Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba hii. Kwa kuwa ni mara ya kwanza kabisa kuweza kuchangia katika Bunge hili la Kumi na Moja, nachukua nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Busanda kwa kuendelea kuniamini tena wakanipa ridhaa katika awamu hii. Napenda kuwahakikishia kwamba nitaendelea kufanya kazi kwa nguvu zote ili kuweza kuwatumikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kupongeza huu Mpango wa mwaka 2016/2017. Ninachopenda zaidi ni kusisitiza suala la reli ya kati. Nazungumzia suala la reli kwa sababu ni injini ya uchumi. Bila ya kuwa na reli, uchumi wetu hauwezi kukua kwa sababu hatuwezi kusafirisha mizigo kutoka Dar es Salaam kwa njia ya barabara, kiasi kwamba mizigo mingi inasababisha barabara zetu ambazo tumezitengeneza kwa fedha nyingi kuharibika kwa haraka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kabisa kwamba hii reli ya kutoka Dar es Salaam kwenda Tabora, Mwanza, kutoka Tabora kuelekea Kigoma; kutoka Isaka kuelekea Keza na nyingine zote, naomba Serikali ituletee Mpango Mkakati, namna itakavyoweza kufanya ili kuweza, kutengeneza reli hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la maji. Naomba katika Mpango huu, Serikali iwekeze Mpango Mkakati wa uhakika, kwa suala la maji, kwa sababu maji ni tatizo kubwa sana hasa vijijini kwa wananchi wa Tanzania. Katika Jimbo la Busanda, pengine ni asilimia kumi tu ya wananchi wanaopata maji safi na salama. Kwa hiyo, nachukua fursa hii kuomba Serikali inapoleta mpango mkakati, ihakikishe suala la maji, linakuwa ni la kipaumbele kikubwa sana kwa sababu maji ni uhai. Hatuwezi kuwa na mapinduzi ya viwanda bila kuwa na maji ya uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa zaidi katika Mkoa wetu wa Geita tumebahatika kuzungukwa na maji ya Ziwa Victoria. Hebu Serikali basi ifikie hatua, iangalie uwezekano tuweze kupata maji ya uhakika kutoka Ziwa Victoria. Tayari katika Mji wa Geita, tumevuta maji kutoka Ziwa Victoria, kwa hiyo, basi Serikali iangalie uwezekano hata sisi vijijini tuweze kupata maji ya uhakika hasa maeneo ya Busanda na Sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile upande wa afya, napenda kuishauri Serikali iangalie katika Mpango wake wa mwaka 2016/2017, katika Mikoa mipya hatuna Hospitali za Rufaa. Katika Mkoa wa Geita, hatuna Hospitali ya Rufaa. Katika takwimu inaonesha kwamba vifo vya akina mama wajawazito, takwimu bado iko juu sana. Sasa ili tuweze kupunguza vifo vya akina mama wajawazito, ni vizuri Serikali iweke mkakati mkubwa wa kuwekeza katika upande wa afya hasa kwa kujenga Hospitali za Rufaa katika Mikoa ambayo hatuna Hospitali za Rufaa kama Mkoa wa Geita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo pia tuangalie katika Kata zetu, tuwe na hospitali, Vituo vya Afya, lakini pia katika Wilaya tuwe na Hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, naomba Serikali kweli iwekeze katika upande wa Afya, kwa sababu haiwezekani tukafikia uchumi wa kati bila kuwa na afya kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, naomba sasa katika Mpango Mkakati, nahitaji kuona kabisa kwa dhahiri kwamba Hospitali ya Rufaa ya Geita ipo kwenye Mpango, lakini vile vile Mpango wa Vituo vya Afya katika Kata zetu na Zahanati katika Vijiji vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwa upande wa elimu, nami naendelea kushukuru sana kwa huu mpango wa elimu bure. Baada ya kutangaza kwamba elimu ni bure, imeonekana hata watoto ambao wanapelekwa shule kuandikishwa Darasa la Kwanza, wameongezeka kwa kiasi kikubwa. Hili linaonesha jinsi ambavyo kumbe wazazi wengi walikuwa hawapeleki watoto wao shule kwa sababu wanaona kwamba ni gharama kuandikisha, ni gharama kulipa ile ada. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa hatua hiyo na juhudi ambazo imezifanya.
Naomba tu sasa Serikali iendelee kuongeza zaidi namna ya kuwezesha hii elimu bure, ili iweze kwenda kwa utaratibu sahihi ili watoto wetu waweze kunufaika zaidi katika elimu hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili sasa, ili tuweze kufikia katika uchumi wa kati, Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni amesisitiza sana suala la viwanda kwamba Tanzania yetu itakuwa ni Tanzania ya viwanda, nami hili suala nalipongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iwe na viwanda vya kimkakati kila Kanda. Kwa mfano, Kanda ya Ziwa, tuna mazao yetu, tuna dhahabu, tuna mifugo, tuna uvuvi; kwa hiyo, Serikali iangalie viwanda gani ambavyo itaweza kuwekeza ili wananchi wetu kulingana na mazao tuliyonayo tuweze kunufaika zaidi na vijana waliyo wengi waweze kupata ajira katika viwanda hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuangalie viwanda vya kimkakati katika Kanda ya Ziwa Viwanda vya Samaki; tunahitaji tuwekeze katika Viwanda vya Samaki, Viwanda vya Nyama na vile vile Viwanda vya Dhahabu, yaani kuongeza thamani ya dhahabu. Mkoa wa Geita tumebahatika dhahabu kwa wingi. Naomba pia Serikali katika mwaka huu wa fedha, tuangalie uwezekano wa kutoa maeneo ya kutosha kwa ajili ya wachimbaji wadogo, kwa sababu ndiko ambako vijana wengi wamejiajiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, kwa sababu hii imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana ya Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, lakini vile vile Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, naomba kweli mwaka huu Serikali iangalie uwezekano wa kutoa maeneo ya kutosha kwa ajili ya kuwapatia wachimbaji wadogo ili vijana wengi waweze kupata ajira katika shughuli za uchimbaji wa madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naiomba sana Serikali kwamba tunaupokea huu Mpango lakini iweke mkakati mzuri na itakapouleta vizuri tuone katika Mpango huu iguse hayo maeneo ambayo pengine hayajaweza kujionesha kwa dhahiri ndani ya Mpango ili basi tunapopitisha tuweze kuona kabisa kwamba Tanzania tunapiga hatua katika uchumi, kutoka uchumi wa chini kwenda uchumi wa kati kama ambavyo mategemeo na matarajio yetu yalivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa upande wa elimu…
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja, Serikali iendelee kutekeleza hayo.