Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata fursa hii. Kwanza naitumia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii, lakini nawashukuru sana wananchi wa Wilaya ya Ukerewe kwa kuniamini na kunituma niwawakilishe kwenye chombo hiki muhimu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mchango wangu utajikita kwenye maeneo kadhaa. Nikianza na eneo la Afya; Mpango ulioletwa katika Bunge ni Mpango wa Maendeleo kwa ajili ya wananchi kwenye nchi yetu na kaulimbiu ni kutengeneza Tanzania ya Viwanda, lakini hatuwezi kutengeneza Tanzania ya Viwanda kama tutakuwa na jamii yenye afya dhaifu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la Afya kwa mfano nikiongelea kwenye eneo langu la Ukerewe; Ukerewe ni kisiwa. Kwa ujumla tuna visiwa zaidi ya 30; visiwa kama 38 hivi, lakini huduma za afya kwenye eneo la Ukerewe ni mbovu sana, kiasi kwamba ikitokea dharura kwa mfano, tuna hospitali ya Wilaya pale, ina matatizo makubwa, wahudumu wachache na tukizingatia mazingira ya jiografia ile, watumishi wengi wanapangiwa kwenye kisiwa kile hawaendi.
Kwa hiyo, naomba katika mipango yenu mliangalie jambo hili na hasa watu wa Utumishi kwamba watumishi wanaopangwa kwenye maeneo ya visiwa kama Ukerewe mhakikishe kwamba wanafika kwa ajili ya kuwahudumia kwa sababu Ukerewe ni eneo muhimu kama yalivyo maeneo mengine katika nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu zaidi, ukizingatia kwamba ni kisiwa, tuna usafiri wa meli pale. Kutoka Ukerewe kuja Mwanza, tunatumia zaidi ya masaa matatu, ni masaa matatu kama na nusu hivi. Kwa hiyo, ikitokea dharura, mtu akipata tatizo la dharura la kiafya, kuletwa Mwanza ni tatizo kubwa sana. Wakati fulani tulileta mapendekezo ikaletwa ambulance boat, cha ajabu ambacho tulitegemea kwamba itakuwa ni speed boat, badala ya kutumia chini ya masaa matatu, boti natumia masaa manane kwa ajili ya kumsaidia mgonjwa.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Wapi na wapi? Kwa hiyo, pendekezo langu kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Ukerewe, hebu tusaidieni ambulance boat ili kusaidia huduma za kiafya kwa wananchi wa Ukerewe waweze kushiriki kwenye shughuli za maendeleo na kuimarisha uchumi wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile bado katika mgao wa watumishi kama nilivyosema ni jambo muhimu sana, watu wa utumishi hakikisheni kwamba kwenye maeneo yaliyoko pembezoni kama Ukerewe, basi watumishi wakipelekwa wanafika kwenye maeneo yale wanawasaidia wananchi wa maeneo yale waweze kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuliongelea ni suala la miundombinu. Tuna barabara inayotuunganisha na maeneo mengine kama Bunda. Tuna barabara ya Bunda, Kisorya, Nansio mpaka Ilangala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu uliowasilishwa nimeona tu eneo la Kisorya, Bunda. Sijaona mwendelezo wa kwenda Nansio, Ilangala, kitu ambacho ni muhimu sana kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Ukerewe. Kwa sababu tunapoongelea habari ya Tanzania ya Viwanda tunahitaji tujenge uchumi wa wananchi na hatuwezi kujenga uchumi wa wananchi hawa kama miundombinu ina matatizo na mojawapo katika miundombinu hiyo ni eneo la barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara hii wakati itakapokuja na Mpango, ioneshe ni mpango gani uliopo juu ya ujenzi wa barabara hii ya Bunda - Kisorya - Nansio –Ilangala. Barabara hii ijengwe kwa lami ili kuimarisha uchumi wa wananchi wa Ukerewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuliongelea ni eneo la uvuvi. Uvuvi ndicho chanzo kikubwa cha uchumi wa wananchi wa Kanda ya Ziwa na specifically eneo la Ukerewe kama Wilaya. Tunazungukwa na Visiwa