Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kuweza kuchangia hotuba hii kwa maandishi pia naiunga mkono na kushauri yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuishukuru Serikali kupitia Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kutoa elimu bure kwa kuchangia madawati katika Wilaya zinazopakana na hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua na kuthamini uhifadhi wa wanyamapori na faida yake kwa Taifa ambapo unachangia 25% ya Pato la Taifa katika sekta ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapaswa iendelee kutoa elimu katika jamii inayoishi karibu na hifadhi na wananchi waone/wapate faida kutokana na hifadhi. Wawekezaji wamekuwa wakitoa michango ya maendeleo katika Pori la Akiba la Makao lakini mazingira yanaonesha wananchi hawaelewi mwekezaji anatoa kiasi gani cha fidia, ipo haja taarifa ya mapato na matumizi yasomwe katika vijiji vinavyounda Jumuiya za Hifadhi ya Wanyamapori (WMA) ili wananchi wasiendelee kumchukia mwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na mgogoro wa wananchi na mwekezaji wa Mwiba Holding Company katika Pori la Makao na magazeti yamekuwa yakiandika habari mbalimbali kutoka pori hilo lililopo Wilaya ya Meatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro huo ukiuangalia kwa nje kuna mgongano wa maslahi hivyo kuendelea kuiathiri Wilaya ya Meatu. Mimi nikiwa Mbunge Viti Maalum kutoka Mkoa wa Simiyu na ninayehudumia Halmashauri ya Wilaya ya Meatu nilifika kuongea na wananchi (viongozi) wa kijiji cha Makao mgogoro huo unazungumzika pia zipo sheria za nchi zinaweza kutumika.
Naiomba Serikali itoe tamko kuhusu mwekezaji Mwiba Holding Company ili wananchi wa Wilaya ya Meatu waweze kupata msimamo kuhusu mwekezaji katikati ya mwezi Aprili, 2016 wakati wa kikao cha wadau wa maendeleo ya Wilaya. Baraza la Madiwani lilishindwa kupokea ahadi ya mchango katika mfuko wa maendeleo kwa kuwa bado kuna mgogoro. Serikali itakapotoa suluhu itasaidia sasa kama Wilaya kuweza kushirikiana katika shughuli za maendeleo na pia kuweza kushirikiana katika shughuli za maendeleo na pia wananchi wakazi wa Wilaya ya Meatu walioajiriwa na Mwiba Holding Company waweze kujua hatma ya ajira zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Wizara ya Maliasili na Utalii kuharakisha mchakato wa matumizi bora ya ardhi ndani ya hifadhi ili wananchi waweze kulima na kuchunga mifugo. Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka 2015 aliahidi wananchi akiwa Jimbo la Meatu kuwa tatizo hilo la malisho litapatiwa suluhisho.
Pia niishauri Serikali kutokana na ongezeko la mifugo na wananchi, athari ya mabadiliko ya tabia ya nchi maeneo mengi katika Mkoa wa Simiyu yamekuwa makame kwa kipindi kirefu hivyo Serikali iangalie upya mipaka ya hifadhi katika Wilaya ya Bariadi, Busega, Itilima na Meatu ili kupata suluhu ya migogoro ya wafugaji na hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kifuta machozi/fidia; kumekuwepo na tatizo la wanyama pori kuwaua wananchi mfano; mtoto Malangwa Kasenge mwenye umri wa miaka tisa wa Kijiji cha Mwaukoli, Wilayani Meatu aliuawa kwa kuliwa na fisi mnamo tarehe 03/05/2013 lakini hadi leo familia haijalipwa kifuta machozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upo uharibifu wa mazao mashambani kutokana na tembo na nyati katika maeneo tofauti na wakati tofauti katika Wilaya ya Meatu na yamefanyiwa tathimini lakini hadi leo wananchi hawajalipwa fidia au kifuta machozi na sijaona katika bajeti ya Wizara ya Fedha imetengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tathimini ilifanyika kwa kuzingatia Sheria Uhifadhi wa Wanyamapori Namba Tano ya mwaka 2009 (The Wildlife Conservation Act, No. 5 of 2009) na kanuni yake (The Wildlife Conservation rates of Consolation Payment). Hivyo naiomba Serikali ifanye fidia kwa wananchi hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inapaswa irejeshe asilimia 25 ya uwindaji wa kitalii ya mapato katika Halmashauri, lakini marejesho haya yamekuwa ni ya kusuasua pia yamekuwa yakitofautiana mwaka hadi mwaka, naiomba Serikali yafuatayo:-
Kwanza Halmashauri ijue ni kiasi gani kinapatikana kutoka katika hifadhi inayoizunguka Wilaya ili kuweza kujua stahili zao na pili, Serikali irejeshe kikamilifu asilimia 25 ya uwindaji wa kitalii katika Halmashauri. Naunga mkono hoja.