Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kuchangia hotuba hii kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Tunduru kuna hifadhi kadhaa za misitu ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Selous iliyopo Jimbo la Tunduru Kaskazini pamoja na Hifadhi ya Misitu ya Mwambesi, Muhesi na kadhalika. Mwaka huu tembo wamekuwa wakipita katika hifadhi hizo na kuzagaa katika vijiji mbalimbali kama Mtina, Angalia, Mchesi, Kazamoyo na Kalulu na kuharibu mazao ya wananchi na wanadai malipo ya uharibifu huo wa tembo bila mafanikio. Kumekuwa na malalamiko mengi ya wakulima ambayo hayajafanyiwa kazi na Idara ya Wanyamapori, wanyama hao wanasumbua sana hivyo kuna uhitaji mkubwa wa watumishi wa Idara ya Wanyamapori ili kusaidia kufukuza wanyama hao waharibifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Tunduru Kusini kumekuwa na kero kubwa ya fisi kuua watu. Mpaka sasa watu wawili wameuawa na fisi na watu wawili wameuawa na mamba katika Mto Ruvuma na wawili wamejeruhiwa lakini utaratibu wa kulipwa fidia unachukua muda mrefu. Mpaka sasa wahanga hao hawajalipwa, mbaya zaidi majibu wanayopewa yanawakatisha tamaa. Ni vyema utaratibu wa kuwalipa wahanga hawa wa wanyamapori ukafanyiwa marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, TFS inashirikiana na Watendaji wa Vijiji kukata miti/magogo bila kufuata utaratibu wa kisheria na wanashirikiana na wafanyabiashara kukata miti hovyo bila kufuata utaratibu. Kwa mfano, katika Kijiji cha Semeni na Muungano, mfanyabiashara mmoja amekata magogo bila ridhaa ya mikutano mikuu ya vijiji hivyo na hata ushuru wa vijiji hivyo haujalipwa na kuna mgogoro mkubwa unafukuta na wanataka viongozi wa Halmashauri wa Kijiji na Mtendaji kupelekwa mahakamani. Hivyo, TFS inamaliza misitu ya Tunduru kwa kuruhusu magogo na mbao kukatwa hovyo bila kufuata utaratibu wa kisheria na sasa wanakata magogo Kijiji cha Machemba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya hifadhi za misitu na wakulima. Ni vyema mipaka ya hifadhi hizo ikaangaliwa upya ili kutoa maeneo kwa wakulima kutokana na ongezeko la watu mfano Muhesi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyakazi wa hifadhi na wanyamapori kutumia nguvu kubwa kuwanyanyasa watu kwa kuwapiga, kuharibu mazao yao, kuwanyang‟anya vitu vyao bila makosa. Ni vyema wakatumia ustaarabu katika kuwaelimisha wakulima badala ya kutumia nguvu. Ni vyema sheria ikatumika zaidi badala ya nguvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Operesheni Tokomeza. Jambo hili limekuwa mradi wa watu kwani kila mwaka wanaokamatwa ni watu walewale, wanateswa, wanapigwa, wanatoa rushwa ili waachiwe bila kupelekwa mahakamani. Ni vyema basi watuhumiwa wote wapelekwe mahakamani wakachukuliwe hatua badala ya kila mwaka wanakamatwa, wanateswa, wanawekwa ndani, wanatoa rushwa, wanaachiwa bila kuwapeleka mahakamani. Jambo hili linasababisha wananchi kuichukia Serikali yao bila sababu. Inaonekana kuwa umekuwa mradi wa watu fulani badala ya kufuata utaratibu. Ni vyema utaratibu wa kisheria ukafuatwa na haki za binadamu zikazingatiwa zaidi. Hakuna anayependa uharibifu unaofanywa, bila kuwachukulia hatua makundi mengine yanajitokeza, ila wakifungwa watu wataogopa kujishirikisha na biashara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kutenga maeneo ya hifadhi ni vyema elimu na mikutano ikafanyika katika vijiji husika ili kuondoa migongano na migogoro ya kutoelewa manufaa ya misitu. Naamini wananchi wakipewa elimu migogoro hii itapungua kwa kiasi kikubwa na hifadhi zisaidie vijiji vinavyopakana ili kutoa imani na nguvu ya watu wa maeneo hayo kulinda hifadhi hizo. Hifadhi zikisaidia vijiji jirani vijiji vingine vitahamasika katika kuanzisha hifadhi zao ili kupata manufaa wanayopata wenzao.