Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii nikiamini kabisa kuwa kupitishwa kwa Bajeti ya Wizara hii kutaleta changamoto chanya katika kutangaza na kuinua sekta ya utalii nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wa sekta ya utalii katika nchi yetu ni mkubwa sana kwa kuwa ni chanzo kikubwa cha uingizaji wa fedha za kigeni kupitia watalii mbalimbali wanaoitembelea nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu limejaaliwa kuwa na vivutio vya utalii kuanzia mbuga za wanyama (national parks) na mapori ya akiba (game reserves), utalii wa mali kale, fukwe mbalimbali zenye mandhari nzuri na zenye kiwango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto lukuki hasa katika mapori ya akiba yakiwemo mapori ya akiba ya Kigosi Moyowosi ambavyo kimsingi yanazo changamoto nyingi hasa miundombinu ya barabara za viwanja vya ndege na huduma za hoteli za kitalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kujenga barabara za kudumu kuyaunganisha mapori yetu haya ya Kigosi na Moyowosi kuanzia Kata ya Iponya, Wilayani Mbogwe kuunganisha na makao makuu ya mapori huko Kifura katika Wilaya ya Kibondo Mkoani Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ikifunguliwa na ikaimarishwa itasaidia sana shughuli za ulinzi wa wanyama pori kwani doria zitaweza kufanyika kwa urahisi hivyo kudhibiti uwindaji haramu hasa ujangili unaofanywa na waharibifu kutoka ndani na nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, uwepo wa barabara za uhakika katika mapori haya kutasaidia doria zitakazosaidia kuyabaini makundi makubwa ya mifugo yaliyovamia mapori haya na kuharibu ikolojia ya mapori haya mazuri na tegemeo la Taifa katika ukuaji wa sekta ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uwepo wa Shirika la Ndege lenye ndege zake za uhakika zenye kufanya safari zake katika Mataifa mbalimbali duniani kutasaidia kuvitangaza vivutio mbalimbali tulivyonavyo hapa nchini. Hii itaongeza idadi ya watalii wanaotembelea hapa nchini na kuvitembelea vivutio hivi na hivyo kuchangia pakubwa katika Pato la Taifa na pengine kusaidia kuwavutia wageni wawekezaji katika sekta hii kutoka katika mataifa ya nje tajiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, ni jukumu la Serikali na Bodi ya Utalii nchini kuhakikisha kuwa vivutio hivi vingi tulivyonavyo vinatangazwa duniani kote ili viweze kuwezesha watalii wengi zaidi kuja hapa nchini na kuchangia katika upanuzi wa ukuaji wa uchumi wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.