Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba nimpongeze Waziri kwa kazi nzuri na hasa kwa hatua yake ya kuwatimua baadhi ya watumishi wasio waaminifu katika Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Nampongeza sana Waziri kwa hili na namwomba aendelee kwa sababu bado wezi wapo wengi na ndiyo maana kwa kiasi kikubwa fedha nyingi zinazopatikana za utalii zinaishia mikononi mwao. Nampongeza sana kwa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Niwapongeze baadhi ya Wabunge na hasa wale ambao kwa namna moja au nyingine wametambua jitihada, uhifadhi wa mazingira unaofanywa na baadhi ya makabila ambayo yanaishi katika hifadhi zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu turudi nyuma kidogo. Nimefurahishwa na baadhi ya michango na baadhi ya michango mingine kwa kweli inaniweka katika wakati mgumu. Ni kweli, wanasema kitanda usichokilalia huwezi kujua kunguni wake; najua kunguni wake, kwa sababu hata mimi pia nimesomeshwa na mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo kati ya wafugaji na wakulima linahitaji busara, kwa sababu kila mmoja anavutia upande wake. Wengine wanasema kwamba wafugaji ni waharibifu na ndiyo chanzo cha uharibifu wa mazingira. Katika kumbukumbu zangu, Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa mikoa ambayo ilikuwa inatiririsha maji kwa kipindi chote cha mwaka mzima, lakini leo hii hata mkoa huu kwa kiasi kikubwa hayo maji ambayo siku za nyuma Mwanamuziki Salum ambaye alikuwa ni mzaliwa wa Morogoro aliimba kwamba Mji wa Morogoro unatiririsha maji safi, lakini leo si kama ilivyokuwa zamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote ni kutokana na uharibifu wa mazingira uliofanywa na wakulima katika vyanzo vya milima; je, hapa wafugaji wanaingia vipi? Kwa sababu wafugaji ndiyo wanaohesabika kwamba ni waharibifu wakubwa wa mazingira; ndiyo maana nikasema hili jambo linahitaji busara. Humu ndani kila mmoja atavutia upande wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wataalam wetu wasipokaa, wakaandaa mipango ambayo itawawezesha wafugaji waweze kufuga kwa amani na utulivu, wakulima waweze kulima pasipo usumbufu wowote ili pasiwepo na malalamiko ya watu mifugo yao kuuawa, kusiwepo na malalamiko ya wananchi nyumba zao kuchomwa moto, tutapata shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tu tulishuhudia ukatili uliofanywa kwa baadhi ya mifugo kule Morogoro. Kwa maana hiyo, kama busara isipotumika, narudia tena kama busara isipotumika, wataalam wetu wakakaa, mipango hii ikapangwa kuhakikisha kwamba kila mmoja anafuga katika eneo ambalo Serikali imeweka mipaka, inatambua lile eneo na linatambuliwa eneo hili ni kwa ajili ya wakulima, hii migogoro itaendelea kuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wanasema ng‟ombe ni wadudu, lakini utashangaa ndiyo hao hao wanakula nyama. Ikifika Jumamosi Waheshimiwa wengi tunakimbilia mnadani, tunakwenda kula nyama hivi kama wafugaji wasingefuga tungekula wapi hizo nyama? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vyema tukatambua kwamba kila mmoja ana nafasi yake katika nchi hii na hata hao wanaohama kutoka sehemu moja kwenda nyingine hakuna anayependa; hebu fikiria kutoka Mwanza mtu mpaka anakwenda Lindi mwendo huo ni wa siku ngapi? ni kutokana na kutokuwepo na mipango ambayo inawafanya hawa watoke sehemu moja kwenda eneo lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo narudia tena busara itumike ili tuweke mipango ya kuhakikisha kwamba kila Mtanzania ana haki ya kuishi katika nchi yake, popote pale anapoweza, ili mradi tu kwamba sheria hazivunjwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano katika Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, zipo sheria za tangu mwaka 1959; pamoja na kwamba ipo Sheria ya 2009 au 2010 lakini je, hii sheria ya tangu enzi za ukoloni ni lini sheria hii italetwa ili ifanyiwe marekebisho? Kwa kufanya hivyo tutapunguza kwa kiasi kikubwa migogoro, tutawaacha watu wanaoishi katika jamii ile, hasa ya wafugaji ambao ni Wamasai, wataishi lakini pia wakitunza mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri pia Serikali, kuhakikisha kwamba katika haya mapori tengefu, yapo maeneo mengine ambayo tuwaachie wafugaji, kwa maana kwamba, kama kweli yakitengwa na kuhakikisha kwamba wafugaji na wao wanafuga; kwa sababu tangu tunazaliwa wananchi, babu zetu, mama zetu, baba zetu, walikuwa wakiishi huko. Kwa hiyo, tuangalie ni maeneo gani ambayo ni mapori tengefu, tutawatengea wananchi wetu ili waweze kuishi na mifugo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nije katika suala la utalii. Katika suala la utalii nimwombe Mheshimiwa Waziri, hebu aiangalie Bodi ya Utalii, sioni kama kuna kazi wanafanya, kwa sababu tuliwatarajia hawa waweze kutangaza kwa kiasi kikubwa utalii wetu, lakini mpaka leo kitu gani kinachofanyika?
