Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika bajeti hii ya Maliasili na Utalii maana ukizungumzia Jimbo la Mikumi moja kwa moja unazungumzia masuala haya muhimu ya utalii na maliasili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa masikitiko makubwa niongelee jinsi ambavyo wananchi wa Mikumi wamekuwa wakilia kutokana na jinsi ambavyo wanabanwa na migogoro mbalimbali ambayo inasababishwa na kuongezwa mara kwa mara kwa mipaka ya hifadhi ya Taifa ya Mikumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana wananchi wa Jimbo la Mikumi waliokuwa wakiishi katika maeneo ya Kipogoga pamoja na Mgoda walihamishwa mwaka 1963 na kupelekwa kwenye Vijiji vipya vya Vikweme, Rwembe maeneo ya Tindiga na sehemu nyingine. Hiyo ilisaidia kuifanya hifadhi ya Mikumi iweze kuanza mwaka 1963, lakini sasa hivi mipaka hiyo imeonekana kuwa inaongezwa na sasa hivi wananchi wamefuatwa kwenye vijijji, kwa mfano Kijiji cha Vikweme wanaambiwa tena waondoke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Vikweme wamekuwa na kilio cha muda mrefu sana ambapo upande mmoja wanakabwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania na sasa hivi wameambiwa wahame maeneo yale kwa sababu ni ya Jeshi, lakini upande wa pili Hifadhi ya Mikumi inasema ni eneo lao, mnataka wananchi hao wa Mikumi waende maeneo gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wazee ninaozungumza wamehamishwa mwaka 63 ni pamoja na akina mzee Leonard Haule ambaye tulimzika mwaka 1981, ambaye ni babu yangu. Wazee mwenzake akina mzee Mbegani mpaka leo wamekuwa wakitaabika na wakiililia Serikali kwamba mnataka waende wapi wakati wenyewe ndiyo watu wa Mikumi wazawa waliokuwa pale?.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na migogoro mingi kutokana na hifadhi kuongeza mipaka katika maeneo mengine kama ya Uledi, Ng‟ombe ambapo inaonekana kuna heka karibu 200 za wakazi wa Lugawilo ambao hifadhi pia imesema huu mpaka ni mpya. Wananchi wa huku wamekuwa wakilia kwa muda mrefu wakiitaka Serikali iweze kurudisha ule mpaka wa zamani wa mwaka 1957 uliokuwa ukiwawezesha kupata ardhi ya kulima na kujenga nyumba zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakazi kama wa Vikwema, Kitete Msindazi, maeneo ya Mululu, maeneo ya Msange pamoja na maeneo ya Lumango wameonekana kuwa wanataabika kwa sababu wamekuwa na ugomvi wa mara kwa mara na watu wa hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna suala la buffer zone. Eneo la Buffer Zone limekuwa likiongezeka kila siku. Eneo hili wananchi hawatakiwi kuingia kabisa. Mama zetu wamekuwa wakipigwa kwa sababu ya kuingia kuokota kuni kwenye maeneo haya. Ndugu zetu wamekuwa wanataabika na sasa tumesema kuwa Mikumi mpya ya Profesa J. tunataka haya mambo yakome na tuweze kukaa chini na wananchi ili tuweze kusuluhisha. (Makofi)
Mheshimwia Mwenyekiti, tunapozungumzia masuala ya hifadhi tunazungumzia ujirani mwema. Hapo zamani sisi tulipokuwa tunakua tulikuwa tunaingia kwenye mbuga ya wanyama ya Mikumi kwenda kuona wanyama, lakini pia tukicheza michezo pamoja na Maaskari wa Wanyamapori na vitu vingine kama hivyo. Pia walikuwa wakitusaidia kujenga zahanati, shule na wanafunzi walikuwa wakibadilishana uwezo. Sasa hivi kumekuwa na uadui mkubwa kati ya watu wanaokaa katika vijiji vinavyopakana na hifadhi na wahifadhi wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiongelea suala la ujirani mwema kwa sababu tunasema wananchi kama watathaminiwa watapewa thamani wanaostahili na fidia lakini pia watashirikishwa kwenye mambo mbalimbali, hii itawasaidia sana kulinda rasilimali zetu na wanyama wetu. Kwa hiyo, tunataka tusisitize suala la ujirani mwema ili tuweze kuwatumia wananchi kuweza kulinda wanyama wetu na rasilimali zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa style hii mnayosema kila siku kuna ujangili, wananchi wanawachukia tembo, wanawachukia askari wa wanyamapori na ndiyo wamewaweka kama maadui, kwa hiyo hata wakiona majangili wanaingia hawawezi kuwapa ripoti ndugu zangu wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli mnataka tulinde rasilimali zetu, tuwape nafasi hiyo wananchi wa Tanzania tuwaoneshe umoja na ushirikiano, tuwaoneshe jinsi ya kucheza michezo ya pamoja; na kama inahitajika tuwape elimu ili wajue kitu gani cha kufanya na kipi sio cha kufanya, lakini sasa hivi ndugu zetu wanaokaa kwenye vijiji vinavyopakana na mbuga wameonekana kuwa wanateswa. Niwaambie tu Mikumi kuna watu wengine tumezika nguo kwa sababu hata maiti zao hatujaweza kuzipata kwa sababu wamepigwa risasi ndani ya hifadhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kutokana na hilo tunataka tuisisitize Serikali kama kweli mnataka tulinde rasilimali za Mikumi tupunguze uadui huu kati wa wananchi wanaoishi kwenye vijiji vinavyopakana na hifadhi na watu wa hifadhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tuzungumzie pia masuala ya tembo. Wanyama hawa sasa hivi imekuwa kama fashion kila mtu anayekaa karibu na hifadhi anazungumzia masuala ya tembo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa juzi, karibu wiki mbili katika kijiji kilicho katikati ya Kilosa na Mvomero kinachoitwa Mangae mtu mmoja ameuawa na tembo. Sasa ndugu zangu Serikali kila anapokufa mtu ndipo mnataka mje? Kila siku tunalia, tunapaza sauti ndugu wanakufa lakini hakuna linalochukuliwa lolote. Tunataka tuwaambie tunawapenda tembo, tunapenda ralisilimali zetu, tunaomba mtusikilize na sisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zetu wanalima mashamba makubwa ya mpunga, watu wanatumia hela nyingi, lakini tembo wanakula zile mali. Wananchi wanapata tabu, sasa hivi kuna mafuriko huko Mikumi, watu wana njaa, wanajitahidi kulima lakini tembo wanakula, Serikali imekaa kimya. Kuna Kata inaitwa Kilangali kila siku wimbo ni kuhusu tembo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba, tunaomba watuangalie kwa jicho pevu, itafika kipindi hawa wananchi watachoka na tutaamua kufanya jambo litakalokuwa baya, watatuongeza kwenye magereza yao. (Makofi)
Mheshimimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho kinatakiwa kusema ni kwamba, tunaangalia sana utaratibu wa kuwatunza tembo wetu lakini pia kuna suala la mamba, ambapo katika mto Mwega kwenye Kata ya Maloyo, mamba wameonekana kujeruhi sana ndugu zetu na watu wengine wamekufa. Kitu cha kustaajabisha ni kwamba, Halmashauri ya Kilosa imenunua bunduki mbili kwa ajili ya kuongezea nguvu kwenye maliasili, lakini cha ajabu ni kwamba mpaka leo wameshindwa kupata vibali kutoka mkoani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atumie nafasi hii. Halmashauri ya Kilosa imenunua bunduki, lakini vibali vinaonekana kupigwa chenga. Sasa tusije tukawafanya wananchi na sisi tukawaambia watumie mbinu mbadala ili kuweza kukabiliana na wanyama hao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa pale Mikumi tozo lote limeonekana kuwa linakwenda kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina, wananchi wa Mikumi wamekuwa lonely, pesa ya pale haiwahusu, ni kama wamekaa kisiwani hata mbuga imekuwa kama sio mali yao tena. Tunataka wananchi wa Mikumi wasikie ownership, waone ile mbuga kama ni ya kwao, tuwashirikishe wakae pale wajione kwamba ile mbuga ni ya kwetu na sisi ni watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa hivi kila kitu kinatolewa kinapelekwa Dar es Salaam, Mikumi hakuna kitu. Waheshimiwa Wabunge mnapita sana Mikumi pale mnaangalia wanyama mnapiga selfie, lakini mnashindwa kujua hata mnawasaidiaje wananchi wa Mikumi ambao mbuga ipo pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Serikali iliangalie kwa jicho pevu mnawaachaje watu wa Mikumi? Maana imekuwa kama kisiwa, tunakuwa maskini wakati tumebarikiwa kuwa na mbuga nzuri ya wanyama ndugu zangu. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali tunataka tutengeneze kijiji cha makumbusho. Kama Zanzibar wameweza kuwa na mji mkongwe, watu wakishafanya utalii pale wanakaa tunacheza ngoma tunakula misosi, tunakula vyakula vya asili na kuuza vitu vyetu ambavyo vitakuwa pale Mikumi. Kwa hiyo tunataka tutengeneze kijiji cha makumbusho pale Mikumi wazungu na ninyi mkitoka mbugani kuzunguka mnaweza kuzunguka Mikumi ili ku- boost uchumi wa watu wa mikumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Wizara wanatuacha kama kisiwa, hakuna shughuli yoyote ya utalii inayoendelea Mikumi. Tena nimesikia wametenga bilioni moja ambazo zimeenda kwenye vijiji vinavyohusika na mbuga, kwa Mikumi sijasikia, mimi ndiye Mbunge lakini sijasikia hayo madawati sijui walimpa nani au hiyo michango imekuwaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipouliza kuhusu giving back kwenye society kuchangia vitu vingine wamesema sasa hivi hawataki kujadili kuhusu majengo, hospitali na vitu vingine bali wanataka sasa hivi kuweka hela inayozunguka zunguka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine. Kuna ile Mikumi Lodge ambayo ilikuwa pale Mikumi, ndiyo iliyokuwa tegemeo la watu wa Mikumi kwenda kutalii, lakini sasa hivi ile hoteli ilibinafsishwa tukasikia imechomwa moto. Nataka Waziri akirudi hapa aje atuambie nini mustakbali wa ile Mikumi Lodge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye barabara inayopita Mikumi ya kilomita 50, takwimu zinaonesha mnyama mmoja anagongwa kila siku, wanyama 956 wanagongwa kwa miaka mitano, tangu 2011 mpaka 2015 wamegongwa wanyama 956. Nataka Serikali ije na majibu ituambie wanataka kufanya jambo gani kuhusu kukomboa hawa wanyama wa Kitanzania na ina mpango gani na hawa wanyama ambao wanagongwa kila siku na wanawaona na takwimu wanazo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumaliza na hayo, naomba kuwasilisha.