Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwanza sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, na viongozi wote wa Wizara hii, kwanza kwa hotuba nzuri waliotusomea imeifunika hotuba ya Kambi ya Upinzani, ndio maana mkawaona wamekuja na jazba kubwa mpaka mwisho mtu anakunywa maji, ili kutafuta sauti akwamue, aifunike speech ya Mheshimiwa Waziri, lakini ameshindwa na vilevile nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi ya Upinzani wamezungumza kwamba Mheshimiwa Rais anajifungia Ikulu, anashindwa kutoka nje. Nawaambia Mheshimiwa Dkt. Magufuli ndiye Rais bora duniani na ambaye ameweza kutekeleza sera zake, kwa Watanzania na hivi sasa ana sifika Tanzania nzima na nje ya nchi kwa sababu ya uwezo wake, na hapo anapokuwepo Ikulu si kwamba anakaa anafanya kazi, anatafakari nini cha kuwafanyia Watanzania kuwaondoshea madhila, lakini mimi ninajua wenzetu ninyi kazi yenu ni kupinga tu kila kilichokuwa kizuri kazi yenu ninyi kupinga, kila kinachotendeka kikiwa kimekaa sawa imekuwa sawasawa na mke mwenza, amelisifia kaburi la mke mwenzie, hili kaburi la nani zuri limependeza, alipambwa na mke mwenzie, ndio maana nikaona limekaa upande, ndio upinzani huo, wakati ameshalisifia anakuja analiponda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mabalozi. Mabalozi wetu wanafanya kazi nzuri, hata wao wanapokwenda nchi za nje, wanahemea kwa Mabalozi. Sasa leo imekuwaje maana yake baniani mbaya kiatu chake dawa, jamani hebu tuwe makini katika masuala yetu tunapozungumza. Maana yake wakati mwingine mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni, tusiwe kwa sababu kuna upinzani, ndio upinge kila kitu mengine mshukuru kwa sababu yanawafaeni na ninyi wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na suala lingine, kuna siku alisimama Mbunge akazungumza kwamba Zanzibar utalii wao kama hauna uendelezo wala hauna faida nao upo upo tu. Namwambia huyo Mheshimiwa kwamba Zanzibar hivi sasa bajeti yake anatumia pesa za ndani, hategemei za nje na kinachofanya hivyo ni kwa sababu utalii unaenda vizuri, karafuu anauza vizuri na ndio maana ikaweza kujitosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa utamkuta mtu anakurupuka anakuambia, Seif ndio atakuwa Rais atauweza uchumi, unajidanganya. Seif alitia mpira kwapani na Bwana Jecha alimpa uhuru mkubwa tu wa kugombea na alimuambia tarehe 20 Machi, 2016 uchaguzi kashindwa. Katia mpira kwapani, ninawaambieni msilolijua ni sawa na usiku wa kiza, tulieni Mheshimiwa Shein akamate madaraka aendelee nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa uchaguzi mwaka 2020, mwaka 2020 kama hamkuja basi tena tunaendelea, tunapiga more waliyojionea vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nitajikita katika diplomasia ya kiuchumi. Ninajua Wizara imejipanga katika kukuza diplomasia ya kiuchumi na kwenye kitabu chenu nimeona kwamba tayari mmejikita na mnakwenda vizuri. Nilikuwa nataka kusema hivi, kwa sababu Tanzania hivi sasa inataka kujikita katika viwanda, je, Wizara imejipanga vipi kutafutia masoko ya biashara ambapo kwa sababu tutakapojiingiza kwenye viwanda, lazima tuwe na masoko nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namtaka Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujumuisha, uniambie masoko ya nje tumejikita vipi ili kwa bidhaa zetu tuweze kuuza. Kwa kweli Tanzania inajikita katika mambo ya utalii, kwa sababu tunavyo vitu vinavyotufanya ili tuweze kuvutia watalii wetu. Kuna Mlima Kilimanjaro, kuna fukwe za Bahari za Zanzibar, kuna bustani ndani ya Bahari ya Hindi na hiyo wanakuja wanapoenda kuangalia, vilevile tuna mbuga za wanyama. Sasa ningekuomba na haya sasa myafanyie kazi ya kuyatangaza, msiwaachie Kenya ambao wakitoka wao ndio Tanzania wakatutangazia, wakati sisi tuna uwezo na uwezo huo najua Mheshimiwa Waziri unao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia ambalo sikuliona kwenye kitabu chake, mwaka jana tulizungumza kwamba kuna vijana Wazanzibari 13 mliwasomesha, ili baadae muwaajiri katika Wizara zenu au vitengo vyenu. Lakini kwenye kitabu chako sijaona hao vijana ambao wameajiriwa au hawakuajiriwa, umetuambia kwamba kuna watu wamestaafu, kuna watu wamemaliza muda wao, lakini hujasema vijana gani ambao tayari umewaajiri kama kutoka Tanzania Bara au Tanzania Visiwani. Sasa hivyo Mheshimiwa Waziri ningependa pia ukija unijulishe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kuhusu kitabu chako cha mwaka jana ukurasa wa 61; mlisema Wizara mnajikita katika kuweka vitega uchumi, kufanya wafanyakazi watakaokuwa nje ya taasisi yenu ambao watakua Ubalozi kupata sehemu zao za kukaa na ofisi zao za kukaa. Lakini sijaona kwenye kitabu chako maendeleo yake yamekuwaje kama kweli, maana ulisema mpaka mtakuwa na mapato katika sehemu za vitega uchumi, kwa kupata viwanja na majengo ambayo mengine mtaweza kukodisha. Sasa na hilo ningependa utakapokuja Mheshimiwa Waziri nipate kujua maendeleo yake yakoje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa sababu Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki makao makuu yake yako Zanzibar. Sasa hili lazima nitoe pongezi kwamba Zanzibar ambayo mmeipa kitengo kama mlivyosema kwamba Kamisheni ya Kiswahili Makao Makuu yake yatakuwa Zanzibar, ni katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ilianzia kuanzia mwaka 2014. Sasa hili kwangu ni pongezi na ninashukuru, na tutaendelea kuilinda, na tutaendelea kuilea kama tunavyoilinda na kuilea CCM, kwa maelezo hayo naunga mkono hoja.