Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Pia namshukuru Mungu kwa kutuamsha salama na kutufikisha hapa. Nami naomba nichangie mambo machache juu ya hii hotuba ya Mheshimiwa Profesa Maghembe. Nataka kuwapongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa hotuba nzuri iliyosheheni masuala mbalimbali ya maendeleo ya utalii na uhifadhi katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kusikitika juu ya bajeti ya Wizara hii. Wizara hii ni kati ya Wizara ambazo zinachangia pato kubwa sana kwa nchi yetu na ina fursa kubwa sana ya kuchangia pato letu la Taifa, lakini ni Wizara ambayo vilevile haitendewi haki inapokuja kwenye bajeti. Bajeti yake haiendani na uwezo wa Wizara hii kuiletea nchi yetu mapato. Wizara hii haitengewi bajeti ya kutosha kwa utangazaji, tumeona mifano mingi ya nchi jirani na nchi nyingine duniani kiasi ambacho wanatenga kwa ajili ya utangazaji peke yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna vivutio vingi sana na tunapenda kujikumbusha kila mara, lakini vivutio hivyo tunavijua sisi tuliomo humu ndani, walioko nje ambao wanatakiwa kuja kuvifaidi hawavitambui. Kwa hiyo, ni muhimu kwa Serikali kuhakikisha kuwa matangazo yanapewa bajeti na profile ya kutosha ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha watalii wanavutiwa kuja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia utalii wa ndani. Bado utalii wa ndani haujapewa kipaumbele au haujazingatiwa. Sisi Watanzania vile vile tunaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa sana utalii wa ndani. Kama hiyo haitoshi, Maafisa Maliasili walioko katika wilaya hawazitendei haki fursa za utalii zilizoko katika wilaya zetu. Karibu wilaya zote zina nafasi na fursa za vivutio vya utalii, lakini inaonekana yanazingatiwa maeneo makubwa makubwa tu ya Kaskazini, hifadhi za wanyama lakini hatuangalii utalii wa aina nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija katika Mkoa wangu wa Songwe peke yake kuna vivutio vingi sana vya utalii. Kuna vijito au chemichemi za maji ya moto, hicho ni kivutio cha kutosha. Tuna kimondo Mbozi ni kivutio cha kutosha. Zamani tulikuwa tunasikia kinatajwatajwa sasa hivi hata kutajwa hakitajwi tena. Mikoa yetu sisi ni ya milima na mabonde ambayo ni mizuri sana kwa utalii wa kijiografia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watalii wengi wanapenda kupanda milima, trekking na camp sites. Watalii wengi wanapenda sana kuja kuangalia mazingira yetu jinsi tunavyoishi. Kwa hiyo, hivi vyote ni vivutio ambavyo vingepaswa kuendelezwa ili vilete kwanza ajira kwa wananchi walioko pale lakini vilevile vituletee mapato kwa ajili ya nchi yetu na kupanua wigo wa utalii ambao unapatikana kwenye nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika vilevile kuwa katika mradi au mpango wa BRN utalii haupo wakati tunajua kabisa kuwa ni chanzo kikubwa cha mapato. Napenda Serikali ituambie huo mpango wa BRN kwa nini umeacha utalii nje na kuacha kuushughulikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la miundombinu ya utalii, kuna matatizo makubwa ya miundombinu ya utalii kwa mfano barabara, hoteli katika maeneo mbalimbali ambayo watalii wanatakiwa kufikia hata katika Mlima Kilimanjaro. Tumesikia na wale waliopanda mlima ule wameona, vile vibanda vinavyotumika kufikia wageni havifai, sasa hivi vinatakiwa viboreshwe kwa kiasi kikubwa, kuna masuala ya vyoo na sehemu za kupumzika zote hazifai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mlima Kilimanjaro ni kivutio kikubwa dunia nzima na wageni wanaokuja pale ni wengi sana kwa nini isitengwe fedha kutokana