Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia afya na nguvu kuweza kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Naomba nimpongeze Waziri Maghembe na timu yake kwani hotuba yake ina vina, imegusa, lakini nimuombe isiwe ya maandishi tu iwe ya vitendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite moja kwa moja katika kuchangia juu ya upandaji wa miti. Miaka ya nyuma misitu iliungua baadhi ya maeneo katika nchi hii, hususani Lushoto, mpaka sasa hivi maeneo yale bado ni mapori hayajapandwa miti. Niishauri Serikali yangu sikivu iandae mikakati kwa ajili ya kupanda miti katika maeneo yale kuanzia Korogwe, Lushoto mpaka kushuka maeneo ya Same kule ni jangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pamoja na kupanda miti iwasaidie pia wakulima mmoja mmoja wa miti waweze kupanda kwenye mashamba yao, kwani ukitaja Lushoto ndiyo kuna wahifadhi, watunzaji wa mazingira wakubwa sana. Leo hii maeneo yale ambayo ni vichaka yanatia aibu. Naiomba Serikali yangu tukufu ipange fungu kwa ajili ya kupanda miti katika milima ile ya Lushoto, pia iwasaidie wakulima hawa mmoja mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie moja kwa moja kwenye mgao na uvunaji. Tunashukuru tumepakana na misitu ya Shume, Mazumbai, Baga, Gare, lakini misitu ile bado haisaidii wananchi. Katika mgao wanaangalia wale watu ambao wana uwezo na kila mwaka watu wanaopewa mgawo ni wale wale. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu na nimuombe Waziri Maghembe kipindi hiki ahakikishe kwamba mgao ule aufuatilie waliopata ni wangapi na ni wa aina gani? Mimi kama Mbunge wao wamenituma baada ya kulalamika kilio hiki kwa muda mrefu sana. Mgao huu pia au uvunaji huu haujazingatia watu wanaochakata viwandani, kwa mtu mmoja mmoja na kwa vikundi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la uvunaji kwa mtu mmoja mmoja. Misitu ya Serikali hii watu wanapeleka kuchakata kwenye viwanda, viwanda viko mbali sana na miti ile. Kuna sehemu wanaita Makanya, Ngwelo, Gare, Ubiri, Lushoto, Mbwei, Malibwi na Kilole, maeneo haya yako mbali sana na viwanda. Kitu cha ajabu na cha kushangaza watu hawa wameweka sheria moja kwa ajili ya kuvuna kwa vikundi au kwa ajili ya kuvuna na chainsaw, wamekataza kuvuna kwa chainsaw wavune kwa shoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana wakulima wangu wale wa miti sasa waruhusiwe kuvuna kwa chainsaw kwani ukitoa mti kutoka Makanya au mtu wa Makanya akivuna mti hawezi kupeleka moja kwa moja mpaka kiwandani, lakini Mheshimiwa Maghembe watu hawa anawakataza anasema kila mtu avune kwa shoka kitu ambacho ni kigumu, ndiyo maana nikasema ameangalia upande mmoja tu kwa ile misitu ya Serikali lakini hajaangalia kwa mtu mmoja mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Maghembe, atakaposimama ku-wind up basi aangalie vitu hivi. Ahakikishe kwamba watu wangu awaruhusu sasa wavune kwa chainsaw. Kwa sababu mtu yule hawezi kukata mti wake kule mpaka akapeleka kiwandani, itakuwa ni shida. Tunawaomba hata mbao za madawati wanashindwa kuvuna wanasema kwamba tumekatazwa kuvuna kwa chainsaw. Kwa hiyo, hili ningeomba baada ya kusimama Mheshimiwa Maghembe basi alitolee ufafanuzi, ili watu wangu waweze kuvuna kwa chainsaw.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru Mheshimiwa Maghembe alitembelea Jimboni kwangu kule Lushoto, alikuta changamoto, pamoja na kwamba sikuwa na taarifa za ujio wake kama angenipa taarifa, basi ningemwambia hali halisi ilivyo, yeye alienda moja kwa moja mpaka ofisini kwa wataalam wake tu, na alipofika kule alichukua maneno ya wataalam akayaacha ya wananchi. Ninamshauri siku nyingine akienda atafute na Wabunge, hii siyo kwa Waziri Maghembe tu, Waziri yeyote atakayeenda site basi atafute Wabunge kwa sababu Wabunge ndiyo wanajua changamoto zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema Lushoto inapakana na msitu, ninamuomba Mheshimiwa Maghembe kuna akina mama kule wanatafuta kuni msituni wanakamatwa, shoka zao zinachukuliwa zinaenda kuhifadhiwa ofisini, mapanga na kila kitu, watu wale ni walindaji wakubwa wa misitu. Nashukuru Mheshimiwa Maghembe alienda pale akawaambia kina mama wale basi waendelee kutafuta kuni na waende na mapanga na mashoko, lakini wasije wakatafuta mti ambao ni mbichi. Kwa hiyo, nimuombe atakaposimama basi aliongelee hilo suala hapa ili liingie kwenye Hansard na watu wangu waweze kupata nguvu kwa ajili ya kutafuta kuni msituni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri wa Maliasili na Utalii, ashirikiane na Waziri wa Viwanda, kuna Kiwanda cha Ceiling Board pale Mkumbara; kiwanda kile kinakufa, hakina tatizo lolote, kina skyline inatoa magogo kutoka Shume kushuka chini. Lakini kwa sasa hivi kinakufa, na kinakufa bila sababu yoyote, ningemuomba sasa Mheshimiwa Waziri Maghembe na Mheshimiwa Mwijage wafike pale Mkumbara Ceiling Board, waone kiwanda kile jinsi kinavyonyanyasika, na watu wa pale jinsi wanavyonyanyasika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa pale hata kulipa bili ya umeme wameshindwa, sambamba na hayo naamini kabisa Mheshimiwa Mwijage na Mheshimiwa Maghembe watakapofika Mkumbara basi moja kwa moja wataenda mpaka kwenye Kiwanda cha Chai Mponde, naamini Mheshimiwa Mwijage kama kweli ana hofu ya Mungu atatoa sauti yake na kufungua viwanda vile, wananchi wa kule wananyanyasika, hata kulipia karo ya shule wanashindwa, hata mlo ni mmoja kwa sababu ya chai yao kiwanda hakijafunguliwa wanashindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Mwijage, nitamwekea hata mafuta aende Mkumbara Ceiling Board kwa sababu itakuwa ni ziara yake hiyo basi aende mpaka Mponde pale aone wakulima wa chai wanavyonyanyasika…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.