Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya masuala haya ya ardhi, ndugu yangu Mheshimiwa William Vangimembe Lukuvi, kwa kazi yake nzuri anayoifanya pamoja na Naibu Waziri wake. Niseme tu kwamba sisi kama Serikali tutaendelea kushirikiana nao ili haya yote yanayojiri kwenye migogoro ya ardhi yaweze kupatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kusema kwamba yale yote ambayo yanafikiriwa kwamba Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ingeyachukua na kuyashughulikia kwa uzito, Kaimu Kiongozi wa Shughuli za Serikali hapa Bungeni yupo na ameya-note vizuri. Mimi pia kama Waziri mwenye dhamana chini ya ofisi hiyo basi niseme kwamba tunayachukua yote. Waheshimiwa Wabunge tuwahakikishie kwamba tutayafuatilia na tutayatekeleza na tutashauriana na ninyi ili kuboresha haya yote yaliyojitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza sana Wabunge wa Mkoa wa Dodoma na hapa leo wamewakilishwa vizuri sana na Mheshimiwa Felister Bura, amezungumza vizuri sana habari ya CDA na Mheshimiwa Kunti naye amezungumza vizuri sana habari ya CDA. Niseme Wabunge hawa wawili wamewawakilisha Wabunge wenzao wa Mkoa wa Dodoma lakini naamini kabisa Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini, ndugu yangu Mheshimiwa Mavunde naye amekuwa mstari wa mbele sana kushughulikia masuala haya yanayohusiana na CDA. Wote kwa ujumla wao mara nyingi wamekuwa wakinieleza habari moja ama nyingine kuhusiana na CDA. Kwa hiyo, naomba tu niwahakikishie Wabunge wa Mkoa wa Dodoma na Wabunge wengine wote na Watanzania kwa interest ya kuhamishia makao makuu yetu ya nchi hapa Dodoma tuko pamoja na tutashirikiana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Wabunge wote wa Mkoa wa Dodoma na hasa Mbunge mwenyeji wa Jimbo la Dodoma Mjini, nadhani itapendeza sana kama tutapata nafasi kabla Bunge hili halijaisha tungekutana ili tutizame haya yote ambayo yamekuwa yakijiri kwa CDA hapa Dodoma. Pia tutathmini kwa pamoja umuhimu wa kuhamishia makao makuu ya nchi hapa Dodoma na hii itakuwa pia kwa faida ya wananchi wa Mkoa wa Dodoma.
Kwa hiyo, naomba tu nichukue nafasi hii kuwahakikishia Wabunge wa Mkoa wa Dodoma kwamba tuko tayari sisi kama Serikali na mimi Waziri niko tayari kukutana nao na tukatathmini haya matatizo ambayo wanafikiri kwamba yamekuwa yakijitokeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ili kuwapa matumaini vizuri naomba niwathibitishie kwamba tumeanza kujipanga na CDA na hasa baada ya Mkurugenzi wa CDA kuthibitishwa rasmi na Mheshimiwa Rais, mwezi Februari, 2016, kuona kwamba tunarudisha mahusiano mazuri kati ya CDA na wananchi wa Mji wa Dodoma na kumaliza ile migogoro yote ambayo ilikuwa ikijitokeza kwa namna moja ama nyingine. Ijumaa nilianza kwa kufanya kikao na wafanyakazi wote wa CDA, tumekutana kwa pamoja, tumejitathmini kwa pamoja na tumejenga mkakati wa pamoja wa kuhakikisha kwamba tunapohamia hapa Dodoma kwa kweli wao wana wajibu mkubwa wa kusimamia mambo na mipango yote itakayowekwa. Kwa hiyo, naomba tu niwathibitishie kwamba tuko pamoja na tutaifanya kazi hii kwa uadilifu mkubwa.
