Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana. Awali ya yote, nimpongeze sana Mheshimiwa Msigwa kwa hotuba yake nzuri sana pamoja na kwamba wengine imewakwaza lakini kwetu ni nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na jambo ambalo limezungumzwa sana na niseme kwamba last time nilikuwa kwenye Kamati ya Mambo ya Nje, suala la Chuo cha Diplomasia ni la msingi sana, wamezungumza wengi lakini naomba niende kwa maswali tu. Chuo hiki kilikuwa kipanuliwe na eneo walikuwa wanafuatilia kule Bagamoyo. Nataka Waziri anapokuja kujumuisha atuambie suala hilo limeishia wapi maana silioni mahali popote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni suala la diaspora, ni jambo la kusikitisha sana. Bahati nzuri nimeangalia hotuba ya mwaka juzi, ya mwaka jana, hotuba ya mwaka 2014 inaonesha kwamba walikuwa wanafanya utafiti kujua Watanzania wangapi wanaishi nchi za nje, two years ago. Leo Mheshimiwa Waziri anatuletea taarifa kwamba Watanzania waishio nchi za nje wanakadiriwa kuwa zaidi ya milioni moja. Tulitaka kujua idadi kamili ni wangapi ili tujue ni kiasi gani wanaweza kuleta nchini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi kama Nigeria leo inaingiza dola za kimarekani bilioni 21. Sawa Nigeria ina watu wengi lakini Kenya jirani zetu, bilioni 1.4 mwaka 2015, Tanzania wanaingiza kiasi gani, hatuna kiasi. Kwa hiyo, kama walivyosema wenzangu nadhani hii Wizara diplomasia iko kisiasa zaidi lakini haiko kiuchumi Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine na tulilizungumza sana ni suala la kuhakikisha kwamba Mabalozi wetu wote walioko nje ya nchi wanakuwa angalau na mkutano mmoja ili wajue huko kwingine kuna fursa kiasi gani wakae pamoja wapeane taarifa. Nina taarifa kwamba nchi nyingine wanafanya hivyo, nimekuwa Finland nimeona kila tarehe fulani Mabalozi wa nchi zote wa Finland wanarudi nyumbani ili kutoa feedback ya mambo gani au changamoto gani wanakutana nazo na fursa gani wanakutana nazo. Hapa Tanzania tuna utaratibu gani, ni mwaka gani Mabalozi wetu wote wamewahi kuitwa wakakutana ili angalau wazungumzie fursa na changamoto wanazozikabili ili tuone nchi yetu inaendelea kiuchumi zaidi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kusikitisha, nimepitia kitabu cha maendeleo, Wizara kubwa namna hii ina shilingi bilioni nane (8) tu fedha za maendeleo, unless kuna fedha nyingine. Ukiangalia hotuba ya Waziri anazungumzia suala la kupanua Balozi, kwa fedha zipi? Hizi ambazo tunazo tumeshindwa, ukienda kwenye Ubalozi wa Zambia ni matatizo, ukienda kwenye Balozi nyingine nyingi ni matatizo, bahati nzuri tumekwenda, ni matatizo makubwa, mpaka hata Ubalozi wetu Marekani ni shida. Kama mwenzetu Idd Amin aliweza kujenga jengo kubwa sana pale New York Tanzania tumeshindwa na alijenga miaka ile, ni jambo la kusikitisha, tunaendelea kupanga. Tulisema ni kwa nini makampuni kama NSSF, NHC wasiingie ubia na Serikali kupitia Wizara hii ili waweze kujenga nyumba huko nje lakini naona jambo hili nalo limekufa kifo cha kishujaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za nyuma akiwa Waziri Membe mwaka 2014 na huko nyuma tuliongelea sana suala la dual citizenship (uraia pacha) lakini leo halionekani mahali popote na ni kama vile limekufa. Mheshimiwa Waziri anajua watu kwenye Diaspora walilalamikia sana suala hili la uraia pacha na tukawa tumeambiwa na Mheshimiwa Membe kwamba jambo hili linafanyiwa utafiti, litaendelea kushughulikiwa na litaingizwa kwenye Katiba iliyokuwa inapendekezwa lakini leo hakuna kitu, sasa tuwaeleweje jamani? Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba tujue status ya uraia pacha ikoje sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kuzungumza ni kwenye masuala ya ndoa. Tunajua kwamba ukiwa mwanaume Mtanzania, ukioa raia wa nje automatically yule mama anakuwa raia wa Tanzania lakini mwanamke wa Kitanzania akiolewa na mzungu au mtu mwingine ni tatizo kubwa. Sasa tunaomba kujua hii double standard inakuwaje kwa sababu hawa akinamama wananyimwa haki yao ya msingi. Kwa hiyo, naomba hilo lizingatiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kulizungumzia ni suala la mjusi (dinosaur). Wizara hii pamoja na mambo mengine inashughulikia pia masuala ya kiutalii, huduma za jamii, elimu na kila kitu. Tuliambiwa kwamba yule dinosaur akiletwa hapa kwenye hili jengo hataenea, hiyo siyo issue yetu wala siyo hoja. Hoja ya msingi tunataka kujua, toka huyu mjusi amepelekwa huko Ujerumani ameingiza kiasi gani na Wizara hii ikishirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii wana utaratibu gani kuhakikisha kwamba tunapata fedha? Suala kwamba hakuna jengo la kuweza kumweka halituhusu, ilitakiwa Serikali ihakikishe kwamba inatafuta sehemu ambapo huyo mjusi akija atawekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani tupoteze fedha nyingi hivyo za kutoka nje, watu wanaenda pale maelfu kwa maelfu kumwangalia yule mjusi lakini Watanzania hatupati chochote. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri akishirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii wa-make sure kwamba wanatuletea utaratibu kidiplomasia ni jinsi gani huyo mjusi ama analetwa au Tanzania tunapata kiasi gani na hicho kiasi hakianzii leo, kinaanzia miaka hiyo waliyompeleka? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili lilizungumzwa sana hapa Bungeni na Mheshimiwa Fatuma Mikidadi mpaka maskini na Ubunge hajapata. Kwa hiyo, ili kumuenzi mwenzetu hebu tuhakikishe hili jambo linafikia mwisho wake. Bahati nzuri ni Mbunge wa CCM kwa hiyo naamini suala hili litashughulikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niongelee suala la itifaki. Siku za nyuma Bunge jipya linapozinduliwa tunakuwa na semina ya masuala ya itifaki ili Waheshimiwa Wabunge waelewe ni mambo gani yanatakiwa na yanakatazwa na tulikuwa tunaletea Chief of Protocol anatupa semina. Sasa hivi utaona mtu amevaa suti bado ina label anaingia Bungeni anaenda popote, utaona mtu ana begi lake bado lina nylon yuko nalo tu. Kwa hiyo, haya ni mambo ambayo kwa kweli kama Wabunge tunapaswa kuyajua siyo tu hapa na Wabunge wengi wanasafiri nje, wanaenda hivyo hivyo. Kwa hiyo, nadhani ni wakati muafaka watuhakikishie kwamba hilo jambo linafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kabisa ni suala la mtangamano wa Afrika Mashariki. Nilikuwa naangalia hivi ni lini tutafikia huo mtangamano wa Shirikisho la Afrika Mashariki kama kila leo tunaongeza nchi. Mimi najua kuna wengine wakiulizwa ni nchi ngapi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki watasema ni tatu, nne, tano na wengine watasema sita. Naomba kujua Sudan tayari imeshakuwa member au haijawa, maana yake mimi hata sijui. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaangalia vigezo gani, maana nilikuwa nafikiri, pamoja na geographical location lakini vilevile masuala mazima ya tabia yaangaliwe. Kwa hiyo, nadhani imefika wakati sasa tuangalie mambo haya. Pia napenda kujua ni nani wanaotoa kibali cha nchi kuwa ndani ya shirikisho?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.