Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. WILLIAM T. OLENASHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kumpongeza Waziri wa Ardhi, Naibu Waziri pamoja na watumishi wa Wizara ya Ardhi kwa kutayarisha hotuba nzuri iliyosheheni mikakati mizuri ya kuondoa changamoto ya sekta ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutumia fursa kutoa changamoto kadhaa za ardhi kwenye Jimbo la Ngorongoro ambayo ningeomba Wizara ya Ardhi iangazie mwanga ili kutafuta suluhu ya kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya vijiji na vijiji. Ngorongoro kuna migogoro mingi ya ardhi inayohusu mipaka. Kutokana na kukosekana mipaka ya kisheria kati ya kijiji kimoja na kingine migogoro hii mara nyingine imesababisha mauaji na uharibifu wa mali. Mifano ya migogoro ni kama ile kati ya vijiji vya Naar na Kisangiro Maaloni na Yasi Ndito, Sale na Malambo, Ngarwa na Oloipiri na Kirtalo Oldoinyosamba na Pinyin na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuwasihi wenzetu wa Wizara ya Ardhi washirikiane na Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ili kupima mipaka ya vijiji. Ili kuondoa migogoro isiyokuwa ya lazima na kuokoa maisha na mali za wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro kati ya hifadhi na vijiji. Wilaya ya Ngorongoro ina mgogoro mkubwa kati ya vijiji na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti (Serengeti National Park). Vijiji hivyo ni pamoja na Ololosokwari, Kiitalo, Oloipiri, Oloiriori, Lopulun, Loosoitik, Arrash, Piyaya na kadhalika. Kukosekana kwa mpaka unaoeleweka kwa alama kunaleta mgogoro mkubwa sana kwani mara nyingi wananchi wanakamatwa na kutozwa fine kwenye eneo ambalo wao wanafahamu kuwa ni eneo la vijiji toka siku nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutoa rai kwa Wizara ya Ardhi kwa kushirikiana Wizara ya Maliasili na TAMISEMI kupima na kuweka bayana mipaka ya hifadhi ili kuondoa migogoro isiyokuwa na maana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro kati ya vijiji na wawekezaji. Migogoro mingine ambayo ningependa Wizara ya Ardhi iitazame na kutatua kwa kushirikiana na wadau wengine ili ipatikane suluhu ya kudumu ni migogoro kati ya kampuni ya uwindaji ya Orthelo Business Cooperation (OBC) na vijiji vilivyopo ndani ya Pori Tengefu la Loliondo (Loliondo Game Controlled Area). Migogoro hiyo ni dhahiri kuwa inasababishwa na mgongano wa Sheria za Ardhi (Na. 4 na 5 za mwaka 1999) na Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009, ambazo zinatoa ardhi kwa vijiji na hapo hapo kuweka mamlaka ya rasilimali za wanyamapori chini ya mamlaka nyingine na hivyo kuleta mgongano wa matumizi ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa Wizara ya Ardhi ishirikiane na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kutengua na kufuta mapori tengefu yaliyopo ndani ya ardhi ya vijiji vya Loliondo ili wananchi waweze kupata mamlaka kamili ya kusimamia ardhi zao kama vijiji vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro mwingine kati ya vijiji na wawekezaji ni kati ya vijiji na wawekezaji, ni ule kati ya kampuni ya kitalii ya Thompson Safaris na vijiji vya Sukenya, Mundorosi, mgogoro ambao umezuka baada ya TBL Ltd. kuuza ardhi ya shamba la Sukenya ambalo kwa miaka mingi lilitelekezwa na wananchi kulitumia zaidi ya miaka 20. Aidha, wananchi wamefungua kesi mahakamani ya kupinga shamba hilo kuuzwa kwa kile wanachosema kuwa wameporwa na TBL bila kufuata taratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro kati ya Wilaya/Mkoa. Ningependa vilevile kati ya mipaka ya Wilaya/Mkoa. Kuna migogoro ya mipaka kati ya Wilaya ya Meatu (Simiyu) na Ngorongoro (Arusha), Longido (Arusha) na Ngorongoro (Arusha) na Karatu (Arusha) na Ngorongoro (Arusha). Mgogoro kati ya Meatu na Ngorongoro umechochewa zaidi na wawekezaji wa Mwiba Holdings ambao wanasemekana kusogeza mpaka wa Meatu na Ngorongoro na kumega ardhi ya kijiji cha Kakessio ili kunufaika na rasilimali ya wanyamapori waliopo ndani ya hifadhi. Mwiba Holdings Ltd. inasadikika kuwa wanamiliki ardhi ya kijiji cha Makao kinyume na sheria kwani kampuni ya nje ya kijiji mwekezaji hawezi kumiliki ardhi ya kijiji bila ardhi hiyo kuhuishwa na kuwa ardhi ya jumla na hati kutolewa na kamishina wa ardhi. Aidha, kampuni hiyo inafanya ufugaji wanyama pori pembezoni mwa Hifadhi ya Ngorongoro na Pori la Akiba la Maswa kinyume cha Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni rai kwamba Wizara ifute miliki ya Mwiba Holdings kwenye ardhi ya kijiji cha Makao, lakini vilevile Wizara ishirikiane na TAMISEMI kupima mipaka ya Wilaya zenye mgogoro. Naunga mkono hoja.