewa hapa Bungeni Machi, 2024 uwezo wetu wa kuzalisha mitambo yote ilikuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 2,138 lakini taarifa ya Februari mwaka huu tulikuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 3,796.7.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Waziri ametoa Taarifa hapa Bungeni kwamba uwezo wetu wa uzalishaji umepanda mpaka kufikia megawati 4,031.71. Hii ni hatua kubwa sana kwenye uzalishaji wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza sana kazi kubwa inayofanyika. Pamoja na pongezi hizi, nafahamu tunao umeme mwingi na chenji sasa hivi tunayo kwenye uzalishaji. Umeme huu unatakiwa uwafikie wananchi, na ili uwafikie wananchi, lazima tuendelee kuwekeza kwenye usafirishaji wa umeme, kwenye usambazaji wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu umeme huu tukipeleka kwenye vitongoji, pamoja na kwamba tumesogea sana, tukipeleka kwenye viwanda, migodi, huduma nyingine za jamii ndani ya muda mfupi utakuwa mdogo. Kwa hiyo, tuendelee kuwekeza kwenye uzalishaji wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu ya Hanang pamoja na kwamba tumeshafika vitongoji 305, bado vitongoji 101. Pia kwa sasa Wilaya ya Hanang nafikiri kama siyo namba moja kwa kukatika kwa umeme Tanzania labda itakuwa namba mbili. Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati nimeomba mara nyingi kujengewa kituo cha kupooza umeme, pale Wilaya ya Hanang ili kuondoa adha ya umeme kukatika mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliahidiwa kujengewa kwenye mwaka wa fedha 2022/2023 mpaka sasa Wanahanang wanasubiri adha ya umeme ni kubwa. Jumamosi hii nilikuwa wilayani kwenye Kata za Magharibi, siku tatu hawakuwa na umeme kwa sababu kulikuwa na hitilafu. Changamoto kubwa tuliyonayo, line ndefu sana, ukiwa na kituo cha kupooza umeme, pakiwa na hitilafu sehemu moja, sehemu nyingine zinaendelea kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni hitaji la wananchi wa Hanang. Tunaomba mtusaidie, tukipata umeme wa uhakika ambao haukatikikatiki Hanang tutawekeza kwenye ujenzi wa kiwanda cha simenti, tutawekeza kwenye kiwanda cha kuchakata chumvi kwa sababu tuna akiba ya chumvi pale Ziwa Gendabi, tutawekeza kwenye viwanda vya kuchakata mazao, na baada ya hapo tutatengeza ajira kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akina mama na Watanzania wa Hanang watapata ajira ya uhakika, na hili ni hitaji namba moja, hitaji kubwa la wananchi wa Hanang. Ninachoomba, kwenye bajeti hii ya mwaka 2025/2026 shilingi bilioni 250, sehemu yake iende Hangang ikajenge kituo cha kupooza umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Meneja wangu wa Wilaya anafanya kazi nzuri sana na timu yake, lakini wanayo changamoto ya usafiri. Nimeshaongea na Katibu Mkuu, aliniahidi, naomba gari iende angalau tuwasaidie wale vijana wafanye kazi yao vizuri kwa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka kuchangia ni eneo la nishati safi ya kupikia ambapo Mheshimiwa Dkt. Kikoyo pia amechangia. Kwa sasa hamasa kubwa tunayoifanya ni kuhakikisha ile mitungi ya gesi tunawafikishia wanachi wengi. Gesi tunayopeleka ni LPG ambayo haipatikani hapa nchini, bali tunaiagiza kutoka nje ya nchi. Hamasa inayofanyika ni nzuri sana ya kuhakikisha tunatumia nishati safi ya kupikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba kwenye eneo hili, tutafute namna ya kutumia teknolojia zinazopatikana nchini. Kwa mfano, hayo majiko banifu tunayoyasema au tutafute majiko ambayo yanatumia umeme kidogo, umeme ambao tunazalisha kwa rasilimali ambayo iko hapa nchini kama vile maji, gesi, upepo, na jua, itasaidia nchi yetu kujitegemea na kuepuka kupeleka fedha nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuangalie teknolojia kama biogas ili angalau sasa nishati safi tutakayoipata iwe inapatikana hapa nchini badala ya kuwa wategemezi kuagiza sehemu kubwa ya nishati kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitamani niliongelee ni eneo la makaa ya mawe. Imekuwa ni wimbo wa muda mrefu, yale makaa ya mawe hatujayatumia kuzalisha umeme. Ombi langu kwenye eneo hili, kwa kuwa ule mgodi wa makaa ya mawe uko chini ya STAMICO ambayo ipo Wizara ya Madini, lakini anayehitaji umeme ili tuzalishe kwa kutumia makaa ya mawe ni TANESCO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni Wizara mbili tofauti. Yawezekana kuna ukinzani kwa sababu ya utendaji kazi ndani ya Serikali. Kwa makusudi kabisa Serikali iamue namna ambavyo tunaweza kutumia yale makaa ili hatimaye tuweze kupata manufaa kwayo kwa sababu baada ya muda, dunia inakoenda ni nishati safi, yale makaa ya mawe yanaweza yasitumike na tutakuwa tumepoteza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni mradi wa muda mrefu ambao tumeuongelea wa gesi asilia kwa maana ya kuisindika ili iwe LNG. Mradi huu tumeusema miaka mingi na ninaamini kwamba tungeanza kutekeleza, ungetusaidia kwa kiasi kikubwa kwenye eneo la nishati kwa sababu sehemu kubwa ya magari yetu yote yanatumia mafuta ambayo tunaagiza nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tumeanza kidogo kwenye CNG. Tukianza kuwekeza kwenye LNG tunaweza kusafirisha gesi ambayo tunayo kwa urahisi ikawafikia wananchi wakapikia, tukayatumia kwenye magari na hatimaye tukapunguza utegemezi wa nishati nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka niseme, ukienda kwenye suala la kuwapelekea wananchi wetu umeme, Kamati ambayo na mimi ni mjumbe, tumelisema kwa sauti kubwa. Chini ya mita 30 wananchi wanaunganishiwa kwa shilingi 27,000, ambapo bei hii imepangwa na EWURA. Ikifika mita 70 wananchi wanaungiwa kwa shilingi 515,617 na chenji, lakini ikifika mita 120 inakaribia shilingi 700,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hao wanaopelekewa ni hao hao maskini wa Tanzania. Hizi gharama ni kubwa, TANESCO na Wizara waangalie namna bora ya kupunguza gharama kwa sababu ni kweli miundombinu ile ikiwekwa ni mali ya TANESCO, siyo mali ya mwananchi anayepelekewa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa uwekezaji ule ni mali yao, waone namna ambavyo wanaweza waka-recover taratibu kutoka kwa wananchi wanaounga umeme ili hatimaye wananchi wapate umeme wa uhakika kwa gharama nafuu baada ya kuwaunganishia. Inawezekana tuka-recover zile fedha kwa kupitia bills za umeme ambazo wananchi wanalipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)