Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, huyu ambaye amenijalia afya na nguvu ya kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu na kuweza kuchangia bajeti ambayo iko mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nikupongeze wewe mwenyewe na tutaendelea kukuombea dua sisi Wabunge wote kwani unatosha. Kwa kuwa sisi wengine ni Masharifu basi naamini hakuna kitu kibaya ambacho kitakupata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niendelee kumpongeza Waziri wa Fedha na timu yake kwani bajeti yake kwa kweli ni nzuri na inatia moyo. Tuna uhakika sasa kwamba tunakwenda kwenye Tanzania mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kuchangia suala la kilimo. Nchi yetu inasema kilimo ni uti wa mgongo, lakini inasikitisha tunaposema kilimo ni uti wa mgongo, kilimo hiki kimetengewa bajeti ya shilingi trilioni 1.56, bajeti ambayo ni ndogo sana, haikidhi haja. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu sasa Tukufu iongeze bajeti hii kwani kama tunategemea uchumi wa viwanda, uchumi wa viwanda hautoki sehemu nyingine zaidi ya kwenye mazao ya kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu zinanyesha mvua za msimu, niishauri Serikali yangu sasa ijenge mabwawa kila maeneo ili kuweza kukinga mvua zile na wakulima wetu waweze kulima kilimo cha umwagiliaji. Kama alivyosema viwanda vinategemea kilimo kwa maana kwamba malighafi zinatoka kwenye kilimo, kwa mfano kule kwangu kuna maeneo mengi sana lakini ni kame, kwa maana hiyo tukiyajengea sasa mabwawa ina maana tutalima kilimo cha umwagiliaji na tutaongeza mnyonyoro wa thamani kwenye mazao yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna asiyejua kwamba Lushoto ni ya kilimo cha mboga mboga na matunda lakini kilimo kile wanalima kwa mazoea. Niiombe Serikali yangu ipeleke ruzuku za pembejeo kwenye kilimo cha mboga mboga na matunda. Wenzangu wote wanaposema ruzuku basi mimi kwa Wilaya ya Lushoto kwa kweli mboga mboga zile na matunda hayajawahi kupata ruzuku. Niishauri Serikali yangu sasa kama ina nia ya dhati, basi iweze kuwezesha kilimo kile kiweze kupata pembejeo za ruzuku.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niingie kwenye afya. Wakati tuko kwenye mchakato wa kampeni tulikuwa tunanadi Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwamba kila kijiji kitajengwa zahanati na kila kata itajegwa kituo cha afya. Leo hii katika bajeti nimeona tu mambo ya dawa na madeni ya MSD na vinginevyo lakini sijaona zahanati hata moja wala kituo cha afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kuangalia wananchi wetu kule vijijini kwa kweli ni masikitiko makubwa sana. Laiti ningekuwa na uwezo ningemchukua Waziri wa Fedha akaenda moja kwa moja kwa wananchi wale awaone kwani kuna wananchi kule hawajui hata hospitali. Wananchi wale kwa kweli wako kwenye mazingira magumu, wanalala chini, leo hii ukimchukua ukisema umpeleke hospitalini, kwa kweli hata mwili wake umekakamaa kama mbao. Hata umchome sindano ina maana haingii, sasa huyo unategemea nini, lakini mtu yule amekosa huduma. Niiombe Serikali yangu iende moja kwa moja kwa wananchi wale ili waweze kupata huduma.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tumeongea suala la walemavu, lakini tumeangalia walemavu wa mjini wale ambao tunawaona lakini wa vijijini wala hawajafikiwa. Niombe sasa katika bajeti ya walemavu basi iende moja kwa moja kwa wale walemavu wa kule vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala zima la shilingi milioni 50. Tulikuwa tunapigia kelele kwamba jamani mkituchagua basi shilingi milioni 50 zitakuja tena kwa wakati kwa kila kijiji, lakini leo hii naona bajeti imetengwa tu kwenye mikoa 10. Niishauri Serikali yangu wasipeleke kwenye mikoa 10, watenge hata vijiji vitano vitano kwenye mikoa yote Tanzania Bara na Tanzania Visiwani. Sisi wengine tumeshajiandaa watu wetu tumeshaanza kuwapa pesa ya kufungulia akaunti mahsusi kwa ajili ya pesa hizi. Mpaka sasa ninavyoongea, nina vikundi zaidi ya 100 ambavyo nishavifungulia akaunti wanasubiri pesa hizi. Kwa hiyo, niiombe sasa Serikali yangu Tukufu iweze kupeleka pesa hizi kwa wakati ili nikirudi Jimboni wananchi wale wasije wakaniuliza maswali magumu ambayo nitashindwa kuyajibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye kodi ya bodaboda. Wakati Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli anapita alisema katika watu ambao nitawaangalia ni watu wa bodaboda, leo hii naona watu wale tunazidi kuwaongezea mzigo kwani walikuwa wanalipa Sh. 45,000/= sasa hivi wanatakiwa walipe Sh. 95,000/=. Hebu jamani hili tuliangalie kwa jicho la upendeleo kwani ndugu zangu itafikia hatua sasa bodaboda hawa hawatatuelewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kuongelea ushuru wa mitumba. Mitumba hii imeajiri wananchi wengi sana. Leo hii ukifika pale Dar es Salaam au nimtume Waziri wa Fedha pale Dar es Salaam ataona ma-godown ya mitumba ambayo inasafirishwa mikoa yote Tanzania. Niiombe Serikali yangu iondoe ushuru huu ibaki VAT ileile ya mitumba iliyokuwepo siku zote ikiongezwa ina maana tumewapa mzigo watu ambao hawastahili kubeba mzigo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia moja kwa moja niende kwenye suala la mifuko ya nailoni. Unapopiga marufuku matumizi ya mifuko ya nailoni unakuwa umepiga marufuku utunzaji wa mazingira kwani miche inaoteshwa kwenye mifuko ya nailoni. Kwa hiyo, anaposema mifuko ile ipigwe marufuku isitumike ina maana atakuwa amewaambia wananchi wasipande miti.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hii asilimia tano ya vijana na asilimia tano ya akinamama, tunaipeleka wapi kama wananchi wetu hawa hatuwasaidii ipasavyo. Tunawapa wananchi asilimia tano kwa ajili ya kupata mitaji ndiyo anakwenda kununua bodaboda ambayo ina kodi kibao, unategemea mwananchi huyu atafaidikaje? Mwananchi huyu tumembebesha mzigo ambapo ni sawasawa na kumpaka mafuta kwa mgogo wa chupa. Kwa hiyo, hebu ifikie hatua sasa Serikali yetu iliangalie hili kwa jicho la huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja.