Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Ahmed Juma Ngwali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ziwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii japo kwa ghafla.
MWENYEKITI: Niichukue hiyo nafasi nimpe mwingine?
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Aah okay, aah usimpe! (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, lakini kabla ya kuchangia Mpango kuna jambo naomba niliweke sawa, japo nilitamani sana Mwanasheria Mkuu angekuwepo tukaenda sawasawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya (1) naomba niisome, inasema: “Tanzania ni nchi moja na ni Jamhuri ya Muungano.” Kwa hiyo, sisi hapa kama Wazanzibari tumo ndani ya Tanzania na ni Watanzania. Hakuna Mzanzibari kwa mujibu wa Katiba kwa sababu Tanzania ni dola moja tu, wala Zanzibar siyo dora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, unaposema Wazanzibari wakatatue matatizo yao, huo ni ubaguzi ambao umekatazwa na Katiba. Haiwezekani tatizo linatokea Arusha, mkasema kwamba tatizo hilo ni la Waarusha tu, haliwahusu watu wa maeneo mengine; linawahusu Tanzania nzima. Kwa hiyo, hili naomba niliweke sawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili watu wanasema kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haihusiki kabisa na masuala ya Zanzibar, lakini naomba niisome Katiba ya Zanzibar… nani kaikimbiza tena! Aah! (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niisome. Ukisoma Katiba ya Zanzibar Ibara ya 119… imechukuliwa bwana! (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 119(14) inasema kwamba; “Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar itashirikiana na Tume ya Taifa katika kuendeleza shughuli zao za uchaguzi.”
Sasa ikiwa Tume ya Uchaguzi ya Taifa ambayo ni ya Jamhuri ya Muungano inashirikiana na Tume ya Zanzibar, kwa hiyo, hata uchaguzi uliofutwa, Tume ya Taifa imeshiriki katika kufuta uchaguzi ule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kitu kimoja cha busara sana; tumetoka mbali sana na Taifa hili, tuna maingiliano ya muda mrefu; tuna maingiliano toka karne ya 16 na nyuma huko, tumeishi kwa udugu sana, tumeishi kwa mapenzi, tumeishi kwa furaha wala hakuna tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na matatizo mengi yanayojitokeza madogo madogo, lakini yamekuwa yanapatiwa ufumbuzi na mambo yanakwenda. Leo isifike wakati Mpango huu ukawa hautekelezeki kwa sababu ya mtu mmoja tu peke yake. Nikimtaja mtu anayeitwa Jecha Salum Jecha, mseme laanatullah, kwa Kiswahili “laana za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.” (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi mbalimbali ambao wanaitakia mema nchi hii, naomba nimtaje kwa heshima kubwa Komredi Salim Ahmed Salim, alisema kwamba lazima tatizo la Zanzibar lipatiwe ufumbuzi, lakini pia Mheshimiwa Bernard Membe aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje katika Serikali ya Awamu ya Nne, kwa ufasaha kabisa alisema tatizo hili lazima tulipatie ufumbuzi. Vilevile Jaji Warioba, watu hawa ni watu wenye heshima kubwa katika nchi hii, ni watu ambao tunawaheshimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tatizo lisichukuliwe kama ni tatizo dogo tu. Niwaambie kitu kimoja; tunapanga mipango hapa, hata Kenya na Burundi wana mipango wanapanga, inakuwa sasa? Mara Garissa limelipuka! Mara hapa, mara pale, kwasababu mnaonea watu waliokuwa hawana silaha. Watu waliokuwa hawana silaha, wanatafuta namna.
Kwa mfano, Waziri Mkuu aliyepita alikaa pale wakati Mheshimiwa Mama Asha Bakari, Marehemu, Mungu amrehemu, alipokuwa akisema nchi hii haipatikani kwa vikaratasi. Sasa ukisema nchi hii haipatikani kwa vikaratasi, maana yake ni kwamba, huo ni ugaidi, tutafute utaratibu mwingine. Hata Mheshimiwa Lukuvi naye aligusagusa sana kwenye swali hili, mtu mbaya sana yule! Tuendelee lakini. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme kwa busara kabisa, viongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakae pamoja tuone namna gani wanalishughulikia tatizo la Zanzibar na uchaguzi usifanyike. Uchaguzi kwanza ukae pembeni, usifanyike tuone ni namna gani Serikali hii inatatua tatizo letu hili, kwa sababu mkiacha uchaguzi ule ukifanyika, na sisi tumetangaza rasmi kuwa hatushiriki kwenye uchaguzi ule; ninyi mnaona ni busara hiyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnaona ni busara, endeleeni na uchaguzi, lakini niwaonye kitu kimoja, Serikali mnanisikia vizuri sana, mpo hapo. Haya makundi yote yaliyojitokeza kama Islamic State, Al-shabab, Boko Haram yalitokana na kudhulumiwa haki zao. Haya hayakuwa bure! Hayakujitengeneza tu, yalijitengeneza baada ya kudhulumiwa. Sasa msije mkatuharibia nchi yetu kwa kumlinda mtu mmoja tu. Serikali ya Muungano mmewabeba sana Serikali ya Zanzibar! Mmewabeba mwaka 2000… (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ngwali!
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Naam!
MWENYEKITI: Huo mfano ulioutumia, chimbuko la hayo makundi uliyoyataja wewe, una ushahidi kwamba misingi yake ndiyo hiyo?
MWENYEKITI: Unaweza ukatuthibitishia hapa?
MWENYEKITI: Mimi nakusihi sana, ufute tu hiyo kauli yako, tusifike mbali.
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nafuta kauli yangu, haina shida. (Kicheko/Makofi)
MBUNGE FULANI: Taarifa, Mheshimiwa Mwenyekiti.
MWENYEKITI: Taarifa! Keti tu Mheshimiwa Ngwali, muda wako umekwisha.