Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, utunzaji wa misitu na maliasili yetu ni jambo la msingi sana. Kila Mtanzania ana wajibu wa kutunza na kuhifadhi mazingira. Wafugaji wapo ambao wanafuata sheria za nchi za uhifadhi wa mazingira yetu na wapo ambao ni waharibifu wa mazingira. Kuna haja Serikali kusimamia sheria katika kuhakikisha ufugaji hauathiri mazingira yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hao wafugaji ambao hawafuati sheria za uhifadhi wasisababishe wafugaji wote wakaonekana ni adui mkubwa wa hifadhi ya nchi. Lazima pia tujiulize ni kwa nini wapo baadhi wanafuata sheria na wengine wanakiuka sheria? Je, Serikali yetu imetimiza wajibu wake katika kuwasaidia wafugaji wetu? Sheria za nchi zinaangalia vipi hifadhi zetu za mapori zilizotengwa miaka hiyo, idadi ya watu waliokuwepo miaka hiyo na mahitaji yao ya ardhi, ikiwepo mahitaji ya ardhi kwa ajili ya makazi, mahitaji ya ardhi na idadi ya mifugo yetu iliyopo kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo haja ya kujiangalia upya kisheria kuweza kupata ardhi kulingana na mahitaji ili kuepusha mauaji, mapigano na kugombea ardhi katika maeneo mbalimbali. Wafugaji wasibezwe na kuonekana wao ni tatizo kubwa katika kuharibu mazingira. Naomba niulize, je, wafugaji na wakata mkaa nani anaharibu mazingira?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiwahukumu wafugaji kwa kigezo cha kwamba wao wanaharibu mazingira. Tuwatengee maeneo kisheria, tuwamilikishe tuone kama kweli watakiuka utaratibu na wataharibu mazingira. Nakubali wapo wafugaji wanaingilia maeneo ya wakulima na kusababisha uharibifu. Narudia, haiwezi kuwa wafugaji wote wapo hivyo. Isituondoe katika kutetea wafugaji wetu kupatiwa haki zao na wajibu wetu wa kuwapatia mazingira bora ya ufugaji wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji wangu katika Jimbo la Igalula, Kata ya Goweka Miyenze, Intende na Kigwa wanateseka sana na wanateswa na kusumbuliwa sana na askari wa maliasili, wakati mwingine ng‟ombe wanakua nje ya reserve sisi tunaita ujije, wanaswaga mifugo hiyo na kuiingiza reserve na kuwakamata na kuwatoza fedha nyingi au kutaifisha mifugo hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lote la Jimbo la Igalula halina eneo rasmi la wafugaji, lakini kuna mifugo mingi na pia wakulima wapo wengi lakini pia maeneo makubwa ya Jimbo yamo ndani ya hifadhi. Mgogoro wa eneo la kulimia, kufugia na makazi ni tatizo kubwa sana. Tunaomba wakulima wetu wapewe eneo la kufugia na kulimia ili kuondoa tatizo hili. Tulishaomba kumegewa eneo la kilometa nne katika eneo lililohifadhiwa katika Kata ya Lutende na Miyenze ili wapewe wafugaji na wakulima ili kuondoa adha hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiwabeze wafugaji wetu, ndiyo wapiga kura wetu, leo tusiwadharau na kuwabeza. Watengenezewe mazingira rafiki ili wasiwe tatizo katika uharibifu wa mazingira. Tuangalie wakata mkaa na mbao kama waharibifu wakubwa wa mazingira na si wafugaji wetu ambao wana haki pia katika nchi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wafugaji wangu wa Kata za Lutende, Miyenze, Kigwa na Goweko wapewe maeneo na wamilikishwe ili wapate eneo la kufugia mifugo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja kama wafugaji wetu wataheshimiwa na kuthaminiwa na si kuonekana wahalifu na watu wabaya kwa mazingira.