Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Niungane na wenzangu kukupa pongezi kwa jinsi unavyoendelea kusimama imara na kuliongoza vizuri Bunge letu Tukufu. Sisi tupo pamoja na wewe na kwenye wengi kuna Mungu na kwenye Bunge hili sisi ndiyo wengi. Kwa hiyo, kaza buti na tunakutabiria kuna mambo mengine makubwa yatakujia mbele yako. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nichukue nafasi hii vilevile nimpongeze Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu Waziri wa Fedha kwa kuja na bajeti ambayo kwa kweli inaonyesha kuna matumaini kwetu sisi Watanzania. Kwa mara ya kwanza tumeona kwamba bajeti yetu ya maendeleo ni asilimia 40, haya ni maendeleo makubwa lakini tumeona jinsi gani bajeti hii inavyopunguza kero za wananchi. Mimi natoka Jimbo ambalo ni la wakulima wakubwa sana wa korosho, kuna tozo tano pale zimeondolewa, hongera sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nipongeze kwa ujasiri wa kutenga fedha nyingi kwenda Wizara ya Afya, karibu shilingi trilioni moja na bilioni mia tisa ambazo zitasaidia vilevile kulipa deni la MSD. Tunapolipa deni la MSD tuna uhakika sasa zahanati zetu, vituo vya afya, hospitali za wilaya na hospitali za rufaa za mikoa kutakuwa na dawa, wagonjwa wetu wakienda hospitali hawatarudi na cheti tu, watarudi na dawa. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nianze kuchangia hili suala la tozo tano. Kama nilivyosema, niendelee kuipongeza Serikali yangu ya Awamu ya Tano kwa sababu hii ilikuwa ahadi ya Mheshimiwa Rais wakati anaomba kura. Alisema kwenye korosho kuna kodi nyingi na akiingia Ikulu atapunguza na mwaka wake wa kwanza ameanza na hizi tozo tano na hiki kitabu kinasema kwamba hii ni awamu ya kwanza, kazi inaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri sasa, Serikali au Wizara ya Kilimo itoe mwongozo, sasa hivi kuna hofu na kuna maneno mengine kwamba kuondolewa kwa tozo hizi kutaathiri mfumo wa stakabadhi ghalani. Kwa hiyo, naomba sasa Wizara ya Kilimo itoe mwongozo kupeleka kule chini kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, mikoani na kwenye Vyama Vikuu vya Ushirika kwamba utaratibu gani utafuatwa kuhusu masuala ya usafirishaji wa korosho na minada ili tuwaondolee hofu wale ambao wanaanza kueneza maneno mengine kwamba kwa kuondosha tozo basi mfumo wetu wa stakabadhi ghalani utakuwa ni kifo chake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nitoe rai kwa wale wenzetu ambao wapo kwenye mfumo huu, mabadiliko yoyote yale lazima yalete hofu. Kwa hiyo, naomba sana wale ambao wanahusika na mfumo huu wa ununuzi wa korosho wajikite kuangalia the way forward na siyo kujadili kwamba tozo hii kwa nini itoke au isitoke, tuangalie mbele sasa baada ya kutolewa hizi tozo nini kifuate ili kuboresha uendeshaji wa mfumo wetu wa stakabadhi ghalani.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala langu la pili ni kuhusu CAG kuongezewa fedha. Bajeti ambayo amepewa CAG ni shilingi bilioni 44.6, hiki kiasi cha fedha hakitoshi. Ukiangalia kwenye fedha hizo kuna shilingi bilioni 12 ambazo ni za maendeleo lakini vilevile CAG ana deni ambalo amevuka nalo la shilingi bilioni nne kwa hiyo ukitoa kwenye hesabu hiyo bado fedha zake zinazidi kupungua. Hata hivyo, kwa maneno yake mwenyewe CAG wakati tunafanya discussion kule Dar es Salaam alisema kwa fedha hii sasa atashindwa kukagua Halmashauri 94. Sasa hebu piga hesabu, tuna Halmashauri 181, kama atashindwa kufanya ukaguzi kwenye Halmashauri 94, ina maana karibu nusu ya kazi yake hataikamilisha. Kama Halmashauri 94 hazitakaguliwa unajua ni athari gani ambayo itapatikana kwa sababu fedha zetu nyingi tunazipeleka kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna ahadi ambayo ilitolewa kwamba ataongezewa fedha kwenye mid-year review pengine Desemba. Kwa CAG kupewa fedha Desemba yeye haimsaidii kiutendaji kwa sababu kwenye ukaguzi kuna phases tatu na zinakamilika kabla ya Desemba. Januari mpaka Machi kwa CAG ni muda wa kuandika ripoti, kwa hiyo additional yoyote ya fedha mwezi Januari kwake haimsaidii kwenye ukaguzi. Kwa hiyo, naomba sana tusimpe fedha wakati wa kuandika ripoti, tumuongezee sasa ili CAG aweze ku-cover maeneo yake. Kwa sababu punguzo hili la fedha, kwanza hata scope ya ukaguzi itaathirika lakini hata ubora. Kama unavyofahamu kwamba chombo chetu hiki sasa kilishapata hadhi ya Kimataifa. CAG sasa anakagua taasisi za Umoja wa Mataifa, kwa hiyo, tusimshushe nguvu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende tena upande wa property tax ambayo sasa tumesema kwamba itakusanywa na TRA badala ya Mamlaka za Serikali za Mitaa. Niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba huko nyuma kulikuwa na policy paper ya Local Government Reform ilitolewa mwaka 1998, ina maeneo manne, mimi kwa sababu ya muda sitaki kuyataja mengine, lakini eneo kubwa ambalo ilitakiwa tutekeleze ni financial decentralization, lazima Mamlaka za Serikali za Mitaa tuzipe uwezo wa kifedha. Dawa ya mtu ambaye hana uwezo wa kukusanya siyo kumnyang‟anya, nilitarajia kwamba tungekuja na mbinu za kuziongezea uwezo Mamlaka za Serikali za Mitaa kukusanya lakini kusema hawana uwezo tupeleke TRA hiyo kwa kweli siyo solution. Tufanye kwa mwaka huu kwa sababu tumeshaamua hivyo lakini naomba sana Serikali yangu Tukufu tuangalie jinsi ya kuziwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kukusanya fedha za kutosha, zikikusanya fedha za kutosha basi wataweza kutoa huduma ambazo tunazitarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuwe na wazo la kuzipa Mamlaka za Serikali za Mitaa vyanzo ambavyo ni vya uhakika. Vyanzo vilivyobaki kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa havina uhakika na mapato yake ni ya kusuasua. Kwa hiyo, tuangalie kwenye suala la ugatuaji wa madaraka siyo kupeleka mamlaka tu kule, tupeleke na fedha. Hii inanikumbusha wazo la Mheshimiwa Oliver ambaye alisisitiza sana umuhimu wa kuwa na semina ya ugatuaji, semina ya D by D kwa Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Mawaziri kwa sababu sasa hivi inaonekana kwamba tunataka kurudi nyuma tulikotoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.