Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nichangie kwenye hoja hii ambayo iko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jina langu naitwa Mashimba Ndaki, natoka Maswa Magharibi. Nachukue nafasi hii pia kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa neema zake na uwezo wake ambao umeniwezesha kufika kwenye Bunge lango Tukufu. Pia nachukue nafasi hii kuwashukuru wananchi na wapigakura wangu wa Jimbo la Maswa Magharibi kwa kunipa kura nyingi ambazo hazikuwa na maswali; na hata wapinzani wetu walinyoosha mikono. (Makofi)
Nawashukuruni sana wapigakura wa Jimbo la Maswa Magharibi, kama nilivyokuwa nikiahidi na kama nilivyokuwa nikisema, niko hapa kuwawakilisha, kuwatumikieni na tutafanya kazi pamoja, tumeshaanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia kumpongeza sana Rais Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa namna ambavyo ameshaanza kazi baada ya kulihutubia Bunge hili. Tunamtia moyo kwamba sisi Wabunge wa Chama cha Mapinduzi tuko pamoja naye, tutasaidiana naye ili ndoto ambayo anayo kwa ajili ya Watanzania iweze kukamilika. Tunajua anayo ndoto kubwa na inaeleweka mpaka inatisha upande ule wa pili. Tutakusaidia Mheshimiwa Rais kama Wabunge ambao tumeaminiwa na wananchi kwa kipindi hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri ambao wameshateuliwa na kuanza kazi zao. Kazi yenu ni njema, endeleeni, msikatishwe tamaa na maneno ya wachache wetu ambao wao siku zote ni kukatisha tamaa tu. Kazi yenu ni njema, tuko pamoja. Mahali ambapo mtahitaji msaada wetu, kuweni na uhakika mtaupata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwa namna ambavyo mmeanza kwa kasi wengi hawapendi; na hasa hii slogan ya hapa kazi tu, wengine wanajaribu kuipotosha na kusema yasiyokuwepo kwenye hiyo slogan, hata hivyo, endeleeni! Hata ninyi mliofunga mageti, mimi nawapongeza. Wenzetu wanasema eti mngeanza kwa kujengea watu uwezo. Unamjengea mtu uwezo wa namna ya kuja kazini kwa muda uliopangwa! Unataka kumjengea mtu uwezo kwamba atoke saa ngapi kazini anapofika! Hii itakuwa nchi ya namna gani? Endeleeni, chapeni kazi, tuko pamoja! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze sasa mchango wangu kwenye hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango. Mapendekezo yake ni mazuri na yana kitu ukisoma unaona kabisa kwamba nchi yetu sasa inaelekea wapi. Mheshimiwa Waziri, hongera sana kwa mapendekezo haya na Mpango huu ambao umeuleta mbele yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni tofauti sana ukisoma na maoni ya wenzetu. Nimesoma sana ndani yake, huwezi kusema utapata kitu hapa cha ushauri. Sijui kama Mheshimiwa Waziri amesoma na kwamba labda kapata chochote, kwa sababu imejaa malalamiko, manung’uniko, hakuna ushauri wowote ndani yake, ina maneno tupu, wala hakuna takwimu. Sasa sijui kama upinzani wako serious kama wanakuja na vitu vya namna hii Bungeni na wanataka kweli kuongoza nchi hii na kuifikisha mahali pazuri. Wapinzani ninyi ni watu wazuri sana, lakini kuweni serious…(Makofi)
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Taarifa imefika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka sasa nichangie tu kwa haraka haraka katika mapendekezo haya ambayo yako mbele yetu. Kuhusiana na suala la viwanda, naunga mkono kwamba sasa tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda. Nakubaliana kabisa na hayo yaliyoandikwa lakini nataka tu kuweka angalizo kwamba bado tunavyo viwanda kwenye nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mapendekezo ya Mpango sijaona mazingira mazuri yanayojengwa kwa ajili ya viwanda ambavyo tayari vipo na vinajikongoja au vinapata shida kwa sababu ya changamoto mbalimbali.
Kwa hiyo, nilikuwa nasihi kwamba wakati tunatengeneza na kuimarisha Mpango huu kuelezwe bayana kwenye Mpango ni kwa namna gani mazingira yataboreshwa ili viwanda vilivyopo na ha ta hivyo vitakavyokuja viweze…
MWENYEKITI: Muda umekwisha.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.