na Mlima Kilimanjaro peke yake kwa ajili ya kuboresha ile miundombinu ya kutumika kwenda kupanda? Vilevile Watanzania wengi wahamasishwe na wawezeshwe kwenda kupanda Mlima Kilimanjaro, mlima uko kwenye nchi yao lakini wao wenyewe hawajaupanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia vilevile ufugaji wa nyuki na uhifadhi wa mazingira. Tanzania ni nchi ya pili Afrika kwa kuzalisha asali lakini hata kiwango ambacho asali hiyo inazalishwa bado ni kidogo sana. Tuna uwezo wa kuzalisha asali nyingi sana Tanzania, lakini Maafisa Maliasili wetu wala hili hawalizingatii. Wanakimbizana na kuuza magogo tu na kukata miti tu, jamani sasa hivi warudi kuzingatia mambo ya utalii katika maeneo yetu, lakini vilevile ufugaji wa nyuki na upandaji wa miti. Hii ndiyo njia pekee ambayo kwanza itatuletea uhifadhi lakini vilevile itatuwezesha kufuga nyuki wengi na kupata pato kubwa na kwa vijana wetu ufugaji wa nyuki ni ajira nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kurudi kwenye suala la Bodi ya Utalii. Pamoja na malalamiko kuwa haipati fedha ya kutosha lakini bado na yenyewe haitumii ubunifu wa kutosha. Kuna mambo mengine bodi inaweza kufanya bila kutegemea fedha nyingi. Nchi yetu mara nyingi inashiriki kwenye maonesho nchi za nje, ya kibiashara, mikutano mikubwa ya Kimataifa na maonesho ya mambo mbalimbali, hizi ni fursa zinazoweza kutumika vilevile katika kutangaza utalii wetu. Tuna fursa vilevile za sisi wenyewe kukusanya watu nje ya nchi, wafanyabiashara au watalii wenyewe, ma-agent wa utalii kuja katika maonesho hayo ili tuoneshe nini tunacho ili waweze kuvutiwa. Hili suala naona bado halijatiliwa mkazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mheshimiwa jana alisema kuwa ni wavivu, mimi naweza nikakubaliana naye, kwa sababu uvivu ni pamoja na kutokuwa mbunifu. Kama umepewa majukumu lazima uyatendee haki majukumu yako kwa kuhakikisha unajituma kwa kiasi kikubwa ili nchi yako ikafaidike. Hatuwezi kuendelea kuimba nyimbo za kuwa sisi tuna vivutio vingi wakati vivutio hivyo hatuviendelezi wala havituletei faida yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea ningependa kutoa pendekezo kuhusiana na miundombinu ya hoteli. Tunasema kuwa sisi tuna upungufu mkubwa wa vitanda ndiyo maana watalii hawaji kwa wingi. Nataka kutoa pendekezo ambalo naomba lifikiriwe kuwa, mifano imeonekana kwa nchi nyingine kwa mfano Zambia, walitoa msamaha wa kodi na ushuru kwa wale wanaokuja kuwekeza kwenye hoteli za nyota tatu mpaka tano kwa kipindi cha miaka miwili wakati wanajenga na baada ya kumaliza ujenzi wakati wa kuanza ku-operate zile hoteli ndiyo wakaanza kulipishwa kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi sana walijitokeza kujenga hoteli katika sehemu mbalimbali za utalii na sasa hivi Zambia wanapata watalii wengi. Hebu na sisi tulitafakari hilo, tulifanyie mahesabu tuone, je, itatugharimu kiasi gani kwa muda wa miaka miwili, mitatu kuachia wawekezaji wajenge kwa misamaha maalum, baada ya hapo tuanze kuwatoza kodi inayostahili na tutahakikisha kuwa tunapata watalii wa kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwa hoteli zilizopo ziboreshwe, watenda kazi wafundishwe jinsi ya kuhudumia wageni ili tuweze kuwa na ubora unaohitajika kwa sababu tunalalamika sana kuwa wanakuja wageni kuja kufanya kazi katika hoteli zetu lakini ni kwa sababu wafanyakazi wetu labda hawajapata ujuzi wa kutosha jinsi ya kuhudumia watalii na kutoa huduma ambazo zinafaa kuvutia watalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja hii, lakini naomba yote ambayo tumeyatoa hapa yakazingatiwe. Ahsante.