Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara ya Ardhi, kwa sababu mimi pia ni miongoni mwa wananchi ambao wanaguswa na migogoro ya ardhi nikitokea katika jamii yangu ya Wamasai. Kwa hiyo, moja kwa moja naomba nigusie baadhi ya maeneo ambayo kwa namna moja au nyingine yamechangiwa na migogoro hii, hasa kutokana na kwamba Serikali ama viongozi husika kutokuvalia njuga migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya mambo ambayo kwa namna moja au nyingine yamechangia sana migogoro baina ya wafugaji na wakulima ni Sheria ya Utambuzi wa Mifugo ya mwaka 2010 ambayo inashindwa kutambua wafugaji wa asili na hasa katika maeneo yao husika. Pia Sera ya Wanyamapori ya mwaka 1998 na yenyewe pia imekuwa ikizuia mifugo katika maeneo ya wanyamapori ilhali maeneo hayo siku za nyuma yalikuwa ni wazi kabisa kwa ajili ya wafugaji na wafugaji hawa walikuwa hawabugudhiwi na kitu chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine pia ni hizi sheria ambazo ni nyingi, mfano Sheria ya Mazingira ya mwaka 2007 na yenyewe pia kwa sababu inaainisha kuwa ufugaji wa asili ni moja ya vyanzo vya uharibifu wa mazingira, hii pia imechangia kuwepo kwa migogoro baina ya wafugaji na wakulima. Maeneo mengi yaliyokuwa yakitumika na kutambuliwa na wafugaji, nakumbuka tangu nikiwa mdogo maeneo hayo wafugaji walikuwa wakiyatumia na wafugaji hawa wamekuwa wakilisha mifugo yao na kumekuwepo na amani baina ya wafugaji na wakulima, hakukuwepo na migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sababu sheria hii sasa haiwatambui wafugaji na haithamini ile mifugo yao na kuona kwamba mifugo hii ya asili ni chanzo cha uharibifu wa mazingira, sheria hizi zimekuwa zikichangia migogoro hiyo na kwa sababu haitambui imekuwa ni chanzo cha uharibifu huu au migogoro hii baina ya wakulima na wafugaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba yapo maeneo mengi ambayo yametengwa, migogoro hii pia inachangiwa na baadhi ya viongozi, viongozi wa Kiserikali, viongozi wa kisiasa, viongozo wa kimila, viongozi wa kidini, wote hawa wamekuwa wakichangia migogoro hii. Kwa mfano, katika Ranchi ya Manyara ambayo hata wakati huo akiwa Rais wa Awamu ya Tatu Mheshimiwa Benjamini Mkapa, eneo hili la Ranchi ya Manyara lilitamkwa wazi kwamba litumike kwa ajili ya mifugo, lakini mpaka leo hii baadhi ya viongozi wa kisiasa wamekuwa wakilitumia hili eneo na kuwanyima hata wafugaji ambao na wenyewe wanatoka katika jamii hiyo, kuwazuia kulisha mifugo yao na hata wakati mwingine maeneo haya ambayo mifugo inatakiwa ipite na kwenda kunywa maji imekuwa ni shida pia. Hili ni eneo la Ranchi ya Manyara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine wanasema kwamba kabla ya kutoa kibanzi kwenye jicho la mwenzako, ni vema basi ukatoa boriti kwenye jicho lako. Ijumaa, miongoni mwa walichangia hapa na hasa nizungumzie eneo la Monduli ambako mwaka jana nilipata bahati ya kuzunguka katika Kata zote katika Uchaguzi Mkuu, yapo baadhi ya maeneo ambayo baadhi ya viongozi wenyewe kama nilivyosema wamechangia, lakini pia hata viongozi wengine hao ambao tunaowatarajia na …
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, na tunapokuja huku tukitarajia kwamba wao ndio faraja kuweza kuishauri Serikali ndiyo wamekuwa hao wanaochangia migogoro. Mfano katika Milima ya Nanja, mmoja wa viongozi ambao wakati huo alikuwa ni Diwani wa CCM na kwa hivi sasa yuko upande wa pili, ameuza eneo hili la Mlima Nanja na hivi sasa eneo hilo linatumika kwa uchimbaji wa kokoto na eneo hili limeuzwa pasipo ridhaa ya wananchi wenyewe. Kwa hiyo, wakati mwingine tunapozungumzia kuhusiana na hii migogoro, ni vema na pia tukajiangalia, je, tumechangia kwa kiasi gani, tumetatua migogoro kwa kiasi gani ili basi tuweze kuwanyooshea vidole wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi katika Wilaya ya Monduli na hasa nimpongeze Mheshimiwa Waziri mwenye mamlaka husika kwa jitihada zake, ambapo Februari na Machi mwaka