na ajira kubwa kwa wananchi wa Ukerewe, ni Sekta ya Uvuvi, lakini uvuvi huu kama chanzo kikubwa cha mzunguko wa pesa na kuimarisha uchumi wa wananchi wa Ukerewe, inakabiliwa na changamoto nyingi sana kubwa; ambapo Mheshimiwa Waziri katika Mpango wako, kwa kushirikiana na Wizara inayohusika na masuala haya ya uvuvi, mwangalie namna gani mnaweza mkawasaidia wavuvi wa Ukerewe ili angalau waweze kuimarisha mazingira yao ya kiuchumi na kujenga uchumi wa Kitaifa kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wa Ukerewe wanapata shida kubwa sana, kimsingi katika eneo lote la Ziwa Victoria; wanafanya shughuli zao hawana uhakika na usalama wa maisha yao; wanafanya shughuli zao huku wanavamiwa, wananyang‟anywa rasilimali zao kwenye Ziwa Victoria; wengine wanajeruhiwa, wanapoteza maisha yao. Ni lazima Tanzania kama nchi, tufike mahali tuone umuhimu wa jambo hili, tuhakikishe usalama wa watu hawa ili waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi wakiwa wana uhakika na usalama wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, shughuli zao za uvuvi vile vile watu hawa wanapofanya shughuli zao, uvuvi unakuwa na tozo nyingi mno ambazo zinafanya hata kile wanachokipata, kisiwasaidie sana kuimarisha uchumi wao. Mvuvi mmoja anakuwa na tozo takriban 12, 13, leseni za uvuvi; mtu analipa leseni katika Wilaya moja, akienda Wilaya nyingine anatozwa tena leseni, kitu ambacho kinawaathiri sana kiuchumi. Ni lazima katika Mipango yenu mtakapokuja na Mpango wa jumla, mwangalie namna gani mnaweza mkasaidia watu hawa ili waweze kuwa imara kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Ukerewe kama visiwa, ni eneo ambalo ni very strategic tunaweza tukalitumia kwa ajili ya kuimarisha utalii. Maeneo mengine kwenye nchi nyingine wametumia visiwa kwa ajili ya kuimarisha pato la kiutalii kwenye nchi zao. Tunaweza tukaitumia Ukerewe. Kwa mfano, kuna eneo moja la Ukara kuna jiwe linacheza, ambalo kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya, mnaweza kuona ni namna gani tunaweza tukatumia vyanzo kama hivi kuvutia Watalii, ikasaidia kuongeza pato la nchi yetu. Kwa hiyo, naombeni mlichukue na muweze kulifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado kuna changamoto kwenye eneo la usafiri. Kama nilivyosema, sisi tunaishi katika Visiwa, lakini tuna meli moja ya Serikali ambayo ni chakavu. Tulikuwa na meli ya MV Butiama, miaka mitano sasa haifanyi kazi. Wananchi wanasafiri kwa shida kweli kweli na wala hatuoni kama kuna utaratibu wowote au mpango wowote wa kutengeneza meli ile na kuwasaidia Wananchi wa Ukerewe.
Kwa hiyo, napenda kusikia wakati mtakapokuja na Mpango wenu, tujue kwamba ni mpango gani mlionao juu ya kuimarisha hali ya usafiri kwa wananchi wa Ukerewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuliongelea kwa sababu naona muda siyo rafiki, ni juu ya suala la umuhimu wa Halmashauri katika ujenzi wa uchumi ya nchi yetu. Halmashauri hizi kama tutazitumia na hasa kwa kuimarisha watu walioko katika Halmashauri, ni bahati mbaya sana kwamba katika nchi hii, kwa sababu tunaziita Local Government, tunahisi kwamba hata watu waliopo kule, basi ni local tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuzitumie Halmashauri hizi kwa ajili ya kuimarisha uchumi wetu. Halmashauri hizi haziwezi kuwa imara kama hatutaimarisha Viongozi wa Serikali za Mitaa. Kwa sababu tunaongea habari ya kujenga uchumi, lakini tunapojenga viwanda, tunaimarisha mazingira, kuna watu watahitaji kusimamia shughuli kule chini. Kuna Wenyeviti wa Viijiji, Wenyeviti wa Vitongoji, tuwaimarishe ili waweze kusaidia kujenga uchumi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naomba kuwasilisha.