Mheshimiwa mwenyekiti, lakini jambo lingine naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba ili kuondoa kutokuelewana kwenye masuala haya kati ya CDA na wananchi wa hapa Dodoma tumefikiri ni lazima tuharakishe sana kuleta ile sheria ambayo itaitambulisha vizuri Dodoma kama capital city. Kwa hiyo, sheria ile tumeanza kuitengeneza na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba sheria ile iko mbioni kabisa kuletwa na niwaombe tutakapoileta ndani ya Bunge basi mtusaidie kuipitisha. Tukiipitisha sheria hiyo itasaidia sana kupunguza migongano na migogoro mingi ambayo inajionyesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ile pia itasaidia kusimamia azma ya Serikali ya kuhamia hapa Dodoma. Niwathibitishie tu kwamba ni lengo hasa la Serikali kuhamia Dodoma na iko pia kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, ni lazima tuone kwamba katika kipindi hiki tunajitahidi kuhamisha makao makuu na kuyaleta hapa Dodoma na hilo tutalisimamia na sheria itatusaidia sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini sheria hii pia itaondoa migongano ya kisheria kati ya taasisi mbalimbali ambazo pia zinasimamia matumizi ya ardhi katika makao makuu haya yanayotarajiwa kwenye mji huu wa Dodoma. Vilevile itaondoa pia migongano ya kisheria kwa sababu pia zipo sheria nyingine mbalimbali kwa mfano Sheria ya Local Government Authority na sheria nyingine. Tutakapoileta sheria hii itakuwa ni mwarobaini, itatusaidia sasa ku-define mipaka ya CDA lakini kutoa tafsiri halisi ya majukumu ya kila chombo ili migongano hii yote iweze kuondoka na azma hii ya Serikali ambayo ni njema iweze kutekelezeka ikiwa imefanikiwa kwa kiasi kikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niendelee kutoa rai kwa wananchi wote wa Dodoma waamini Serikali yao inafuatilia kwa karibu sana kwanza kuhakikisha azma hii inatekelezeka lakini vilevile kuona kwamba migogoro inaisha kwa kufuata sheria na taratibu tulizojiwekea. Niwaombe wananchi wa Dodoma pale wanapoona kuna matatizo waamini kwamba sisi kwa kushirikiana nao tunaweza tukafanya vizuri sana na siyo vinginevyo. Sisi tuko tayari na tumeanza kufanyia kazi changamoto zilizopo na juzijuzi tu tumemaliza migogoro kadhaa ambayo ilikuwa inawakabili wananchi wa Dodoma. Kwa hiyo, waamini ile migogoro iliyobaki tutaendelea kuumaliza mmoja baada ya mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile waelewe kwamba na wao wanatakiwa kufuata sheria na kuzingatia sheria, kila jambo ni lazima litaenda kwa kuzingatia sheria. Pale ambapo tutaona kwamba wana haki watapewa haki yao na pale ambapo wao wanaona kabisa sheria inawataka watekeleze majukumu mengine naomba watupe ushirikiano. Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ameamua kabisa kufanya kazi na sisi ili kuhakikisha kwamba tunamaliza matatizo haya yanayojitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini kabisa sheria hii pia itatufanya tuweze kuwa na mji wa kisasa, makao makuu ya nchi ambayo yatafanana na hii azma ya Serikali yetu tuliyonayo. Waheshimiwa wengi wamezungumza hapa, Mheshimiwa Shally ametuuliza mnakwenda kutembea huko hamuoni miji ya wenzenu ilivyo? Naomba nimthibitishie Mheshimiwa Shally tumeona, tumejifunza miji mingi jinsi ilivyo mizuri na hivyo tunataka kuujenga Mji wa Dodoma uwe nao una picha ambayo itaweza kupeleka ujumbe wa namna nchi yetu ya Tanzania ilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi mkiangalia jinsi Mheshimiwa Rais wetu sasa hivi hata ukienda kwenye mataifa mengine amekuwa akitambulika kwa sifa na heshima kubwa sana. Kwa hiyo, tutakapoujenga mji huu katika kipindi hiki cha kwake pia itabidi uendane na hadhi ya nchi yetu na vilevile uendane na kile tunachokifikiri kitakuwa ni sura ya Taifa letu katika mataifa mengine katika ulimwengu mzima. Naomba tu niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge tumeanza kufanya kazi ya kutosha ya kujenga miundombinu na tutaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo naomba niwahikikishie tuko tayari tutafanya kazi pamoja na ninyi na CDA kujenga makao makuu ya nchi hapa Dodoma. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.