Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kuchangia katika Bajeti ya Serikali na Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri inaiyofanya ikiwemo ukusanyaji wa mapato. Serikali imekuwa ikikusanya mapato vizuri tumeona na mpaka sasa imeshafikia zaidi ya asilimia 100 ya ukusanyaji wa mapato yanayotokana na kodi. Changamoto ninayoiona ni ule upelekaji wa fedha katika Halmashauri mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kitabu cha mkaguzi alichokisoma cha hesabu za mwaka 2014/2015 tumeona upelekaji wa fedha za miradi ya maendeleo katika Halmashauri tatu zilipelekwa zaidi kuliko fedha zilizoidhinishwa na Bunge. Halmashauri moja imepelekewa fedha za miradi ya maendeleo zaidi ya asilimia 56 nyingine kwa zaidi ya asilimia 59 na nyingine kwa zaidi ya asilimia 63. Ukiangalia maeneo mengine pia tunayo miradi inayopaswa kutekelezwa, tuna maboma ya zahanati ambayo hayajakamilika, tuna miradi ya maji ambayo haijakamilika. Hata ukiangalia fedha za mwaka huu kwa namna tulivyokusanya ukiangalia ofisi ya CAG ambayo ndiyo inayokagua na kudhibiti matumizi ya fedha ilipelekewa fedha kwa asilimia 52 za ruzuku ukilinganisha na idara nyingine zikiwemo na Wizara zimepelekewa fedha zaidi ya asilimia 100, nyingine asilimia 117, asilimia 125, asilimia 124, sijui ni kigezo gani kinachotumika kupeleka fedha. Naishauri Serikali izingatie uidhinishaji wetu wa Bunge tunavyoidhinisha isitumie fedha nje ya bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Mkaguzi Mkuu kwa mwaka huu imeonekana kupunguziwa fungu lake na ukiangalia Serikali katika kutekeleza miradi ya maendeleo tumetoka asilimia 26 na sasa tumeweka asilimia 40 ya fedha ya miradi ya maendeleo. Ofisi ya CAG inatakiwa iwezeshwe kikamilifu ili iweze kutekeleza majukumu yake. Kwa mwaka uliopita CAG alishindwa kukagua miradi ya maendeleo ya vijijini, aliishia ngazi ya Halmashauri, tukiangalia Halmashauri ni receiving station, miradi inafanyika katika ngazi ya chini. Fedha ya capital development grant ambayo ni fedha ya maendeleo asilimia 50 inapelekwa vijijini, endapo CAG atakuwa anaishia katika ngazi Halmashauri hakuna ambacho tutakuwa tunakifanya kuhusu matumizi mabaya ya fedha za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika subvote 1005 ambayo inahusiana na Serikali za mitaa safari za ndani, mwaka wa fedha uliopita ilitengewa shilingi bilioni 5.4 lakini mwaka huu imetengewa shilingi milioni 332 sawa na asilimia sita tu. Kwa hiyo, naomba ofisi hii iangaliwe vinginevyo fedha tunayopeleka itakuwa haifanyi mambo yaliyokusudiwa.
Napenda pia nichangie kuhusu Hali ya Uchumi wa Taifa katika mwaka 2015. Kiwango cha ukuaji wa shughuli za kiuchumi za kilimo na mifugo kwa mwaka 2015 zilionekana kushuka ikilinganishwa na mwaka 2014. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite zaidi katika Mkoa wa Simiyu. Wananchi wa Mkoa wa Simiyu uchumi wao unategemea kilimo na ufugaji. Tukiangalia ufugaji, mifugo hiyo inatumika kuuzwa na kununua chakula kwa ajili ya familia, kuuzwa na kununua mahitaji kwa ajili ya familia na hata sasa nimeona wananchi wangu wa Mkoa wa Simiyu wakichangia mifugo kwa ajili ya ununuzi wa madawati kwa ajili ya wanafunzi wetu, naomba niwapongeze sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mifugo hii ina changamoto nyingi sana, athari ya mabadiliko ya tabia ya nchi yameathiri upatikanaji wa maji pamoja na malisho. Niiombe Serikali upande wa maji wakati wa utekelezaji wa ule mradi wa kutoa maji ziwa Victoria na kuyaleta Mkoa wa Simiyu, itoe pia kipaumbele cha upatikanaji maji kwa ajili ya mifugo, endapo maji yale yote yataingia katika treatment plant mifugo haitaweza kutumia yale maji kwa sababu yatakuwa na gharama kubwa. Naomba Serikali ikumbuke kutenga maji kwa ajili ya mifugo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu malisho, mifugo imeonekana kukonda na mengine kufa kwa ajili ya ukosefu wa malisho na hata ikienda kwenye minada bei imeonekana kuwa ya chini kwa sababu ya ule udhaifu. Niiombe Serikali iweze kupitia mipaka upya ya hifadhi ya Busega, Bariadi, Itilima na Meatu ili kuweza kupatikana eneo kwa ajili ya malisho kwa sababu jamii imekuwa ikiongezeka na mifugo imekuwa ikiongezeka pamoja na athari ya mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe pia katika vijiji vinavyounda WMA vilivyopo Wilaya ya Meatu Serikali iharakishe mchakato wa matumizi bora ya ardhi ndani ya hifadhi ili wafugaji waweze kupata sehemu ya kuchungia pamoja na kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiongelea kuhusu kilimo cha pamba, zao la pamba limeonekana likidolola mwaka hadi mwaka, wakulima wamekuwa wakilima pamba badala yake wamekuwa hawarudishi ile gharama wanayotumia katika kilimo. Serikali inao mpango mzuri wa kuweza kuleta viwanda vya nguo kwa ajili ya kuongeza thamani ya zao la pamba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata viwanda vilivyopo nikiongelea Kiwanda cha Mwatex 2001 Ltd. Kiwanda hicho baada ya kubinafsishwa kilianza kufanya kazi 2003 kilishindwa kuendelea kwa sababu ya changamoto mbalimbali. Naomba Serikali itatue hizo changamoto ambazo changamoto mojawapo ni upatikanaji wa nishati ya kutosha, upatikanaji wa maji, Kiwanda cha Mwatex kiko kanda ya ziwa ya umeme Mkoa wa Mwanza ambapo kuna ziwa Victoria, Serikali ifanye jitihada za haraka kuhakikisha upatikanaji wa maji ya kutosha. Changamoto nyingine iliyokikumba kiwanda hicho ilikuwa ni watumishi wasio na ujuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.