huu, aliweza kufika Wilayani Monduli katika ziara yake na kufuta baadhi ya vibali 13 vya mashamba ambayo yalikuwa yametelekezwa na mashamba hayo kugawiwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaona kwamba pamoja na kwamba jitihada hizi zipo, lakini bado tuiombe Serikali yenyewe ili iweze kushughulikia migogoro hii ambayo imekuwa ikichangiwa kwa kiasi kikubwa na viongozi hao kama nilivyosema, baadhi yao viongozi wa Kiserikali, vile vile viongozi wa kisiasa ambao wamehodhi maeneo makubwa na matokeo yake wananchi wanapata shida ya kuweza kumiliki ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika Wilaya ya Arumeru ambako hasa ndiko huko ninakotoka, yapo mashamba makubwa na hayo mashamba, mfano shamba la Gomba Estate na kwa bahati nzuri katika moja ya nakala tulizopewa na Mheshimiwa Waziri yameorodheshwa. Mashamba haya tangu tunakua yamehodhiwa na ukienda hata kwa hivi sasa mashamba haya hayatumiki, wananchi wa kule hawana maeneo wakati mwingine ya kulima na hata juzi tu wananchi moja ya mashamba ambayo yapo katika maeneo hayo ya Malalua, maeneo ya Gomba walijikatia baadhi ya maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vema kama hawa wafanyabiashara au hawa ambao wamehodhi maeneo haya hawawezi kuyamiliki, nafikiri ni vema kabisa huu utaratibu ukaendelea kuhakikisha kwamba wananchi wanapewa mashamba haya ili waweze kulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mashamba haya na hasa ukizingatia mfano kwa Mji wa Arusha ambao kila siku umekuwa ukipanuka. Mji huu na maeneo mengi sasa yamekuwa ni maeneo ambayo wananchi wengi nao wanazidi kuvamia na bado yamehodhiwa na hawa watu ambao hawaitendei haki Serikali. Mheshimiwa Waziri kwa dhamana aliyonayo kama alivyofanya katika Wilaya ya Monduli namwomba pia afike katika maeneo ya Vijiji vya Mlangarini afike katika maeneo ya vijiji, Kata ya Manyire ili aweze kufuta baadhi ya vibali hivi ambavyo vinawakosesha wananchi wetu haki ya kumiliki ardhi, vilevile inawakosesha wananchi wetu kupata maeneo kwa ajili ya kulisha mifugo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda katika Jiji la Dar es Salaam, katika Jiji hili la Dar es Salaam na hasa tukikumbuka mvua za mwaka 2011/2012 ambazo zilileta maafa kwa kiasi kikubwa, Serikali kwa wakati ule iliwatafutia eneo la Mabwepande na wananchi wakaweza kupewa viwanja ingawa bado wako wengine ambao wamerudi tena katika bonde la Msimbazi, wamerudi katika mabonde ya Mkwajuni, tuangalie kwamba sheria hizi wapo kweli ambao wameshalipwa, lakini wapo kweli ambao miaka nenda miaka rudi wapo maeneo hayo. Tuangalie ni kwa jinsi gani Serikali inaweza kuwasaidia ili kuepusha migogoro hii ambayo kwa namna nyingine imekuwa ikikosesha amani wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema kwamba tunafahamu umuhimu wa ardhi, kila mmoja wetu anatambua thamani ya ardhi na ardhi imekuwa ikipanda thamani kila leo. Ili kuepusha migogoro hii ya ardhi, tusiwasubiri wananchi mpaka wanajenga, wanamaliza kujenga halafu bado wanapelekewa huduma zote muhimu, utakuta umeme wamepelekewa ,matokeo yake baadaye wanakuja kubomolewa. Hii inakuwa ni kero kwa wananchi na wananchi wanakosa imani na Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba tu Mheshimiwa Waziri na kwa sababu ameingia katika Wizara hii na ameanza vizuri, hebu naomba arekebishe pia hata hao watendaji ambao kwa namna moja au nyingine wamekuwa wakisababisha migogoro hii ya ardhi kwa kutoa vibali maeneo ambayo siyo halali kujenga, matokeo yake pia wananchi wamekuwa wakijenga na baadaye wanakuja kuwabomolea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na nimwombe tu Mheshimiwa Waziri kwamba, kwanza nimtie moyo kwa kazi nzuri anayoifanya na aendelee kufuta mashamba haya ambayo yamekuwa ni kero na hasa ukizingatia kule Bwawani pia kule Lucy mashamba haya yapo namwomba afike pia katika Kata ya Nduruma ufike pia huko Lucy ufute hivi vibali ili wananchi waweze kumiliki ardhi hii. Ahsante sana.