Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo hayawezi kuwa maendeleo bila ya kuwa na maji safi na salama. Katika Jimbo langu la Chalinze kwa kipindi kirefu tumekuwa tunashughulika na mradi wa maji tumejitahidi kuhakikisha kwamba mradi ule sasa umefika katika awamu ya pili awamu ambayo imekamilika, lakini tunapoelekea katika awamu ya tatu nimeona kwamba ndani ya Mpango wa Maendeleo kitabu kizuri kabisa kilichowekwa na Dkt. Mpango kinaonesha kwamba wametenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha mradi wa maji wa Chalinze unafanyika. Ninachowaomba Mheshimiwa Waziri wa Maji atakapofika hapa atuambie juu ya jinsi gani amejipanga kwa kuhakikisha kwamba fedha za mradi ule zinafika haraka ili ujenzi wa awamu ya tatu upate kuanza mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo pia tunatambua maendeleo hayawezi kuwa maendeleo bila kuwa na viwanda lakini viwanda hivyo lazima vitegemee kilimo ikiwa ni kama sehemu ya kupatikana kwa malighafi hizo. Wamesema hapa wenzangu wanaotokea Tabora kwamba leo hii Tabora ndiyo wakulima wazuri wa tumbaku, lakini kiwanda kinachotegemewa kiko Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nafikiri muda umefika wa Serikali yetu kuwekeza nguvu zaidi katika kuhakikisha kwamba viwanda vinajengwa karibu na malighafi hizo ili hii taabu ya kupatikana malighafi ambayo zinasafirishwa muda mrefu isiwepo tena. Hata hivyo, siyo hilo tu ili kuhakikisha kwamba malighafi zinafika vizuri viwandani miundombinu ya barabara zetu na reli ni muhimu sana ikawekwa vizuri. (Makofi)
Niungane na wenzangu wanaozungumzia umuhimu wa kujenga reli ya Kati lakini pamoja na hilo pia reli inayokwenda Tanga ambayo inapita katika mashamba ya mkonge, lakini reli pia ya TAZARA inayopita katika maeneo makubwa yenye kilimo katika Nyanda za Juu Kusini nazo ni muhimu sana zikawekewa umuhimu katika kipindi hiki cha bajeti hii inayofuatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo katika ukurasa wa 31 imezungumziwa kuhusu jambo zima la elimu na afya. Ni kweli Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba inaweka mambo mazuri katika upande wa afya hasa za wananchi wetu wa hali ya chini sana. Niwapongeze sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu na rafiki yangu Dkt. Hamis Kigwangalla kwa kazi kubwa ambayo wamekwishaanza kuifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mipango yao mizuri ya kuhakikisha kwamba afya zinaendelea kuimarika katika maeneo ya vijiji vyetu na kata zetu, lakini uko umuhimu wa pekee wa kutambua pia kwamba ziko shughuli ambayo zimekwishaanza kufanyika, mimi nazungumzia zaidi katika Jimbo la Chalinze ambapo karibu vijiji vyote vina zahanati, lakini pia Kata Nane kati ya 15 zilizopo katika Jimbo la Chalinze zina vituo vya afya.
Sasa ninachoomba Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa kueleza ni vema akatuambia mpango gani walionao kuhakikisha kwamba vituo vyetu vya afya hivi ambavyo tumevianzishwa vinaendelea kuwa bora zaidi hasa kile cha kiwango ambacho tumenunua vifaa vyote lakini mkakati wa kukamilisha ile pale tunasubiri sana kauli toka kwao kama Wizara husika kwa maana nyingine tunazungumzia lugha ya kuja kukagua kwa hatua za mwisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo tunatambua umuhimu wa elimu ikiwa ni moja ya vitu ambavyo ni muhimu sana vikaangaliwa. Katika maeneo yetu sisi tunayotoka majengo yetu mengi miundombinu yake ni chakavu sana, ikumbukwe kwamba Bagamoyo ni moja ya Wilaya kongwe kabisa Tanzania ambapo shule zimeanza kujengwa siku nyingi na majengo yake yamekuwa chakavu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapokuja kuleta bajeti zetu za Halmashauri hasa katika eneo la elimu katika kuimarisha miundombinu yetu, tunaomba sana Wizara ya Fedha, Wizara ya Elimu mpate kuliangalia hili kwa jicho la karibu zaidi ili tuweze kupata fedha za kuweza kuimarisha elimu hii na vijana wetu wapate kuishi katika mazingira mazuri. Bila kufanya hivyo tunaweza kujikuta tunaibukia katika matatizo ya kwenda kuzika vijana wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kwa taarifa tu na nitoe pole sana kwa ndugu zangu wanaoishi katika Kata ya Kibindu au Kijiji cha Kibindu shule yetu