Mheshimiwa Mwenyekiti, twende katika Jiji la Dar es Salaam, hivi mtalii anaposhuka katika Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam kuna kituo gani pale anakwenda kupata maelezo kuona kwamba Tanzania kuna utalii huu? Hakuna! Akitoka katika uwanja wa ndege anapoingia barabarani anakaribishwa na mabango ya simu yanatusaidia nini sisi Watanzania? Kwa nini tusitumie haya mabango kuhakikisha kwamba ni njia mojawapo ya kutangaza utalii wetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jiji la Dar es Salaam, wengi na ndiyo maana kila siku wanazidi katika hili jiji la Dar es Salaam. Hivi katika sheria za mipango miji na hasa kwa sababu utalii si lazima twende mbugani tu, hata baadhi ya majengo yakihifadhiwa vyema ni utalii. Leo hii katika majengo ya Posta ambayo yalijengwa kabla hata hatujazaliwa, yanabomolewa yanajengwa mengine, kwa nini tusitenge eneo ambalo haya majengo yakahifadhiwa ili kiwe ni kituo cha utalii tuje tuone haya majengo ya miaka nenda miaka rudi yasaidie hata vizazi vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi suala la utalii lina mapana sana na naumia sana ninapoona nchi ya Kenya inatumia advantage ya sisi kulegalega, vivutio vilivyoko Tanzania wanavitangaza wao. Ndiyo maana siku za karibuni, tulimwona Mkenya amesimama kabisa anasema bonde la Olduvai Gorge lipo nchini Kenya, Serikali imejibu nini? Itumie nafasi hiyo wakati mwingine kuhakikisha kwamba wanaeleza, huo utalii upo Tanzania; lakini Serikali imekaa kimya. Huu ni utalii wa kwetu; ni vitu vya kwetu ambavyo tunajivunia. Mlima Kilimanjaro, mara ngapi wameutangaza, kwa kujivunia kwamba njoo Kenya uone Mlima Kilimanjaro, lakini ukweli ni kwamba Mlima huu upo Tanzania tunajipanga vipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, mtalii anapotoka katika hifadhi tumejipanga vipi kuhakikisha kwamba anapata maeneo mengine ya kwenda kutembelea? Kwa mfano, Mbuga ya Kruger nchini Afrika ya Kusini, Mtalii akitoka pale atakwenda katika Mji wa Soweto. Kule ataweza kushuhudia, wakati mwingine hata mauaji ya watoto yaliyofanyika mwaka 1976; ni vivutio pia wanakwenda kule kuangalia na kujifunza historia. Historia ya Nelson Mandela, katika vitu vingine tofauti tofauti, pesa zinaendelea kubaki, je, sisi tumejipanga vipi? Mtalii anapotoka Ngorongoro, anapotoka kupanda Mlima wa Kilimanjaro anapotoka huku Gombe, anakwenda wapi? Utamaduni wetu ni upi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja.