Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza kabisa nikupe pole kwa yaliyotokea leo lakini umeonesha ujasiri mkubwa na sisi tupo pamoja na wewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hotuba nzuri aliyoitoa hapa wakati analizindua Bunge hili. Hotuba ambayo ilionesha mwelekeo wa Serikali yetu kwa miaka mitano inayokuja. Hotuba ambayo ina matumaini makubwa kwa Watanzania kutoka hapa tulipo kuelekea kwenye maendeleo zaidi. Pia ameonesha kwa vitendo kwamba sasa tunaelekea kuzuri, ametenda alichonena. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru pia kwa kifupi wananchi wa Igalula kwa imani kubwa waliyonionesha mimi kwa kunileta katika Bunge hili, nawaahidi sintowaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka na mimi nijikite katika maeneo mbalimbali ambayo Mheshimiwa Rais ameyagusia wakati wa hotuba yake. Nianze na eneo alilolizungumzia kuhusu tatizo la maji. Katika kitabu chake cha hotuba ukurasa wa 6 na 22, Mheshimiwa Rais amezungumzia shida ya maji kubwa tuliyonayo katika maeneo mbalimbali aliyopita. Inawezekana kila eneo lina shida kubwa ya maji lakini sisi katika Mkoa wetu wa Tabora tuna shida sana ya maji. Tumekuwa tunaahadi ya kupata maji kutoka Ziwa Victoria. Mradi huu ni mkubwa na inawezekana ikachukua muda mrefu mpaka kufikia kukamilika na wananchi Mkoa wa Tabora kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mradi huu ni mkubwa, tunatarajia Serikali yetu itautekeleza lakini kwa sasa katika Mkoa wetu wa Tabora mvua nyingi zinanyesha, maeneo mengi yamepata mafuriko kwa sababu yale maji hayakingwi vizuri kwa matumizi ya binadamu na matumizi mengine. Mimi nataka kuishauri Serikali ione umuhimu wa kutega mabwawa kwenye maeneo mbalimbali ili kuondoa shida kubwa ya maji tuliyonayo katika Mkoa wa Tabora. Maeneo mazuri yapo ya kutega mabwawa haya na baadhi yameshategwa kwenye maeneo machache, yameonesha kusaidia sana kupunguza kero ya maji katika eneo letu la Mkoa wa Tabora. Niombe sana Wizara ya Maji iliangalie hili badala ya maji haya kupotea bure basi yaweze kutegwa na kuweza kutusaidia kwa matumizi mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 11 amezungumzia hali ya barabara katika maeneo yetu. Amesema kuna haja ya kukamilisha barabara zinazotengenezwa na kuziimarisha zile ambazo zimeharibika. Naomba niizungumzie barabara ya kutoka Tabora - Nyahua - Chaya - Itigi. Barabara hii kwa asilimia zaidi ya 65 inapita kwenye Jimbo langu la Igalula lakini mpaka sasa imekamilika kipande cha Tabora – Nyahua, kilometa 89 kutoka Nyahua - Chaya hazijashugulikiwa kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuja hapa nilikwenda TANROADS kuongea na Meneja, anasema shida kubwa ni consultant anashindwa kukamilisha haraka kazi yake ili tender itangazwe. Designing zinatofautiana na watu wa TANROADS. Niiombe Serikali, kwa sasa ninavyozungumza barabrara ya Itigi - Chaya inapitika, ukifika Chaya - Nyahua imekatika na mvua mara nane. Haipitiki, imesababisha matatizo makubwa, mabasi yaliyokuwa yanapita njia ile sasa yanazungukia Singida – Nzega, wanaongeza zaidi ya kilometa 180 kwa kuzunguka na siyo mabasi tu hata wananchi wa kawaida waliokuwa wanatumia njia hii sasa haipitiki. Hata mimi kwenda Jimboni kwangu inabidi nikitoka Tabora nipite Singida kuingia tena Jimboni kwangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba hatua za haraka zichukuliwe ili kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika. Vilevile tuombe Serikali iweke nguvu ya kutosha kwa sababu tumehakikishiwa pesa zipo, huyu consultant amalize kazi haraka ili mchakato wa kumpata mkandarasi na kuanza kujengwa barabara hii uanze kufanyika haraka sana. Kiuchumi tunaitegemea sana barabara hii, kuna haja itengenezwe haraka sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie suala la viwanda. Katika ukurasa wa 11 Mheshimiwa Rais amesema viwanda tutakavyowekeza ni vile ambavyo malighafi yake inapatikana hapa hapa nchini. Ukizungumzia Mkoa wetu wa Tabora, kuna uwezekano wa kujenga viwanda zaidi ya viwili au vitatu. Zaidi ya asilimia 75 ya tumbaku inayolimwa katika nchi yetu ya Tanzania inatoka Tabora lakini cha ajabu Kiwanda cha Tumbaku kimejengwa Morogoro.
Niiombe Serikali, kwa kuwa ahadi ya Mheshimiwa Rais ni kwamba tutajenga viwanda katika maeneo ambapo mazao yanapatikana, sisi tunalima tumbaku, tunaomba kiwanda cha tumbaku kijengwe katika Mkoa wetu wa Tabora. Itasaidia ajira, itasaidia kukuza uchumi wa mkoa wetu na itasaidia pia ubora wa zao letu la tumbaku kwani kusafirishwa kutoka Tabora kuja Morogoro linazidi kuharibika kwa hiyo ni vema tukatengenezewa kiwanda pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunarina asali nyingi katika Mkoa wetu wa Tabora. Tunaomba tutengenezewe kiwanda cha kusindika asali katika Mkoa wetu wa Tabora. Nisikitike tulikuwa tuna Kiwanda cha Nyuzi sasa kimekufa. Tunaomba pia Kiwanda cha Nyuzi katika Mkoa wetu wa Tabora kiweze kushughulikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kilimo kwa sababu muda unakwenda haraka na hasa nitazungumzia tumbaku. Mkulima wa tumbaku bado hajasaidiwa vya kutosha, kero zake zimekuwa nyingi na utatuzi wake umekuwa wa taratibu sana. Tunaomba Serikali itatue haraka kero za mkulima wa tumbaku ili kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja katika Mkoa wetu wa Tabora. Wananchi wengi wanalima tumbaku na wanaitegemea sana kwa uchumi wao na kuendesha maisha yao. Vilevile Serikali inaweza kukusanya kodi ya kutosha kutokana na zao la tumbaku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunalima mpunga mwingi Tabora. Tunaomba tutengenezewe miundombinu ya kuweza kufanya kilimo cha mpunga kisaidie wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji wetu wanahangaika, hawana maeneo ya kufugia. Tunaomba Serikali ichukue hatua kuwasaidia wafugaji katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, suala la umaskini ambalo Mheshimiwa Rais amelizungumza. Kuna programu ya kupeleka shilingi milioni 50 katika kila kijiji. Tunaipongeza Serikali yetu kwa wazo hili. Tunachoshauri ni kwamba utengenezwe utaratibu mzuri wa kusimamia fedha hizi zisije zikawa kama zile za Mfuko wa Jakaya, zilipotea bila ya maelezo mazuri. Serikali ina nia nzuri itengeneze utaratibu mzuri ambao utasaidia pesa hizi zije kuonekana zinasaidia vijana wetu katika kufanya shughuli zao mbalimbali. Wataalamu waende wakawafundishe vijana wetu kule vijijini namna ya kuendesha biashara ndogo ndogo, lakini na menejimenti pia ya pesa hizi ili zitumike kusaidia vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda ningeweza kuzungumza mengi lakini kwa leo naomba niishie hapa, nashukuru sana. (Makofi)