imeanguka kule yote na vijana wetu zaidi ya 1,100 wako nje mpaka sasa hivi tunapoongea. Pia kwa kipekee kabisa niwapongeze wananchi wa Kibindu kwa hatua zao kubwa walizoanza za kuhakikisha kwamba wanajenga madarasa na mimi Mbunge wao nitakaporudi ahadi yangu ya kupeleka mifuko 1,500 iko pale pale ili kuhakikisha kwamba shule ile tunaijenga na wananchi wangu waanze kusoma hasa vijana wetu ambao ndiyo tunategemea kesho waje kuturithi mikoba hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo nizungumzie jambo zima la uchumi, wananchi wa Jimbo la Chalinze wengi wao ni wakulima na wako baadhi yao ni wafugaji. Tunapozungumzia ufugaji tunategemea sana uwepo wa machinjio yetu pale Ruvu yakamilike mapema sana. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alipata nafasi ya kuja pale, tulimsimulia juu ya ufisadi mkubwa unaofanyika pale lakini pia tukamwambia juu ya mambo ambayo yanaendelea na sisi pale wananchi wa Jimbo la Chalinze ni wakarimu kabisa hasa wananchi wanaoishi katika maeneo yanayozunguka hifadhi ile au ranch yetu ya NARCO pale Ruvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulimuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie juu ya hatua gani wamefikia baada ya mkutano mzuri tuliofanya pamoja na yeye na wananchi wa Kijiji cha Vigwaza, wananchi wa Kijiji cha Mkenge na wananchi wa vijiji vingine ambao vilio vyao kupitia Mbunge wao nilivisema siku hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo natambua pia upo umuhimu wa kumulikwa na umeme, nishati hii ni muhimu sana, wakati wa enzi za Mheshimiwa Waziri Profesa alifanya kazi kubwa sana kuhakikisha kwamba umeme unapelekwa katika vijiji vya Jimbo la Chalinze. Mimi binafsi yangu kwa niaba ya wananchi wa Chalinze nimshukuru, lakini pamoja na hilo mahitaji ya kujengwa na kuwekwa transfoma kubwa kwa ajili ya kuwapatia wananchi wa Kata ya Mbwewe, Kata ya Kimange, Kata ya Miono, Kata ya Msata na Kata nyinginezo zenye mahitaji kama haya hasa Kiwangwa ni mambo ambayo ni ya msingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba anapokuja hapa Mheshimiwa Waziri anayehusika na masuala ya nishati atuambie juu ya mikakati ambayo wamejipanga nayo kuhakikisha kwamba wanamalizia ile kazi ambayo walikwisha ianza katika eneo la Jimbo la Chalinze.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua pamoja na hayo pia iko kazi nzuri ambayo tulianza katika awamu iliyopita ya ujenzi wa bandari ya Bagamoyo. Nataka niliseme hili kwa sababu kumekuwa na kauli za sintofahamu zinazotoka kwa upande wa Serikali ambazo zimekuwa zinaripotiwa katika magazeti. Unaweza kuwa shuhuda katika gazeti moja miezi kama miwili iliyopita iliripoti kwamba ujenzi wa bandari ile hautokuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi binafsi nilipata nafasi ya kuzungumza na Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Waziri akanihakikishia kwamba ujenzi wa bandari ile upo na nifurahi kwamba nimeiona katika kitabu cha maendeleo. Hata hivyo, wananchi wangu wa Jimbo la Chalinze na Wilaya ya Bagamoyo hawana raha na wakati mwingine hata wakituangalia sisi viongozi wao wanakuwa wanapata mashaka juu ya kauli zetu hasa kwa kuamini kwamba tunakitetea Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa naye awahakikishie wananchi wa Wilaya ya Bagamoyo kwamba bandari ya Bagamoyo itajengwa kwa sababu bandari hii ni bandari muhimu na ni bandari ambayo imewekwa pale kimkakati. (Makofi)
Serikali ya Tanzania imekwisha fanya kazi yake ya kutathmini na kuwalipa fidia wananchi wa maeneo ya Pande-Mlingotini na Kata ya Zinga. Sasa iliyobakia ni kazi ya wawekezaji wa China na Oman kuja kuweka hela kwa ajili ya kuanzisha uchimbaji na ujenzi wa bandari hiyo. Nitahitaji sana kusikia kauli ya Serikali ili wananchi wetu wa Wilaya ya Bagamoyo wapate amani ya mioyo yao wakiamini kwamba maendeleo makubwa na mazuri yanakuja katika eneo lao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo nimalize kabisa kwa kuendelea tena kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Chalinze, maana sisi kwetu Chalinze ni kazi tu na kwetu sisi tunafanya kazi kwa ushirikiano, wananchi wanafanya kazi na sisi tunafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.