Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nami nichukue nafasi ya kwanza kabisa, kwanza kukushukuru wewe na kukupongeza sana kwa kazi nzuri unayoifanya. Tunakupa moyo usife moyo, chapa kazi, sisi tutakuunga mkono.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue nafasi hii nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa. Nataka nimpe moyo, kwa kawaida hakuna anayependa kulipa kodi, wote tunachukia kodi, lakini ni ukweli usiopingika kwamba bila kodi hakuna maendeleo. Kwa hiyo, endelea kuchapa kazi, yale tutakayokushauri, tutakushauri na yale mengine ambayo utaona ni muhimu kuyatekeleza basi yasimamie utekelezaji wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme maeneo mawili makubwa. Eneo la kwanza ni eneo la utalii. Sote tunafahamu kwamba utalii ni moja kati ya maeneo yanayoingizia sana pesa nchi mbalimbali. Na hivi sasa duniani Sekta ya Utalii ndiyo sekta kubwa ya kuingizia fedha nchi nyingi duniani. Bahati nzuri mazingira ya Tanzania ni mazuri sana kiutalii. Tunavyo vivutio vingi vya utalii, lakini naomba niseme kwamba sisi Tanzania pamoja na kuwa na vivutio vingi vya utalii, lakini bado hatujavitumia kikamilifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tunatumia sana maeneo mawili kwa utalii. Eneo la kwanza ni eneo la Mlima wa Kilimanjaro na eneo la pili ni la Mbuga za Wanyama, lakini ukienda nchi nyingine duniani, hazina milima wala mbuga za wanyama, lakini zina utalii mkubwa sana. Kwa hiyo, nashauri kwamba tujaribu kujikita kwenye maeneo mengine ya utalii ili kuikuza nchi yetu katika eneo la utalii. Yapo maeneo mengi sana kama tutaamua kujikita tutapata watalii wa kutosha sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mmoja kati ya watu waliopata bahati ya kutembea nchi mbalimbali na nimekwenda kujifunza maeneo mbalimbali jinsi wenzetu wanavyofanya utalii katika maeneo tofauti na yale tunayofanya sisi. Yako maeneo ya upandaji wa milima yenye miamba. Wanasema milima yenye miamba watu wa technical mountain climbing. Wanaipanda milima ile na sisi bahati nzuri tuna milima mingi sana yenye miamba, kule Songea tuna Mlima wa Matogoro ambao hauna utalii lakini tunaweza tukaingiza utalii wa kupanda milima yenye miamba tukapata nafasi kubwa sana ya kuingiza watalii nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ipo sehemu nyingine ya utalii wa historia (Historical Sites). Tuna maeneo mengi sana ya kihistoria; kule Songea tuna maeneo ya Majimaji, Vita ya Majimaji ina historia yake kubwa, ukienda Kalenga kuna historia kubwa, kuna maeneo mbalimbali nchini, lakini hatujafika mahala tukayatangaza vya kutosha na tukayatumia kama maeneo ya utalii. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba tujikite kwenye maeneo mengine ya utalii, ili kuikuza nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini uko utalii wa mila na desturi. Nilipata bahati ya kwenda nchi inaitwa Nepal, kwenye Mji Mkuu wao pale Kathmandu kuna maonesho ya mila. Kuna nchi nyingi zinakwenda kuona mila za Kihindi, historia za Kihindi; wanaingiza pesa nyingi sana kwa sababu ya utalii wa kimila. Sisi Tanzania tuna mila nyingi sana, tuna historia nyingi sana lakini hatuzitumii kwa ajili ya kuingiza watalii ndani ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, yako maeneo mengine mengi, kwa mfano kuna utalii wa Samaki (Acquarium) huu utalii umekua sana, ukienda Dubai saa hizi, wana samaki zaidi ya 33,000 kwenye eneo moja ambalo watalii wanakwenda kuwaona. Kuna nchi mbalimbali zina utalii wa namna hii, nenda Canada, Japan, Ujerumani sisi tuna aina nyingi sana za samaki ambazo tunaweza kuzifanyia utaratibu zikawa ni eneo moja la utalii. Kwa hiyo, naomba Serikali hebu ijaribu kuchambua, maeneo muhimu kwa ajili ya kuweka utalii katika vyanzo vingine tofauti ili kuipatia nchi yetu mapato ya kutosha yanatokana na utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, uko utalii wa wanyama; kule Kilimanjaro kuna sehemu inaitwa Ndarakwai, kuna tembo ambaye ukimweleza anakusikiliza, unampa maelekezo yoyote yale, lakini wale tembo hawatumiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kathmandu kuna tembo ambao wanafanyiwa utalii duniani, watu wanakwenda kupanda tembo; unapanda tembo anakupeleka kwenye maonesho mbalimbali, kwenye misitu unalipa gharama za utalii. Kwa hiyo, nafikiri bado tuna wanyama ambao tunaweza tukawatumia wakasaidia kuweza kuimarisha na kuukuza utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, vitu muhimu; ndugu yangu Shonza alikuwa ananiambia hapa, kule Mbozi kuna jiwe linaitwa Kimondo ambalo tunaweza tukalitangaza kwa nguvu sana tukaimarisha utalii. Nilikuwa nataka nilisisitize hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni juu ya Mlima Kilimanjaro. Mlima Kilimanjaro una sifa duniani kote na unatuingizia pesa nyingi sana, lakini nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri mlima ule unaingiza watu ambao hata moja ya kumi ya watu wanaotaka kuja kuuona hawaufikii kileleni. Tuna uwezo wa kuupanua ule mlima ili ufanye utalii wa watu wengi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa kuja Mlima Kilimanjaro ni lazima uupande, katika kuupanda zipo sifa za kupanda. Kwanza lazima upende kutembea, lakini lazima uwe na umri unaoruhusu kutembea. Kwa hiyo, watu wengi wanapenda kuja Mlima wa Kilimanjaro hawana uwezo wa afya, ama umri wake hauruhusu. Kwa hiyo tunachoweza kukifanya, kwa sababu Mlima Kilimanjaro unajulikana duniani, ni kuwahakikishia watalii kwamba watu waweza kuja kuutalii ule mlima hata bila kuupanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimjulishe, Mheshimiwa Waziri, labda niliseme na hilo kwamba nilishakuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, nilifanya ziara China. China nilizungumza na kampuni ya Serikali kwamba watujengee mnara. Mnara ambao wangetujengea watu ambao afya au interest zao haziruhusu kupanda mlima wangekuja kupanda kwenye mnara huo na tulishakubaliana wajenge mnara wa mita 600, ambapo ukishapanda una uwezo wa kuu-view mlima wa Kilimanjaro kwenye kiganja chako; na kwa hiyo unatembelea Mlima wa Kilimanjaro kwa kutumia mnara huo. Kwa hiyo tunaweza tukafanya hivi na tukapata watalii wengi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda China iko minara ya namna hii, inajaa watu wengi sana, inatumika kwa utalii wa mjini na inasaidia sana hata kufanya shughuli za utafiti. Bado kwa kutumia mnara huo unaweza ukatengeneza sky train ya kukufanya ufike Mlima wa Kilimanjaro bila kupanda kwa utaratibu wa kawaida uliopo sasa. Kwa hiyo, tunaweza kuona hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana hebu Serikali ijaribu kujikita chini kuangalia namna tunavyoweza kuikuza Sekta ya Utalii ndani ya nchi yetu ili iingize mapato zaidi ya hivi sasa yanayoingia.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.