Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia hotuba hii kwa kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Waziri kwa mikakati yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kawaida ya Serikali yetu tatizo kubwa linaanzia pale ambapo Serikali inaposhindwa kutoa fedha zilizotengwa katika bajeti hii. Wizara ya Ardhi kwangu mimi ni kama Wizara mtambuka kwani migogoro mingi husababishwa na maingiliano ya sera kama vile sera ya kilimo, sera ya mifugo, sera ya madini na kadhalika ambazo zote zinaihusu ardhi lakini ni nani anasimamia sera ya ardhi kwa upana wake?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ardhi na umaskini wa watu wetu. Watanzania wengi hasa wa vijijini wanakuwa maskini kutokana na kushindwa kwa Serikali kuwamilikisha ardhi. Hivyo watu hawa hushindwa kuaminika na taasisi za kifedha, hawakopesheki na pale mwananchi anapoomba kupimiwa ardhi yake ili aweze kuwa na hati miliki gharama huwa ni kubwa sana na kuwa na milolongo mingi inayosababishwa na rushwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wengi wanashindwa kuwekeza vijijini kwani kikwazo kikubwa ni vijiji vingi kutokuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi. Kijiji ambacho hakijapimwa kwa matumizi bora ya ardhi kinakosa wawekezaji eti kwa kuwa kijiji husika hakijaingia kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi. Mfano ni jimboni kwangu Liwale wawekezaji wengi wameshindwa kusajili biashara zao kwa kuwa vijiji walivyowekeza havijapimwa kwa hiyo hao wawekezaji kukosa leseni za biashara zao. Yuko mwekezaji ameshindwa kusajili shule kwa kukosa hati miliki ya ardhi kutokana na kijiji kukosa matumizi bora ya ardhi. Vilevile kuna mwekezaji ameshindwa kusajili zahanati kwa kuwa kijiji hakijaingia kwenye matumizi bora ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba mkubwa wa watumishi wa kada hii kunafanya gharama ya kupima ardhi na viwanja kuwa ghali sana. Mfano Mji wa Liwale hulazimika kukodi wapimaji toka Wilaya jirani ya Nachingwea hivyo kufanya bei ya viwanja kuwa juu sana na watu kuendelea kukaa maeneo yasiyopimwa. Namuomba Waziri atuongezee watumishi ili kuhakikisha upimaji wa ardhi Jimboni Liwale unafanyika ili kuharakisha maendeleo ya Halmashauri yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro wa ardhi. Wilaya ya Liwale ina mgogoro wa muda mrefu kati ya wanakijiji cha Kikulyungu na Hifadhi ya Mbuga ya Selous. Mgogoro huu umeshaleta maafa tayari watu wanne (4) wamepoteza maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upimaji wa vijiji; Serikali iharakishe upimaji wa vijiji ili wawekezaji wanapokwenda vijijini wakute kijiji tayari kimeshafanya mpango wa matumizi bora ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.